Kama wewe ni mpenzi wa matangazo ya redioni,hususani ya idhaa za kigeni,basi jina la Mohamed Abdulrahman(pichani)kamwe haliwezi kuwa geni kwako. Huyu ni mmojawapo kati ya watangazaji mahiri na wakongwe ambao nchi yetu ya Tanzania inajivunia.
Mohamed Abdulrahman hivi leo ndiye Naibu Mkuu wa Idhaa ya Kiswahili ya Radio Deutsche Welle,inayorusha matangazo yake kutokea kule Bonn nchini Ujerumani. Radio Deutsche Welle siku hizi inarusha matangazo yake sio tu kupitia vituo mbalimbali vya redio nchini Tanzania na kote Afrika Mashariki na Kati bali pia mtandaoni.Unaweza kuyasikiliza matangazo yao kupitia mtandaoni kwa kubonyeza hapa.
Hivi karibuni tulipata fursa ya kufanya naye mahojiano haya tunayokuletea hivi leo.Kama ulikuwa unamjua Mohamed kwa sauti tu basi leo tuna furaha ya kukuletea sio tu mahojiano naye bali pia picha zake ili wakati mwingine utakapomsikia redioni uwe na picha kamili.Lakini pia ni lazima tukiri kwamba mahojiano na Mohamed ni mojawapo ya yale baadhi yenu wasomaji na wachangiaji wetu mnayoyaita “mahojiano-shule”.Unasoma mahojiano na kujifunza mambo kadha wa kadha iwe ni kuhusu jamii,historia,maisha nk.
Je unajua Mohamed ametokea wapi mpaka kufika hapo alipo?Kati ya Yanga na Simba yeye ni shabiki wa timu gani?Kwanini hatoyasahau kamwe mahojiano aliyowahi kufanya na marehemu Laurent Kabila(Rais wa zamani wa DRC)? Anasemaje kuhusu uhuru wa vyombo vya habari hivi leo?Akistaafu rasmi kazi ya utangazaji, anataka kufanya nini?Kwa hayo na mengineyo mengi,fuatana nasi katika mahojiano yafuatayo;
BC: Wakati mwingine huwa tungependa kuanza mahojiano bila kwanza kutaka kujua kuhusu historia ya maisha ya mtu tunayefanya naye mahojiano.Lakini kwa sababu hii ni mara yako ya kwanza hapa BC, hatuna budi kukuuliza.Unaweza,kwa kifupi tu,kutupa historia ya maisha yako?Ulizaliwa wapi,ukakulia wapi,ukasomea wapi nk?
MA: Nilizaliwa Iringa mwaka 1955 na ambapo tangu mapema miaka ya ´50 Marehemu Baba yangu alikuwa Mhandisi Public Works Department (PWD).Alihamishiwa huko kutoka Zanzibar. Miaka mitano baadae tukahamia Dar es salaam ambako tuliishi mtaa wa Ukami-Kariakoo.Nilisoma shule ya msingi kwanza Aghakhan na baadae Upanga (sasa makao makuu ya jeshi). Ama elimu ya Sekondari nilisomea Zanzibar St Joseph ( sasa Tumekuja ). Desemba 1974 , siku ambayo ilikua fainali ya kandanda kati ya Young Africans na Simba katika uwanja wa Amani kule Zanzibar, nikaelekea Uingereza na pia nilisoma nchini Urusi.
BC: Naona umeitaja Yanga kwanza, je una sababu yoyote ?
MA: Ni siku ya kumbukumbu kwangu, iliyokuwa ufunguo wa maisha yangu ya baadae na labda kwa sababu nilikua tangu utotoni mpenzi wa Yanga. (Tabasamu).
BC: Inaelekea ni mpenzi sana wa kandanda, je ni nani aliyeshinda mechi hiyo na ilikuwa ya ligi kuu au vipi?
MA: Kama sikukosea ilikuwa ni fainali ya kombe la kilabu bingwa Afrika Mashariki na Kati na Yanga ilishinda mabao 2-0 yaliyofungwa na Sunday Manara na marehemu Gibson Sembuli.
BC: Kila binaadamu huwa na hadithi au mikasa ya utotoni ambayo huwa haisahauliki.Kwa upande wako,ukikumbuka maisha ya utotoni,kabla ya kufikisha miaka kumi hivi,nini huwa kinakujia kichwani kwako mara moja?Unakumbuka mkasa gani?
MA: Kwa kweli kuna kumbukumbu nyingi. Kama nilivyoeleza awali kwa wanaoijua Dar es salaam, mtaa wa Ukami na New Street mpaka mtaa unaojulikana sasa kwa jina la Lumumba hadi Gerezani na kadhalika, yaani eneo zima la Kariakoo ndiyo iliyokuwa Dar es salaam. Kwanza kwa upande wa kisiasa, ilikua enzi ya msisimko mkubwa kwani ulikua muda mfupi tu baada ya uhuru na hivyo vigogo wote wa siasa za Tanganyika hadi Tanzania walikuwa wakionekana maeneo hayo mara kwa mara.Watu kama kina marehemu Amri Abedi, Eliufoo, Kambona, Kawawa, Songambele na wengine wengi. Sherehe muhimu zilikuwa zikifanyika sana makao makuu ya TANU mtaa wa Lumumba.Mtaa wa Ukami ulikua ni kandoni tu mwa hapo, hivyo kulikuwa na wahamasishaji kama Mzee Mwinamila, Geugeu na wengine. Kwa ufupi kisiasa ni kumbukumkbu kubwa sana kwangu.
Pili katika burudani na michezo, Kariakoo ilizaa (kama naweza kutumia neno hilo), wachezaji bora wa kandanda. Ninawakumbuka Abdulrahman Lukongo,Abdulrahman Juma, Emmanuel Albert, Arthur Mambeta, Isaac Marande, Mohamed Msomali,Boi Iddi Wickens, Kitwana Manara na hasa wachezaji chipukizi kama Kitwana Douglas, Jamil (Denis Law) Jumanne Hassan(Masimenti) Mohamed Bakari Tall na wengineo. Sasa kina Boi na Juma Bomba na Masimenti walikuwa wakitoka Shule ya Mnazi Mmoja , kituo chao cha kwanza ni Ukami ama wanatukuta tukicheza “ matatu kuondoka” au Kona” basi wanajiunga nasi kabla ya kuendelea na safari.
Wakati huo kulikuwa na timu ndogo ndogo nyingi mfano wa Saigon, Everton, Pool England, Young Kenya ,Dundee na Kahe ambazo zilizotoa wachezaji waliojiunga na timu kubwa za Yanga, Simba na Cosmopolitan na kufikia kiwango cha kuwa wachezaji wa kutegemewa kitaifa na kimataifa.
Na upande wa burundani ndiyo chimbuko la Western Jazz,Dar Jazz ama Kilwa Jazz. Upande wa magoma moto kama utakumbuka kulikua na Rifters, Sparks, Comics, Afro 70 na Safari Tripers ya marehemu Marijani. Ukipendelea taarab kulikua na Egyptian Musical Club, New Extara na Al Watan. Kwa kweli kumbukumbu ni kubwa na ndefu.
BC: Sasa ukikumbuka hayo kwa upande wa michezo , ni kitu gani ambacho utasema unakifikiri sana na labda hata kusikitika kwamba mambo hivi leo hayapo kama yalivyokuwa?
MA: Nafikiria sana kipaji cha wachezaji wa kandanda enzi zile na hasa miaka ya 70 na 80, kwa sababu baadhi walikuwa na vipaji vya kiwango cha juu kuliko baadhi ya wachezaji wa-kiafrika wanaovuma leo katika ligi za Ulaya. Mchezaji kama Maulidi Dilunga, Sunday Manara, Abdullah Kibaden au kwa upande wa Zanzibar, Salhina Maftah (kwa kuwataja wachache) hawa ni wachezaji ambao kama wangekua wanacheza leo basi nafikiri Tanzania ingeshika nafasi ya kwanza ya kuwa na wachezaji wa kulipwa nchi za nje.
Page 1 of 6 | Next page