KWA KINA NA SULTAN TAMBA.

Sekta ya burudani nchini Tanzania imekuwa ikipitia mabadiliko mwaka hadi mwaka,siku hadi siku. Kuna wakati burudani ya disko ndio ilishika hatamu.Hii ilienda sambamba na sinema,zile za yale majumba ya sinema ya enzi zile.Hapa nazungumzia kina Drive Inn Cinema,New Chox,Empress na wenzao. Kisha kuna wakati taarabu ikaja juu.Ukawa ni mwendo wa “mipasho”.Kina Nasma na Bi.Khadija wakawa ndio gumzo la mjini. Haukupita muda muziki wa kizazi kipya ukashika hatamu.Bongo Flava ikawa ndio ya kuamkia na ndio ya kulalia.

 

 

Lakini kabla Bongo Fleva haijapotea (bado inatamba) enzi za filamu za kitanzania,zenye lugha yetu wenyewe,waigizaji wetu wenyewe,zikarejea upya. Hivi sasa Bongo Fleva na Filamu za Kitanzania zinabakia kuwa burudani za aina yake nchini Tanzania. Lakini ni muhimu kukumbuka kwamba filamu za kitanzania zina historia ndefu.Tangu enzi zile za kina Fimbo ya Mnyonge,YombaYomba,Harusi ya Mariam nk. Kinachofanyika hivi sasa ni kurejesha enzi zile.

 

Mtu mmoja ambaye amechangia kwa kiasi kikubwa kuzirudisha zama zile za filamu za kitanzania ni Sultan Tamba ambaye ni mtunzi wa hadithi,mwandishi wa magazetini na vitabuni na pia muongoza filamu. Filamu yake ya iliyoitwa Girlfriend ya mwaka 2002 ambayo aliwashirikisha wasanii kama T.I.D, kundi la East Coast na baadhi ya wacheza filamu walio maarufu sasa kama Monalisa na wengineo, ilichangia sana kuamsha upya ari ya kutengeneza tena filamu za kitanzania.Wakati huo filamu za kutoka nchini Nigeria zilikuwa zishaanza kuotesha mizizi miongoni mwa wapenda filamu nchini Tanzania.Mpaka hivi leo bado zinapendwa nchini Tanzania ingawa hivi sasa zinakumbana na ushindani mpya wa filamu za kitanzania.

 

Hivi karibuni tulifanya naye mahojiano na Sultan Tamba ambapo tumezungumzia mambo mengi kuhusiana na kazi zake za uandishi,utunzi wa hadithi za filamu,uongozaji filamu na mengineyo.

 

Muhimu zaidi alitueleza juu ya ujio wa filamu yake mpya ambayo ameiita Soka la Bongo.Filamu hiyo inatarajiwa kutoka takribani wiki tatu zijazo.Inahusu nini?Kwanini ameiita Soka la Bongo? Unawajua top six wake kwa upande wa waigizaji filamu nchini Tanzania?Ana maoni gani kuhusu wanamuziki kugeuka kuwa waigizaji? Anasemaje kuhusu uhuru wa vyombo vya habari nchini Tanzania? Upo? Unajua ameanza kuandika tangu akiwa na umri gani? Kwa hayo na mengineyo mengi fuatana nasi katika mahojiano yafuatayo;

 

BC: Kwanza naomba uniambie historia ya maisha yako kwa kifupi.Ulizaliwa wapi,ukasomea wapi na mambo kama hayo.

 

ST:Nilizaliwa Dar es Salaam, Ilala mwaka 1973, nilisomea shule ya msingi inayoitwa Ilala Boma, iliyopo jirani kabisa na ofisi ya Mkuu wa mkoa wa Dar es Sakaam. Nilipomaliza darasa la saba niliendelea na sekondari hadi kidato cha pili, halafu sikuweza kuendelea tena kutokana na uwezo wa kifedha wa kifamilia kuwa chini, Huo ulikuwa ni mwaka 1991

 

Nikajiingiza kwenye mambo ya uchoraji kwenye magazeti, kuanzia gazeti la Uhuru na magazeti ya Cheka na Wasaa, kisha kuanzia hapo nikajikuta naweza mambo mengi ya magazeti na nikaendelea mpaka hivi sasa. Hapo katikati nikawa najiendeleza kwa kuchukua kozi mbalimbali katika mambo ya habari na mawasiliano na pia za kiingereza.

 

BC: Unatoka kwenye familia ya watoto wangapi?

 

ST: Natokea kwenye familia ya watoto 11 lakini saba tuko baba mmoja mama mmoja. Wengine baba alizaa na wake wengine.

 

BC: Ulipokuwa mdogo unakumbuka ulitaka kuwa nani ukubwani?Na unakumbuka nini zaidi kuhusu maisha yako ya utotoni

 

ST: Nilitamani sana kuwa mwandishi.Utotoni nakumbuka zaidi nilivyokuwa napenda kujifungia chumbani nikiwa na lundo la makaratasi yangu niliyokuwa nayanunua sokoni.

 

BC: Ulikuwa ukijifungia unaandika au kuchorachora tu wakati huo.

 

ST:Kwanza sikumbuki ni lini nimejua kusoma. tangu nilipoanza nursery school, mwaka wa kwanza tu nilikuwa najua kusoma na kuandika kwa vizuri sana kiasi barua za mechi za timu za mitaa yetu yote nilikuwa naletewa mimi. Nilikuwa najifungia kuandika hadithi, nyimbo ninazozisikia na kujichorea picha mbalimbali katika vijitabu nilivyokuwa natunga tunga mwenyewe tu wakati huo.

 

BC: Unaweza kukumbuka nani hasa alikuvutia kwenye masuala hayo ya uandishi na usomaji? Nauliza hivyo kwa sababu watoto wengi kwenye umri huo wanapenda zaidi kucheza chandimu na michezo mingine kama gololi nk.

 

ST: Wakati ule nilivutiwa sana na michoro ya Phillip Ndunguru kwenye gazeti la Sani, na nikawa naiga anavyochora na kisha natunga watu wangu. Lakini sikuacha mpira, nilicheza kama watoto wengine, ila zaidi nilionekana nafuatilia sana kutunga hadithi, kuandika vitabu, kuchora na kuandika nyimbo ninazosikia. Mara nyingi nilitumia muda wangu kwa mambo hayo.

 

Page 1 of 8 | Next page