
Kwa miaka nenda rudi, tangu miaka ya sabini,jina la Freddy Macha (pichani) limekuwa sio geni miongoni mwa wasomaji mbalimbali wa magazeti, vitabu vya hadithi fupifupi,wapenzi wa muziki na pia sanaa ya ushairi nchini Tanzania. Iwe unamfahamu Freddy kupitia muziki wake,makala zake au mashairi yake, utakubaliana nasi kwamba Freddy ni mojawapo ya hazina tulizonazo linapokuja suala zima la usanii. Wengi miongoni mwa wasomaji wa makala zake katika magazeti ya The Guardian na Mwananchi nchini Tanzania, wanakiri kwamba makala za Freddy huwa ni mojawapo ya sababu zinazowafanya wakati mwingine wadamke asubuhi na mapema ili mradi tu wasikose nakala za magazeti hayo hususani siku zinazochapishwa makala zake.
Wapenzi wengi wa muziki,ushairi, tamthiliya na ngoma mtakuwa mnamkumbuka Freddy Macha tangu alipokuwa na kundi la Sayari. Kundi hilo ambalo lilitamba sana mwanzoni mwa miaka ya themanini, ni mojawapo ya vikundi vichache vya sanaa nchini Tanzania vilivyopata mafanikio sio tu nchini Tanzania bali pia katika medani za kimataifa. Sayari liliwahi kufanya ziara kadhaa za kimaonyesho katika nchi mbalimbali za nje hususani za Ulaya enzi hizo.
Kwa upande wa uandishi,Freddy Macha alianza kunoa kalamu katika magazeti ya Uhuru na Mzalendo na baadaye kuwa mwanasafu(columnist) wa gazeti la kila jumapili la Sunday News hadi mwaka 1984.Freddy amewahi kushinda tuzo kadhaa za uandishi ikiwemo ile ya Ushairi ya BBC mwaka 1981 na hadithi fupi fupi ya Jumuiya ya Madola( Commonwealth of Nations) ya mwaka 1996.
Hivi karibuni, baada ya kumsaka kwa muda mrefu, tulipata nafasi ya kufanya mahojiano ya kina na mwandishi/mwanamuziki/mwalimu huyu ambaye hivi sasa anaishi London nchini Uingereza. Sasa kutokana na ukweli kwamba Freddy ni mmojawapo miongoni mwa wale watu ambao tunaweza kuwaitwa “wenye vipaji vingi”,tumeamua kuyagawa mahojiano yetu naye katika sehemu mbili. Sehemu ya kwanza, ambayo ndiyo hii unayoisoma leo, tumeongea naye zaidi kuhusu kazi zake za uandishi.Sehemu ya pili ambayo itawajieni baadaye kidogo,tuliongea naye kuhusu muziki,jamii na mengineyo kadha wa kadha.
Unataka kujua Freddy ametokea wapi?Amepitia mambo gani mpaka kufikia hapo alipo? Anasemaje kuhusu uhuru wa vyombo vya habari, uandishi wa leo akilinganisha na ule wa zamani? Kwanini kitabu chake cha hivi karibuni amekiita Mpe Maneno Yake? Unafahamu kwamba Freddy aliwahi “kuzamia meli”?Ilikuwaje? Anasemaje kuhusu dhana za mawasiliano kama blogs? Kwa hayo na mengineyo mengi, fuatana nasi katika sehemu hii ya kwanza ya mahojiano yetu naye;
BC: Karibu sana ndani ya BongoCelebrity
FM: Ahsanteni…mambo?
BC: Poa kabisa. Tunayo furaha kubwa kupata nafasi ya kuzungumza nawe hivi leo.Labda tuanze kwa kupata historia yako kwa kifupi.Ulizaliwa wapi,lini,ukasomea wapi nk
FM: Nilizaliwa Old Moshi, mwaka 1955; wazazi wangu walihama hama kutokana na kazi ya Baba ya udaktari na walipiga muziki, Mama akiwa mwimbaji. Tuliishi Moshi mgombani na Bumbuli kule Tanga. Nilisoma huko huko Mgombani (Wachagga tunaita shamba mgombani shauri ya migomba na kahawa na mifugo); hadi mwaka 1967. Nikiwa darasa la sita nilihamia Arusha, shule ya Kaloleni. Aliyekuwa sasa mlezi wangu ni Shangazi Sara Materu ambaye alikuwa Mwalimu Mkuu maarufu wa Shule ya sekondari ya Arusha …akiitwa Mama Materu enzi hizo. Alichanganya tabia na mwenendo (ambao hadi leo anao) wa elimu bora, nidhamu, mapenzi na alinishughulikia vizuri sana.
Nilifaulu na kuingia Sekondari Ilboru, hadi mwaka 1972, baadaye nikaendelea sekondari Mzumbe, Morogoro kidato cha tano na sita hadi 1974.
Enzi hizo tulitakiwa kisheria kujiunga na jeshi la kujenga taifa (JKT) baada ya masomo. Niliingia kambi ya Mafinga mkoani Iringa na kisha kuanza kazi kwenye gazeti la Uhuru mwaka 1976. Kazi yenyewe sikuiomba, niliitiwa kutokana na makala na barua nilizokuwa nikiandika tangu nikiwa shuleni.

BC: Ingawa una vipaji vingi mbalimbali,kama ambavyo tutaviongelea vyote katika mahojiano haya,wengi tunakufahamu zaidi kama mwandishi.Nini kilikuvutia kuingia katika fani ya uandishi?
FM: Najulikana kama mwandishi nyumbani Bongo, lakini nchi za nje kazi yangu kuu ni mwanamuziki. Vitu hivi viko katika damu.
Nikiwa mdogo sikuwa mzungumzaji sana…nilipenda kusoma, kusikiliza, kutazama watu, kuchanganyikana nao lakini kuwasoma…Katika familia kulijaa waandishi, wataalamu na wanamuziki. Babu yangu (Mchungaji Anaeli Macha ) alikuwa mchungaji maarufu na mwandishi ,akachapisha vitabu kadhaa vya tabia, dini, familia na jamii. Pia shangazi zangu wengi walinipa moyo toka utotoni. Nakumbuka mmoja wao,Shangazi Eva, alikuwa akisifia barua zangu akisema “Freddy akiandika barua ni kama kitabu.”
Uandishi rasmi wa kijumuiya ulianza nikiwa kidato cha pili. Ilikuwa hivi. Nilipokuwa Ilboru nilikuwa nikisaidia baadhi ya wenzangu kuandika barua zao za mapenzi kwa akina dada (“girlfriends”) nikaanza kudai pesa. Wakati huo nilikuwa mwanachama wa kikundi cha vijana tukijiita “The Gringos.” Kuna wakati tulipigwa na wahuni na wanajeshi baada ya kuwaandikia wasichana fulani waliogombana na mmoja wetu barua. Zile barua nyingi niliziandika kutokana na ushauri wa kikundi hicho chetu.Zilikuwa si mchezo. Tuliishia kupigwa kishenzi na pia chapwa viboko vya faru na kulazwa hospitali.
Nilipokuwa nikisoma Mzumbe tulikuwa na bendi mbili. Ya walioimba Kiingereza, “Earthquakes” (niliyokuwepo) ikiongozwa na mkimbizi na mpigania Uhuru wa Afrika Kusini, Tabiso Leshoai na Mike Sikawa (aliyekuja kuwa mwandishi Daily News siku hizi yuko BBC anaandikia This Day)…ya pili ilikuwa ya muziki wa Kiswahili. Zote zilipewa moyo na marehemu Mbaraka Mwinshehe aliyekuwa akija pale Mzumbe kupiga piga dansi letu na dada zetu, wapenzi wetu wa shule ya Kilakala.
Lazima nisisitize suala la mtoto kuwa na waalimu wazuri. Moja ya mchango mkubwa katika elimu yangu ulikuwa pia waalimu. Mwalimu Mkuu, marehemu Lema na Mushi (“Chesti”) aliyemrithi, walikuwa wakali na walituchapa viboko na kutupa nidhamu ya kimaisha. Ilboru ilikuwa na waalimu wengi toka mataifa mbalimbali. Mmoja wao aliyenihamasisha kupenda zaidi fasihi ni Mama Chitepo aliyekuja kuwa Waziri wa Elimu nchini Zimbabwe.
Vile vile shule ya Mzumbe. Ilikuwa chimbuko la mwamko wangu kama mwandishi na mwana-jamii hasa kutokana na baadhi ya waalimu wazuri tuliokuwa nao. Namkumbuka mwalimu wangu wa fasihi marehemu John Mdakie(huyu bahati mbaya aliuawa baadaye na majambazi Dar Es Salaam ingawa alikuwa mtetezi mkubwa wa walalahoi) na mwandishi Nizar Visram. Visram alitufundisha kusoma vitabu na kuvijadili. Pia alikaribisha wataalamu mbalimbali wa ngazi za juu, kimataifa, kuja kuongea na kujibu maswali yetu. Kati yao ni mwandishi mashuhuri, mwanahistoria wa Kigayana, marehemu Profesa Walter Rodney (aliyeandika kitabu maarufu “How Europe Underdeveloped Africa”) na mshairi maarufu wa Afrika Kusini, Kgotsitsile. Huyu alifungwa mara kadhaa na makaburu.
BC: Mbali na uandishi kuwa katika damu au katika familia yenu,kwa vyovyote vile kuna mwandishi au waandishi ambao ulikuwa ukipenda kuwasoma tangia utotoni.Unaweza kututajia majina yao?
FM: Kwanza kabisa katika familia, Babu Mchungaji Macha mwenyewe. Halafu hapo hapo Bongo nakumbuka darasa la Sita nikisoma mashairi ya Shaaban Robert nikajiuliza hivi mtu anawezaje kuandika na kuwa na lugha nzuri kiasi hiki? Nakumbuka shairi la “Titi la Mama Litamu Hata likiwa la Mbwa.” Baadaye nilipenda sana kusoma magazeti…hasa kutoka Kenya. Moja liliitwa “Baraza” (miaka ya sitini).Gazeti lile lilikuwa la umbea na mastore kibao. Nina miaka 12-13 wakati huo. Lilinisisimua sana.Tulisoma pia magazeti ya “Film” yaliyokuwa na mbabe Spear na katili Rabon Zollo. Karibuni mwanablogu maarufu Michuzi katoa picha mbalimbali kusisitiza mchango wa magazeti haya ya zamani kusaidia lugha ya vijana enzi hizo.
Baada ya hapo nilianza kusoma riwaya za Kiswahili na Kiingereza. Akina James Hadley Chase…Ian Fleming (aliyetunga James Bond) Kisha, Waafrika akina Chinua Achebe, Ngugi Wa Thiong’o (enzi hizo akiitwa James Ngugi), Euphrase Kezilahabi.Sasa niko sekondari…kidato cha pili…nasoma magazeti, riwaya, nakwenda sinema. Nakumbuka kidato cha kwanza na cha pili nilipewa tuzo na waalimu kama msomaji wa vitabu vingi. Sinema nilianza toka utotoni (wazazi wangu walikuwa wakinipeleka Plaza na Everest pale Moshi) nilipenda sana sinema na kujiunga na michezo ya kuigiza, Ilboru.
BC: Kwa hiyo mbali na uandishi unakumbuka ulitaka kuwa nani ukubwani?
FM: Mbali na uandishi nilitaka, toka nikiwa mtoto, kuwa mwanamuziki. Nakumbuka nilikwenda kuona sinema ya Elvis pale Plaza, Moshi nikiwa na baba na mama. Nikaona yale magitaa, zile nyimbo, zile bichi na wanawake wakicheza nk. Wakati huo nina miaka minane nafikiri. Toka hapo nikasema lazima niwe mwanamuziki. Hii ni ukiachilia mbali kwamba kila siku Baba akitoka kazini au hata akiwa katika breki ya kula chakula cha mchana wakati akingojea mama amalize kupika (yuko na magwanda yake ya udaktari) anacharaza gitaa akisubiri msosi. Ile yote ilinipa hamasa; motisha.Wakati nikiwa sekondari gitaa na utunzi wa muziki ukaja kuwa moja ya njia za kujielezea hisia zangu. Nikikasirika au nikitaka kujieleza nachukua gitaa.
Baadaye ikawa kama natumia uandishi kupikicha muziki na muziki kupikicha uandishi. Nitafafanua mbele kwanini vitu hivi viwili havibandukani hadi leo.
BC: Nini kumbukumbu yako ya siku ya kwanza kama mwajiriwa wa gazeti la serikali,Uhuru,ulipoanza mwaka 1976?Ilikuwaje siku hiyo?
FM: Duh…ilikuwa raha tupu. Niwakumbushe wasomaji miaka ya 70 ilivyokuwa Bongo. Lipo vuguvugu kila mahali. Vijana tuna hamasa,tunataka kubadili jamii.Tunamsikiliza Mwalimu Nyerere akisema nchi inahitaji kuondoa umaskini kuwa wakulima na wafanyakazi ni watu wa mbele.Tulikuwa wengi tuliotoka Mzumbe, Tabora, Mkwawa, nk.
Nilikuwa na akina marehemu Yahya Buzaragi (aliyekuja kuwa Mhariri wa Uhuru) , Marehemu Profesa Chachage (yeye aliingia fani ya uchapishaji vitabu baadaye akaendelea Chuo Kikuu na kuwa Mhadhiri maarufu). Akina Sengondo Mvungi, Harrison Mwakyembe,Palamagamba Kabudi.Wote hawa siku hizi wataalamu wakubwa nchini. Wana hamasa bab kubwa. Sasa siku hiyo ya kwanza…1976.
Nakumbuka nilikuwa nimevalia shati langu la kitenge na suruali ya mtumba nyeusi (niliinunua Kariakoo) viatu vya safari buti.Nimeingia,kijana mbichiiii, miaka 21. Nikawakuta akina Abdi Mushi, Salva Rweyemamu (bado yupo huyu) Mzee Stephen Msuya, na gwiji la uandishi Ndimara Tegambwage.Wamekaa pale wanatupa moyo. Sijui kutumia taipu wala nini.Enzi hizo mashine za kupiga taipu za kelele na zina vibonyezo vigumu.Wakawa wanatuonyesha mambo. Siku hiyo hiyo nikapewa kazi ya kwenda kumhoji mtu huku nimeongozana na mpigapicha bab kubwa marehemu Awadh Shebe.Huyu alikuwa si mchezo. Tuliewana sana. Awadhi alikuwa msanii wa kamera.Walikuwepo wengine akina Khatibu Ali lakini Awadh duh alikuwa pia kijana mwenzangu. Nakumbuka kuna picha alipiga mpirani wakati wa mechi ya Yanga na Simba (enzi hizo si mchezo). Picha ile ilizungumziwa miaka na miaka. Ilikuwa picha ya tikitaka.Brazili wanaita kipepeo (“Bolboleta”); kiingereza wanaiita “Mkasi”…. bahati mbaya Bongo hadi leo hatutoi tuzo kwa waandishi na wasanii bora. Awadhi alistahili.
Bila kusahau kusema, Awadhi ndiye aliyenifanya nianze kujifunza Kifaransa.Tulikuwa kila tukiwahoji watu wasiojua Kiingereza, anasema duh lazima tujifunze lugha zao.

Freddy (katikati kalamu mkononi) , akifanya kazi Uhuru na Mzalendo, akimhoji Meya wa jiji la Amsterdam katika uwanja wa ndege wa Nyerere, Dar Es Salaam mwaka 1978. (Picha na Khatibu Ally)
BC: Tukiwa bado kwenye suala la uandishi.Unadhani waandishi na uandishi wa leo wana tofauti gani na ule wa enzi zile ulipokuwa unaanza kuandika?
FM: Kitu kilichosukuma uandishi wa enzi zile ilikuwa Siasa ya Ujamaa na Kujitegemea. Motisha wa kutaka kuendeleza jamii,kujenga nchi,kupambana na kile Mwalimu alichoita maadui watatu : umaskini, ujinga na maradhi. Leo waandishi wanafikiria fedha. Lakini enzi hizo kulikuwa pia na waandishi wa aina hiyo lakini haikuwa mtindo kama sasa.
Tofauti nyingine kubwa ni kwamba maduka ya vitabu yaliuza vitabu. Waandishi walisomwa. Uandishi ulikuwa na faida kwa vile ukiandika mtu unasomwa. Magazeti yalikuwa mawili tu Uhuru (Kiswahili) na Daily News. Kwahiyo magazeti hayakuwa mengi kama leo. Vitabu vilisomwa zaidi. Leo kuna magazeti elfu kidogo na vitabu havisomwi, lugha mbovu. Enzi hizo hadi uandikwe magazetini lazima uwe na lugha na uwezo mzuri sana; si holela kama leo. Kila mtu anajiandikia tu. Leo kuna sinema, DVD, runinga, enzi hizo hakukuwa na vitu hivi. Mimi nimeona sinema mara ya kwanza katika runinga nikiwa Nairobi,niliona maajabu.
Lakini ule uvivu wa kutotafiti mambo baina ya waandishi bado upo hadi leo. Bado waandishi wa habari hawatafiti. Wakihoji hawatafiti mada sawasawa. Lugha imekwenda chini sana.Si kwa vile waandishi hawajasoma. Wandishi wa leo wamesoma kuliko wa zamani (wengi zamani walitokea kidato cha nne); Tatizo la leo waandishi wenyewe hawasomi vitabu. Vitabu vya fasihi na mashairi ndiyo huongeza msamiati wa lugha. Kiswahili na Kiingereza vimeghafilishwa, viko butu, vimejiinamia kama kuku aliyenyeshewa mvua.
BC: Unaliongeleaje suala la uhuru wa vyombo vya habari enzi zile ukiwa Uhuru na Daily News na hivi leo?Ni kweli kwamba enzi zenu kila mlichoandika ilikuwa ni propaganda kwa manufaa ya watawala?
FM: Kweli kabisa. Leo kuna uhuru wa kuandika kuliko enzi zile. Enzi hizo Mhariri Mkuu alikuwa Rais wa nchi. Leo hata blogu zinasomwa, zinaandikwa na Wabunge kama akina Zitto Kabwe, bila wasiwasi. Mwaka niliokuwa Uhuru, mawazo kama anayoandika Zitto au huyu mwandishi wa This Day, Nkwazi Mhango (ana blogu kali sana http://mpayukaji.blogspot.com ) ingekuwa ni enzi zile wangetiwa ndani moja kwa moja. Sisi tulikuwa na wasiwasi sana.Na mara nyingi tulikuwa tukijihariri kabla ya kutoa makala.
Nakumbuka siku moja mhariri wangu Uhuru (marehemu Costa Kumalija) alivyokuja mkutanoni na gazeti limechorwa chorwa rangi nyekundu na Rais. Akasema Raisi kaudhiwa na habari fulani zilizoandikwa na gazeti. Visa vya aina hiyo vilitufanya waandishi tuwe na wasiwasi. Lakini kama nilivyosema sisi vijana tulikuwa na hamasa fulani, tukifikiria jumuiya, tukifikiria maendeleo. Mimi nilikuwa na safu zangu chungu nzima.Mojawapo iliitwa Wachapa Kazi ambayo nilitafuta wananchi waliokuwa wakijitahidi. Hadi leo napenda kuendeleza sana dhamira hiyo.Kwa upande mwingine ndiyo maana nilipiga muziki, maana yale ambayo hayakuandikwa gazetini niliyageuza ,muziki, niliyaandikia mashairi.

Freddy Macha(kulia) akimhoji mshairi maarufu wa Jamaika ambaye huwa havai viatu, yaani Mutabaruka, Brazili mwaka 1994 (Picha na Amita Macha).
BC: Unaweza kukumbuka kisa chochote ambacho unadhani kilikuwa ni sumu kabisa kwenye dhana nzima ya uhuru wa vyombo vya habari enzi hizo?Kwa maoni yako unadhani nini kimechangia kuboresha uhuru wa vyombo vya habari tulionao hivi leo?Kuna madhara yoyote ya kuwa na uhuru wa vyombo vya habari na pia uhuru wa kujieleza?
FM: Kwanza suala la sumu la Uhuru wa Habari. Kumbuka hali ilivyokuwa. Mwandishi wa habari anakwenda mahali kuchukua habari ili awe mdomo wa serikali na uongozi. Mara nyingi zilikuwepo karamu au pati ambazo pale mwandishi unapata chochote (cha kula na kuandika) .Sasa tatizo lilikuwa hapo. Mishahara yetu ilikuwa midogo sana. Uhuru bahati nzuri waandishi tulipewa pikipiki. Alhamdulilahi. Usafiri mbaya wa Dar ulisaidiwa na zile pikipiki. Lakini baada ya kazi (yaani kuandika store) mwandishi ulichofikiria ni wapi pa kwenda kupata pombe na makulaji ya bure.Huko huko kuna kitu kinaitwa ku-lobby (leo Ulaya wanasema “networking”, wanawake huita umbea wa kirafiki).
Baadhi ya waandishi walitia aibu. Si wote, lakini ukweli hali ya umaskini ilikufanya mtu ujisahau. Mi nikiwa kijana iko siku nililewa nimempakia mtu tukaanguka na pikipiki. Saa za manane hizo. Ukiwa kijana unaona advencha hizo. Humo humo kuna visura wa kukata na shoka. Unaingia baa na vijisenti vyako unawaka. Unarudi… hilo doa la kulewa usiku ili kupata contacts (ambayo ni sehemu mahsusi ya uandishi wa habari) ilitufanya waandishi wa Bongo tuonekane wa njaa. Lakini si wote. Baadhi ya wageni hasa katika balozi walitujua.
Sasa ukija kwenye Uhuru wa kujieleza. Ikiwa mtu una mshahara mbaya, unategemea wakubwa kwa rasilmali na maisha ni wazi kwamba unakuwa huandiki kile unachokitaka. Matokeo waandishi wengi walikuwa walevi. Unajikuta unajua siri nyingi sana za nchi, unajua makosa mengi sana yanayofanyika, unawafahamu waongo na wakweli katika ngazi za juu, lakini huthubutu kutema, kutapika, wala kupiga chafya.
Ninawafahamu jamaa chungu nzima waliopotea. Wengine tukinywa pamoja sikuwaona hadi leo. Wanapotea tu. Wanafichwa. Kitabu changu cha kwanza (Twenzetu Ulaya) kilikuwa na kisa cha kweli cha mtu aliyeshukiwa kuwa “njagu” (shushushu), kinaitwa Masizi. Kumbe hakuwa lolote, maskini. Alikuwa tu na yake. Akauawa Uswahilini. Ile hali ya kuogopa kusema, kuogopa kuandika, kuogopa nani atakusikia, kuogopana hata waandishi kwa waandishi.Hali hii ilizua kitu kama hofu ya moshi na mvuke (“paranoia”) ambayo imewafanya watu wa rika langu hadi leo wawe wanaogopa ogopa na kuwa waangalifu kuzidi kiasi.
Kwa mfano mimi hadi leo nikiwa katika simu hata huku ughaibuni bado nina kawasiwasi kuwa kuna mtu ananisikiliza. Kumbe haiendi hivyo. Kawaida mashushushu wana watu wanaotaka kuwajua. Na leo ukitakiwa na serikali yeyote duniani utapatikana tu,huwezi kujificha. Lakini hapa nazungumzia ule wasiwasi uliokuwa umeenea ambao niliutungia kisa kilichoitwa Masizi katika mkusanyiko huo wa Twenzetu Ulaya mwaka 1984.
BC: Labda kabla hatujaendelea mbele..unakumbuka makala yako ya kwanza kuchapishwa gazetini ilikuwa lini na ilikuwa ikizungumzia nini?Unakumbuka nini zaidi kuhusu siku makala yako ilipochapwa gazetini?
FM: Sikuanza kama mwandishi wa makala, bali utenzi (mashairi) na barua.Ya kwanza ilikuwa barua nilizokuwa nikiandika magazetini,nikiwa bado shuleni.Nyingi sikumbuki lakini iliyovuma sana …nafikiri ilikuwa suala la vitabu vya Kizungu kuzidi kuuzwa nchini kuliko vya wananchi. Ilichapwa gazeti la Kiingereza, Daily News ikasifiwa sana. Nilikuwa kidato cha tano. Mhariri wa Uhuru alipoona akawa anatuma waalimu waniambie niwaandikie. Nilianza kuandika rasmi magazetini nikiwa kidato cha tano na sita.
Wakati huo kulikuwa na vuguvugu likivuma kila mahali.Mapinduzi ya Msumbiji (enzi Samora Machel kanyakua Uhuru Msumbiji), masuala ya Idi Amin akiua watu Uganda, Karume wa Unguja kauliwa Zanzibar, (1972) wakimbizi kibao wakija Bongo (toka Marekani enzi zile “Black Panthers” ikivuma) Wapalestina, Wasoweto (ndivyo tulivyoita wakimbizi toka Bondeni) hali ya vuguvugu, ukiwa mwana fikra unakuwa pia mwanajamii, unaona fahari kuitwa mwanamapinduzi.
Nilikuwa niko tayari hata kwenda Namibia kupigana, Palestina kushika bunduki…ilikuwa si bla bla…kila mtu alikuwa moto. Ndiyo miaka hiyo migomo ikapigwa marufuku Tanzania. Shule zilikuwa zinafungwa, mameneja waonevu wanafungiwa nje…hili vuguvugu ndiyo lilinipa mshawasha wa kuandika magazetini,kutunga mashairi, nyimbo, fasihi.

Jeshi la Kujenga Taifa (JKT) Mafinga, mwaka 1975 (Picha na Harold Mhando)
BC: Unadhani moyo huo wa kujitolea mliokuwa nao vijana wa enzi hizo,moyo huo wa kizalendo,upo mpaka hivi leo?Kama haupo nini kimetokea?
FM: Nafikiri Vijana wote wako sawa kiwakati. Vijana kwa jumla si watu waoga. Lakini vijana pia ni watu wasioona mbali. Wanataka mabadiliko lakini hawaangalii kila kitu. Kwa mfano kuna wakati nilichana chana noti ya shilingi mia moja mbele ya Mama yangu baada ya ubishi wa kifamilia. Hii ni eti miaka kabla sijaanza kazi, nimetoka jeshini, ninakosoa utawala unaowatesa maskini.Enzi hizo shilingi mia zilikuwa nyingi kama noti ya shilingi elfu kumi leo; hata zaidi.
Vijana wa leo wanao urahisi fulani ambao enzi zetu haukuwepo. Leo unaweza kufungua blogu, unaweza kuongea na mwenzako yeyote popote pale kwa SMS au barua pepe. Leo kuna Uhuru wa kuandika, kufanya mambo, kuna urahisi wa kuelewa mambo ya kidunia. Mimi kwa mfano miaka hiyo nilikuwa nakusanya habari kupitia wageni. Chukua suala la magazeti. Kuna majarida ya fasihi ambayo leo kijana anaweza kuyashusha kutokea “Google” kirahisi. Mi nilikuwa nakutana na mtalii,namwomba akirudi kwao anitumie jarida fulani kwa mfano gazeti mashuhuri la watu weusi la Marekani, “Ebony.” Nilikuwa nalihusudu sana.
Kwa hiyo urahisi ulioko leo unawafanya vijana waweze kufanya mengi ambayo sisi tulikuwa tunaotea. Ndiyo maana baada ya kujiuzulu kazi Uhuru mwaka 1978, nikaamua sasa na mimi nataka kuwa Baharia. Nikastoawei kama wengine wote. Tukashikwa India tukarudishwa mkuku.
Zote hizo zilikuwa jitihada ambazo leo, mtu unataka kwenda nje lakini unaweza pia kujaribu mambo ili mradi uwe na fedha.Enzi hizo hata haya mawazo ya kutoka nje ilikuwa unaulizia hujui uyapate wapi. Leo, ukiingia mtandaoni mambo kibao.
Ukija kwenye suala la kujitolea.Leo itikadi au fikra iliyopo kijamii sio uanamapinduzi, uanamabadiliko, bali kutaka kuukata, kutaka fedha.Hakuna wanamapinduzi wanaotia kichaa Afrika.Enzi hizo kila ukifungua gazeti unawaona akina Samora Machel. Unamsoma Steve Biko,unamsoma Mpalestina kafanya hili na lile. Leo marapa waliovalia suruali nusu uchi, chupi nje, kama wasenge, ndiyo wanaonekana wababe.Lakini ubabe wao ni wa “Bling Bling” wa kutumia: pombe, mabibi, magari, shari tupu. Kijana wa leo anafikiria Bling Bling au kuwa mjeuri, pesa, kuwa mtukutu. Sisi tulikuwa tunafikiria sana kubadili jamii iwe nzuri kwa maskini. Tulikuwa tukiwaangalia akina Che Guevara, Fidel Castro, Bob Marley, Malcolm X.Tukimzungumzia Mandela akiwa jela.Hapo hapo wapo waliotaka haya ma-Bling Bling lakini hayakuwa yakionekana kiwingi kama sasa kila kona yamejazana katika mtandao, runinga nk. Lakini vijana siku zote ni vijana,wana moto. Tofauti ni mazingira yao na wakati.
BC: Umegusia kidogo kisa cha kustoawei.Visa vya namna hii huwa vina msisimko wa aina yake miongoni mwa vijana.Unaweza kutusimulia kidogo ilikuwaje mpaka ukaamua kustoawei?Tupe mkasa huo japo kwa kifupi kisha tutaendelea na mada zetu za leo tafadhali.
FM: Hamna noma. Kwanza kabisa ilikuwa siri kubwa. Ukweli sijawahi kuliongelea suala hili katika hadhara hadi karibuni maana hata familia yangu haikujua. Wala girlfriend wangu enzi hizo hakujua. Nilikuwa nimechoka. Nimeacha kazi Uhuru shauri ya uzembe wa utawala.
Nilipoacha kazi, wenzangu kama wanane (au zaidi nasikia) wakafuata. Sasa hakukuwa na pengine pa kwenda. Nilitaka sana kuanzisha gazeti langu. Mtaji sina. Pesa itatoka wapi? Enzi ambazo biashara hazikuruhusiwa na uhuru wa kibiashara haukuwepo. Ah ikawa sasa wazo ni kuwa baharia. Zilikuwepo meli kibao pale bandarini. Kuingia ndani ni kuwapa jamaa chochote. Kifupi tulikuwa kama saba hivi. Tukajichomeka. Tumebeba mandazi,vitumbua, maji ya kunywa (enzi hizo hakuna haya maji ya chupa ya kuuzwa Bongo) tumeingia kule na nguo hizo hizo.
Kujisaidia ni humo humo baharini, mnapeana zamu ya kugadi usiku, mmejificha ndani ya mananihii ya kufunika bidhaa za meli. Wengine wanatapika, wengine wanaona baridi, hasa tulivyofika kati kati ya Bahari ya Hindi kupita visiwa vya Komoro. Mimi nilikuwa mtu wa mazoezi (hadi leo) nikishikwa kipipa ninapiga “mapush-up” yangu mia tatu…najisikia mwepesi na mwenye imani. Kufika Bombay sasa ikawa kazi ya kuvizia tutoke. Nchi yenyewe hatuijui. Lugha hatuongei. Pale kiama. Tumengoja usiku kucha. Kutoka mmoja mmoja.Wengine wakashikwa, wengine tukapotelea mitaani. Sasa pesa hatuna. Mtu unatafuta namna ya kupata kazi. Mipango hakuna. Tunajua tu kazi za meli rahisi.Inakuwa unaulizia kilibeneke,unabahatisha.
Tumekaa pale wiki moja.Namna tulivyokula wala haielezeki.Lakini tulikula. Wengine kama miye tulishapitia jeshini kwa hiyo “ujanja wa porini” tushajifunza.Lakini hatima yake ilikuwa kushikwa. Kurudishwa hadi Kenya. Kupigwa kishenzi. Hadi leo nina makovu. Kimya kimya kupandishwa katika mabasi, kutokea Tanga,kupotelea mitaani. Hapo ilibidi nivae kofia ya uandishi. Maana unaona ni kama “advencha” umepata cha kuandika. Lakini siri yake kubwa ni hii. Usitoke nchi yako kama hujui unakokwenda. Huna mpango. Hiyo ilikuwa moja ya nguzo zangu za kuandika Twenzetu Ulaya.Kuwaonya wenzangu kuwa usiondoke bila mpango.
BC: Duh..kisa cha kusisimua sana hicho.Tutapenda kusikia zaidi next time.Tuendelee
FM: OK. Kuna mengi zaidi lakini iko siku labda…katika biografia yangu

Freddy akitongoa moja ya shairi lake linalopendwa linalozungumzia urasimu liitwalo Papers! Papers! Papers! Katika tamasha la sanaa na muziki wa mtu mweusi, mjini Copenhagen, Denmark mwaka 1985 (Picha na Jørn Stjerneklar).
BC: Tukirudi kwenye uandishi.Kwa maoni yako unadhani uandishi ni kipaji au ni kitu ambacho mtu yeyote anaweza kujifunza na kuweza?
FM: Uandishi ni kipaji, ni kuzaliwa hapo hapo ni kazi. Kila mwanadamu anao uwezo wa kuelezea jambo. Namna ya kuelezea inategemea kipaji, ufundi, silika na hulka. Wengine wazuri wa kusema. Wengine wazuri wa kuimba, wnegine wanachora, baadhi wanaandika. Kama nilivyosema nikiwa mdogo sikuwa mzungumzaji. Leo nimekuwa mzungumzaji sana, hususan shauri ya kufundisha, kuwa mwalimu na mwanamaonyesho.Lakini nimegundua siri moja kubwa. Ukitaka kuwa mzungumzaji mzuri, mwandishi mzuri, mstareheshaji mzuri, mwanafasihi poa, shurti uwe msikilizaji mzuri. Hakuna mpiga picha mzuri wa jamii kama mwandishi. Maana hukaa pale kimya wala hamumjui.
Kazi ya uandishi inaboreshwa pia na kusoma. Linton Kwesi Johnson, mshairi wa Kijamaika alikuwa akiwaasa waandishi chipukizi hapa London miaka michache iliyopita. Akasema mbona wanamuziki wanasikiliza sana muziki? Kusudi wawe mahiri. Mwandishi asiyesoma alisema Linton Kwesi, ni kama bubu asiyejua kutumia ishara za vidole. Maana msamiati utatoka wapi?
Uandishi ni kazi lakini pia ni wajibu kwa watu wako, kwa jamii yako, kwa uhai na kwako wewe mwenyewe. Maana mwandishi unaopoandika unajijua zaidi. Unajielewa zaidi. Ni kama kuoga au kujichana nywele. Unajichana ili upendeze, lakini hapo hapo unajiangalia angalia unaelewa kichwa chako kiko hivi…
BC: Sasa kumekuwepo na hoja kwamba siku hizi nchini Tanzania hakuna tena waandishi mahiri,hususani wa riwaya, kama ilivyokuwa enzi za akina Elvis Musiba, Katalambula, Kezilahabi nk.Je unakubaliana na hoja hiyo?Kwanini?
FM: Kwanza kabisa vitabu haviuziki. Dar nzima kuna maduka mangapi ya vitabu au maktaba ngapi za vitabu vya Kiswahili? Utashangaa jinsi ambavyo sera ya elimu inahusisha tu wale walioko mashuleni. Lakini jamii inahitajika kuwa inasoma na kujielemisha hadi uzeeni. Ndiyo maana wenzetu wa nchi tajiri wanaendelea,wanatunga,wanagundua vitu, wanaishi maisha marefu sisi tunazidi kufa vijana (umri wa wastani leo ni miaka 45, Tanzania, ilhali Uingereza ni 75-80!) wanatajirika nk. Hii ni kwa sababu wanasoma. Sisi hatusomi, si kwa vile hatutaki, ila kwa kuwa hakuna sehemu ya kuuza vitabu.
Nilipomhoji mwandishi makini wa Unguja, Adam Shafi (mtunzi wa Kuli, Kasr ya Mwinyi Fuadi, Vuta Nkuvute na Haini) nilimuuliza swali hilo. Akasema ukisafiri mikoani siku hizi huwezi hata kituo kimoja kununua kitabu. Ukisafiri nchi za ughaibuni katika kila kituo utakuta maduka kadhaa ya aina kadhaa, ya kununua vitabu, majarida na vyakula. Kwetu kinachokutwa ni vyakula tu.
Kwa hiyo kwa kuanzia waandishi hawana pa kuuzia vitabu. Chukua kitabu changu cha karibuni, Mpe Maneno Yake…watu chungu nzima wananiandikia wanataka kukinunua lakini hawajui wapi wakipate. Nimewajibika mwenyewe (kama mfanyabiashara eti) kukiuza,utadhani, njugu. Kutembea navyo…kazi gani hii? Waandishi ni wasanii wanachotaka ni kutunga…si kubeba soko la Kariakoo begani.
Ukiongea na wachapishaji leo Bongo wanakuambia vitabu vinavyouza ni vile vitavyotumika eti mashuleni. Si vibaya hata kidogo; lakini inapaswa viwepo pia vitabu vya watu wazima. Badala yake watu wazima wanachosoma ni chupa za bia, mitungi ya mbege, gongo na matap tap! Nchi itaendelea kweli?

Baadhi ya kazi za mwandishi na mwanamuziki Freddy : vitabu vya hadithi fupi (Twenzetu Ulaya, Mpe Maneno Yake) albam ya Constipation na utenzi wa mashairi ya Kiingereza, Papers! Papers! Papers! (Picha na Ona Macha)
BC: Umegusia suala la kitabu chako cha hivi karibuni kiitwacho Mpe Maneno Yake ambacho nimemaliza kukisoma hivi karibuni.Kwanza kabisa nikupe hongera kwa kitabu hicho chenye visa motomoto.Pia ningemshauri msomaji yoyote wa mahojiano haya afanye juu chini akinunue na kukisoma.Swali; Mpe Maneno Yake ni mchanganyiko wa visa chungu mbovu,miaka nenda miaka rudi.Ulikuwa unajaribu kufikisha ujumbe gani hasa kwa jamii?
FM: Kitabu kinapatikana maduka ya vitabu Chuo Kikuu cha Dar es Salaam au TPH mtaa wa Samora Avenue. Ukitaka pia waweza kuwasiliana moja kwa moja na wachapishaji (E& D Limited) kupitia simu namba ( +255) 78481-8282 au (+255) 754275347. Ongea na Kitunga au Lema, mjini Dar es Salaam
Nashukuru kwa kusifia…maana wewe pia mwandishi mzuri napenda blogu zako zote…na hili ni suala muhimu sana…waaandishi kuelezana ukweli kuhusu maandishi. Bongo tunayo tabia ya kuogopa kusifiana eti utampa mwenzio kichwa.Kumbe si kumpa mtu kichwa bali kuendelezana.
Sikupanga niandike kitabu hiki. Kama nilivyosema awali, wakati nikiwa ripota wa Uhuru na Mzalendo baadaye nikawa naandikia magazeti mengine (New Outlook, Nchi Yetu, Daily News, Sunday News, Mfanyakazi, Kiongozi,nk) kuna habari au story ambazo hazikuwa zikichapwa. Hizi nilizigeuza nyimbo, mashairi (nikazitongoa kupitia kikundi changu enzi hizo cha Sayari) au kuzikusanya ili ziwe kitabu baadaye. Mwaka 1981 mathalani nilipata tuzo ya ushindi wa mashairi ya Kiingereza toka BBC, kati ya tenzi zilizoshinda zilitokana na visa ambavyo vilikataliwa kuandikwa magazetini. Sasa basi kwa kuwa nimezunguka sana, zipo store nyingi namna hii. Mpe Maneno Yake ni asilimia ndogo tu ya mkusanyiko nilio nao. Kila siku miye huandika kitu : wimbo, shairi, hadithi, wazo au makala. Haipiti siku au juma bila kuwa na kitu. Uhai kwangu ni kalamu ya uandishi na utunzi.
Ukitazama kisa cha kwanza katika Mpe Maneno Yake ni mwaka 1976, wakati nikiwa Uhuru. Kilitokea kule Buguruni. Kisa cha mwisho ni Brazili, mwaka 1994, kuhusu mbwa koko. Katikati utakuta London miaka hii…Kanada…Mwananyamala, Mombasa….Sweden…nk…Kitabu ni kama kumbukumbu ya safari na mielekeo yangu, kuna mambo mengi nimeyaona,mengine ya kusisimua sana. Lakini siri ni moja …dunia yote inafafana. Maafa yale yale. Majanga yale yale. Machungu na matamu yale yale. Kinachotofautiana ni sura, rangi za nyumba na nguo, lakini hisia zile zile; kwa hiyo basi nia yangu ni kumkumbusha msomaji kuwa dunia ni ndogo, binadamu ni wale wale na matatizo na raha zetu zile zile.
Hapo hapo lazima nikumbushe kuwa mimi napenda sana hadithi fupi maana ni rahisi kuelezea mambo ya aina nyingi katika maelezo mafupi kuliko riwaya. Kwangu hadithi fupi ni kama kamera. Tuseme Mpe ni kamera.Karibuni nimeanza kumenyana na uandishi wa riwaya. Nimemaliza riwaya ya Kiswahili inayoitwa “Hekaya za Masudi London” (wasomaji wa safu yangu Mwananchi lazima watakuwa wanamjua Masudi Pashamoto) na ninaandika riwaya yangu ya kwanza ya Kiingereza.Uandishi wa riwaya ni mtamu pia. Haina maana kuwa siupendi. Naupenda. Kila kitu kina nafasi yake.

BC: Kwa hakika visa vilivyomo kwenye Mpe Maneno Yake ni vya kusisimua.Hongera tena.Sasa kabla hatujamaliza kwenye masuala ya uandishi ningependa kukuuliza kuhusu tekinolojia mpya kama hizi blogs.Wewe pia siku hizi ni mwanablog.Unadhani blogs zina nafasi gani katika jamii na zinatoa changamoto ya aina gani kwenye uandishi uliokuwa umezoeleka miaka nenda,miaka rudi.Ule wa mhariri,waandishi na wasomaji?Na pia unadhani nini kitatokea ndani ya miaka kumi ijayo endapo blogs zitaendelea kukua kwa kasi hii?
FM: Blogu ni hatari. Blogu inazidi kuwapa wananchi kijiko cha kuchotea na kula chakula…ajabu kuna magazeti hapo nyumbani bado yanaogopa blogu na hayazipi nafasi yake. Huku Uzunguni vyombo vya habari vimeanza kuona umuhimu wa blogu na kuzitumia. Ndiyo maana wanaziita Citizen Journalism. Maasi ya Burma mwaka jana yaliletwa na wanablogu kabla ya wanahabari wa kawaida. Mtu yeyote anaweza kuelezea alicho nacho.
Mimi nimeamua kuwa na blogu mbili kwa kuwa hutumia lugha mbili kuandikia nyumbani (kimuziki hutunga lugha kadhaa pia) yaani Kiingereza na Kiswahili. Tanzania tunatumia lugha hizi mahsusi, na sipendi kuzichanganya; ndiyo maana blogu ya Kitoto ni ya Kiswahili. Nalenga nyumbani na ile ya Kiingereza nalengesha wasomaji wowote duniani watakaotaka kunisoma. Sipendi kujiwekea vikwaazo kama mwandishi…
Kuhusu suala la nini kitatokea baada ya miaka kumi…swali muhimu. Maana dola na serikali zitaamua (hata kabla ya hiyo miaka kumi kwisha) Kuzikamata. Ukweli dunia yetu inatawaliwa na wale wenye nguvu za uchumi na dola. Mawazo au fasihi yeyote inayohatarisha maslahi ya wenye nguvu lazima itazimwa.
Ukiangalia kwa mfano suala la tovuti zilizoanza kama nyenzo binafsi (My space au You Tube) leo zimeshanunuliwa na mabepari wakubwa (aliyenunua My Space) ndiye anayemiliki magazeti kama The Sun (hapa Uingereza gazeti hilo linasifika kwa kutojali sana maslahi ya wananchi hasa wasio weupe) sasa ikiwa watu hawa wanaona mahali pana fedha basi wananunua. Hilo ni suala la kiuchumi. Suala la kisiasa. Suala la mabavu.
Kadri tunavyoendelea ndivyo kadri blogu zitakuwa na nguvu. Wanablogu wataanza kuwa na sauti kali wataanza kutetemesha wenye nchi na vyombo vya dola vitaamua kuwasimamisha. Mchukue mwenzetu Saidi Yakubu. Blogu lake lilikuwa likiwika. Kalianza mwezi wa nne mwaka jana tulipofika mwezi wa Kumi akaanza kuwa maarufu sana.Wakubwa wake wa kazi wakamwambia linaingiliana na kazi yake. Hapo unaona mfano. Hakuna uhuru wa kudumu dunia yenye wanaotawala na waliotawaliwa. Kwa sasa blogu ni sauti ya wanyonge , sauti ya waandishi huria, lakini dunia si laini kama siagi. Ingekuwa laini na tamu kama fenesi kusingekuwa na vita wala viwanda vya bunduki na mabomu.
BC: Ungeshauri nini basi kifanyike ili blogs na vyombo vya habari vya kawaida visikingane bali vishirikiane kama ambavyo nchi za wenzetu magharibi vishaanza kufanya?
FM: Dunia ya leo ni dunia ya mawasiliano. Hatuko enzi zile ambazo kiza kilitawala na viongozi wakawakata mikono waandishi (kama mafashisti walivyomkata mwanamuziki wa Chile, Victor Jara mwaka 1973).Dunia ya leo ni dunia ya teknolojia na habari.
Tatizo la baadhi ya vyombo vyetu vya habari (ukiacha labda Mwananchi wanaotangaza blogu) haviendi na wakati. Si shauri ya umaskini wa rasilimali bali umaskini wa kimawazo. Na haikuanza leo. Toka zamani. Hata nilipokuwa naanza uandishi wa habari hali ilikuwa vile vile. Uzuri mkubwa wa ubepari ni kukua kwa mawazo na uhuru huria wa kujieleza. Hapo hapo uhuru huu una mipaka. Anayetawala uchumi ndiye bosi; kwetu wanablogu lililopo ni kujiendeleza kila siku; kukimbia na kujua teknolojia.
Leo hapa Uingereza wametangaza vyombo vipya vya kuwacheki magaidi wanaopita pita katika matreni ya chini na vyombo vya usafiri. Aliyetengeneza zana hizi anaiuzia pia Marekani, na bwana usalama mmoja huko kwa Rais Bush kasema safi sana. Akaongeza kusema kuwa lazima tuwe hatua moja mbele ya magaidi. Lakini anasahau kitu kimoja.Siri ya ugaidi ni kutokuwa na usawa duniani; kuwepo maskini na matajiri. Blogu zikipigwa marufuku au kuwekewa pingu, wananchi hawatalala, wataendelea kugundua. Pale penye mchana pana usiku; penye hapana pana ndiyo, penye mwanamke pana mwanaume, penye njaa pana umaskini, penye tajiri pana mlala hoi.Uwiano huo ndiyo unaoongoza uhai. Kifupi basi blogu ni hatua fulani za harakati za mwanadamu kujiendeleza na kujieleza. Kwa sasa ni kiwango cha juu sana cha sauti ya mwanadamu.
MWISHO WA SEHEMU YA KWANZA YA MAHOJIANO YETU NA FREDDY MACHA.HUTAKI KUIKOSA SEHEMU YA PILI.STAY TUNED.
Kwa habari zaidi kumhusu Freddy Macha usikose kutembelea tovuti yake kwa kubonyeza hapa. Blog za Freddy Macha unaweza kuzipata kwa kubonyeza hapa na hapa.
Feedback / Comments
29 Responses to “KWA KINA NA FREDDY MACHA”
Leave a Reply


Mahojiano haya ni mazuri mno kuliko mengine meengi niliyoweza kupitia kwenye blogu hii ya Bongo celebrity,Kaka Freddy ni mwandishi na msanii mahiri.
Maandishi yake mengi yanabeba mafundisho na historia ya jamii ya nchi hii na dunia kwa ujumla,
Ushauri mdogo kwake na kwa waandishi na wasanii waliobobea kama yeye..tujiulize tunafanya nini ili Jamiii ya kizazi cha sasa na kijacho waweze kujifunza hasa kutokana na kazi zetu?Vipi tukianzisha shule,au vituo vya sanaa hasa katika maeneo ya vijiji au miji midogo midogo
Heshima yako kaka Freddy.
Bc mliyosema yote juu ya Freddy hakika nakubaliana na nyie.Ni moja ya hazina nzuri tuliyonayo.
Najua tulio wengi utamaduni wa kujisomea vitabu unazidi kututoka lakini ukipta wasaaa siku moja ya jpili nunua mwananchi upitie moja ya makala zake,hakika hutapenda kuzikosa.
Kila la kheri kaka Freddy.
Edwin Ndaki hapa
Brother Fredy pole kwa misuko misuko na hongera kwa kufika apo ulipo brother yote hayo ni harakati za kutafuta maisha nimependa style yako ya maisha.Keep it up.
MCHAGA, MCHAGA TU PESA MBELE BABA ANGU,KWELI IKO KWENYE DAMU DU! HATA MARAFIKI ZAKO ULIWATOZA PESA? KWA KUWAANDIKIA BARUA ZA WAPENZI WAO? YE UWIII! NI PESA KWENDA MBELE HA HA HA!
Hawa watu wenye vipaji kama hivi hawataki kuishi Tanzania, ndo maana cousin wake na fred bwana Ndesanjo Macha anaendeleza harakati za kimapinduzi za walalahoi akiwa Marekani. walalahoi si inabidi uwafate walipo? au ni walalahoi wangapi wanaweza kuja kwenye blog kama hizi na kusikia mawaiza ya watu muhimu kama hawa. I hope Fred na mdogo wake ndesanjo wana mpango wa kuzuru africa, at least twice a year kuonana na walalahoi hasa kule mgombani kwetu. cheers.
BC..habari za asubuhi.
Naomba kuuliza,maana hapa nilipo ni saa 0530am na huko Tz ni 0630am.
Nyie mnafanya update saa ngapi?
Siku nyingine mnakuwa fasta kubadili page,siku nyingine mnachelewa.Jamani hamtutendei haki sisi tunaotumia ka muda ketu finyi kuja na kukuta hakuna jipya.
Ila kila la kheri pamoja.
Nakubaliana na Any,Jamani kwanini Kina Freddy na kina Ndesanjo mnatumia vipaji vyenu ugenini?Vipi kwani hapa nyumbani mbona siku hizi ni swafii tu,kila kitu kizuri na cha kisasa kinapatikana hapa,rudini nyumbani jamani.
Au mnaogopa mambo ya Tindikali kama ilivyotokea kwa wana halisi? “”sumu ya Uhuru wa Habari “
i salute you kaka fred,millionaire wa vipaji.
mungu akubariki.
Big up kaka fredy…. unasura ya kitoto kumbe bro chumvi umekula? nilikua nashangazwa sana na habari zako (kwenye mwananchi) nilihisi kuna mtu unamwibia material, kumbe kichwa kipo…… big up. Tunahitaji wana habari kama wewe wengi, mie sikushauri urudi bongo, wasije wakakumwagia tindikali bureee.
Tutakusomaga kwenye blog na vitabu vyako, mungu akuzidishie hekima busura na mawazo lukuki kwa ajili ya taifa lako la tanzania
ila mtuambie mahojiano hawamu ya pili mtaiweka lini kwenye hii blog ya jamii?
Mahojiano shule haya,nashindwa nianzie wapi kusema palinoga.Kuanzia mwanzo mpaka mwisho ni shule tupu.
Vijana tupo wapi?
[...] Soma sehemu ya kwanza ya mahojiano yake kwenye blogu murua ya BongoCelebrity. Ni Freddy Macha. Bonyeza hapa. [...]
Safi sana Jeff kwa kuamua kumhoji Freddy. Na asante Freddy kwa kutupa elimu, ushauri na maarifa. Nimebandika pale Jikomboe maana nadhani watu wengi wanapaswa kusoma mahojiano haya. Umeongea vizuri sana kuhusu magazeti kuogopa zana mpya hizi badala ya kuzitumia. Na umuhimu wa mwandishi kusoma waandishi wengine kukuza uelewa wake.
Freddy nakukumbuka. Nilikuwa mdogo sana, nilipoanza kusoma makala zako. Ulinifanya nidhamilie kuwa mwandishi wa habari ingawa ilishindikana. Twende zetu ulaya nilikisoma zaidi ya mara tano. Kwakweli miaka ile ilikuwa mitamu
asante sana kwa hiyo. Lakini naona kuwa nakala hii imeibiwa na Jambo blog network………
Hongera sana Freddy,
Kama walivyosema waliotangulia,kaka uandishi wako hauna kifani na ni hazina kubwa sana kwa Tanzania.Mungu akuzidishie.
Swali:una mpango wowote wa kutoa kitabu kingine baada ya “mpe maneno yake”?Tunasubiri kwa hamu kubwa.
Ni kijana tu wa chuo fulani cha takwimu hapa bongo lakini ni mfuatiliaji mzuri sana wa makala zako mbalimbali uzitoazo mjomba hongera sana mungu azidi kukujalia afya ili utupe mada nyingine zaidi na zaidi
swali; waandishi wa habari kwa upeo wangu naamini ni chachu ktk maendeleo ya nchi husika je wewe tangu uanze kazi hii unaona ni mangapi umesaidia ktk kuendeleza nchi yako(tz)? hususani ktk janga la umaskini, ukimwi, rushwa, malaria n.k.
Freddy Macha ni hazina muhimu sana kwenye fani ya uandishi, pia ni ”multimedia machine under one roof”, kwa kweli ukiwa nae unajifunza mengi sana.
Kama mwandishi mahiri wa enzi hizo tumejifunza mengi sana, hongera sana BONGO CELEBRITY kwa mahojiano haya, bring on some more!!
Nakumbuka Mwaka 1984 nikiwa na Miaka 10 hivi nilisoma kitabu chako sijui ni kile chaitwa TWEN’ZETU ULAYA nikiwa kinda bado lakini bado naweza kukumbuka msitari huu “Nimetoka kazini nikafika nyumbani nikala Ugali kwa Mchicha na kipande cha Papai…” Mara Nghhhhhh NACHEUA KIBWEGE” mwisho wa kunukuu… kwakweli msitari huo ulikua unanikuna sana hasa ilo suala la kucheua kibwege…
Kaka Freddy,
Aaaah nimekubali ndugu yangu.Historia ya maisha yako ina msisimko mkubwa.Inatia hamasa ya watu kuvitafuta vipaji vyao na kuvitumia ipasavyo.Jamani hamna raha kama kuishi kwa kutegemea kipaji na elimu iliyoongezewa juu yake.
Kaka Fred kuna haja ya kuanzisha kampeni ya kuhamasisha usomaji.Ukipanda gari leo kwenda mkoani kutoka Dar, hebu tazama wangapi wanajishughulisha kusoma magazeti au vitabu ndani ya basi hilo.
Mungu akuzidishie afya njema.
Kaka Freddy usisahau kunitafutia mtoto wa kizungu pale London.Nataka kuoa nami.
Moses Gasana.Dar es salaam
Fred Macha.
I am a professor of literature. Currently in the US, but hopefully will join my friends; Mulokozi , Senkoro, Tumbo, etc at UDSM, sooner than later. Macha, you are visionary, almost prophetic. You are multicultural, multitalented, multidimentional in all areas of human expeprince. Your auntie, Mrs. Materu, loved me dearly and protected me from Asian( Mr. Pattan) persecution. Mike Sikawa, Patrick Msikinya, Thabiso Leshoayi, etc, were all my best friends even as I belonged to the generation of Jakaya and Mulokozi. Do you remember Walter Rodney? He was my friend and mentor. I am planning to visit his family in Guyana.
Fred, get in touch and interview me anytime. I have things I want to say.
Gobbo.
Tunapaswa kujifunza vijana wa sasa kupitia kwa macha hususani yale mazuri yake aliofanya na anayofanya haswa kwenye taaluma hii ya uhandishi sio tumsifie mtu pale anapokuwa ametutoka duniani ndio tumpe sifa ule ni unafki kaka mimi nakupa heshima zote wewe ni mmoja wa watu muhimu katka taifa hili la tanzania haswa sisi wapenzi vitabu makala haswa mimi nilikuwa mpenzi sana wa makala zako za kwenye gazeti la the guardianLATER from LONDON na sasa hivi makala zako za kwenye mwananchi ya kila jumapili kama ile KAMPENDA FULANI ANATAKA JUJU LA KIBONGO hiki kisa nilikipenda sana big pia unachangia kiasi fulani kukuza kiswahili
mimi niko ujeremani nina adisi nyingi zenye nitataka kuwapa voll geill mann ich komme aus tanzania
Vipi Mzee Macha!
Jama, ilikua ni vizuri kukuona kwa ile function ya Chinua Achebe’s “Things Fall Apart” pale SOAS earlier leo njioni.
Nitakubia simu, kuasiliana nawewe kuhusu jambo flani ndugu yangu…
Shukrani and zindi kuendelea!
Hi brother Freddy! Makala unayotoa kwenye gazeti la Mwananchi is very interesting! I real like it.
Ninamfahamu Fredy Macha kwa miaka zaidi ya thelathini (30). Ni kijana mwenye macho ya upeo wa hali ya juu pia ana falsafa yenye mikakati ya kuwafungua vijana macho ili wawe wazalendo murua.
Bwana Macha umenifungua macho, asante sana kwa mawazo yako mazuri. Naomba email yako.
Big up kaka Freddy mimi mwenyewe mambo hayo unayoyafanya nayapa mikono yote miwili napenda kazi hizo kutoka kwenye damu naomba emael yako niweze kukuuliza mengine vizuri.
kwaheri kaka fre…
Isaya,
Asante kwa mchango wako.Tutampatia Freddy e-mail yako.Atawasiliana nawe.
KWA mashairi yako,nimekubali walikuwa wanahaki ya kukulipa pesa,.ZARINA..WEMBE UMEMKATA MDUDU..MDUDU ANACHEZA KIDUDU?….TUWASUJUDU WALE WANAOTUABUDU..MACHO YAKE YA KITUNGUU,YAMEJAA PENZI KUU…TUWATUNUKU WALE WANAOTUTUNUKU..
kazi zako nziri ni fahari tosha ya kiswahili,..ambacho kimeanza kupoteza mwelekeo.hongera sana