Waswahili tunao msemo usemao, Siku njema huonekana asubuhi. Ni msemo wa kale ambao tafsiri yake halisi inaweza kutofautiana baina ya mtumiaji mmoja kwenda mwingine. Huo ndio utamu wa lugha na misemo ya kwetu. Tunaweza kutofautiana lakini wote tukawa sahihi, angalau kwa mapana yake.
Pamoja na tofauti kadhaa zinazoweza kujitokeza katika tafsiri, nina uhakika kwamba wengi tutaelemea katika tafsiri rahisi ambayo ni kwamba unavyoianza siku ndivyo utakavyoimaliza. Hisia na vitendo vyako unapoianza siku yako vina mengi ya kusema kuhusu itakavyokwenda na itavyofikia ukingoni.
Ukiamka na kujihisi mchovu,ukaichukia siku hata kabla haijaanza,ni wazi kwamba utakuwa umejiweka mwenyewe kwenye mtego wa kuwa na siku mbaya! Hutofanikisha malengo yako.Kazini unapokwenda mambo yanaweza kwenda mrama.Kwanini? Umeiandaa vibaya siku yako.Ikitokea mwenzako fulani iwe kazini au shuleni akakuambia mbona leo unaonekana kama unaumwa au umechoka(hata kama anakutania tu) ndio kabisaaa anakuwa amekumaliza.
Kwa upande mwingine, siku njema huonekana asubuhi unaweza kuwa msemo unaoonyesha nguvu ya utabiri tuliyonayo sisi kama wanadamu.Tunazo hisia.Unaweza kuhisi kwamba kitu fulani unachokifanya au unachoacha kukifanya kinaweza kuwa na matokeo yasiyopendeza. Kila mmoja wetu anazo nguvu za utabiri.Tofauti ni jinsi tunavyozitumia,kuziamini au kuzifanyia kazi.
Bahati nzuri ni kwamba binadamu tumepewa uwezo mkubwa wa kunyumbulisha dunia na mambo mbalimbali.Sasa ufanyeje ili uianze siku vizuri? Wataalamu mbalimbali wa mambo ya saikolojia na utabibu wanakubaliana kwamba ukiianza siku yako mapema, itakuwa nzuri! Kuanza siku mapema, kwa mapana na marefu kunajumuisha kuamka mapema na kuwaza vyema.
Leo nimeamua kuongelea umuhimu wa kuamka mapema kwani kama nilivyotangulia kusema hapo juu,wataalamu wengi wanakubaliana kwamba kuamka mapema ni msingi wa kuwa na siku nzuri,maisha mazuri na kubwa zaidi,afya nzuri.Watu wengi ambao tunawaita “waliofanikiwa maishani” na hata matajiri wakubwa hapa duniani,wanalo jambo moja linalofanana. Katika kuwafuatilia(kupitia makala za magazetini,vitabuni na hata mahojiano yao katika televisheni) wote wanakiri jambo moja.Wote ni wa kwanza kudamka(early birds). Kwanini?Bila shaka kuna sababu.
Pengine baada ya kusoma kichwa cha habari umeshajiuliza; kwanini niamke mapema? Sababu ya Kwanza ni kwamba unapoamka mapema, unapata muda mzuri wa kujiweka sawa,kuipanga siku yako vyema. Imeshawahi kukutokea ukakurupuka usingizini na kukuta muda umeshakwenda na umechelewa kwenda unapotakiwa kwenda iwe ni kazini,shuleni au kwingineko? Umeshaona jinsi mpangilio wako wa mambo unavyokwenda kombo? Unapofika ofisini kwa mfano, unakuwa hata kuamka vizuri hujaamka bado na kila mtu anakutolea macho kwa sababu hata nywele hukukumbuka kuchana? Ungeamka mapema,ukaipanga siku yako vyema yote hayo yasingekukuta.
Faida ya pili ni kuweza kutumia ukimya wa asubuhi. Umeshawahi kudamka asubuhi ukaona jinsi palivyo na utulivu wa aina yake? Amini usiamini,ukiutumia ukimya huo wa asubuhi kuwaza na kupanga mambo yako,ni wazi kwamba utafanikiwa zaidi. Akili ya binadamu imetengenezwa ifanye vizuri zaidi panapokuwa na utulivu. Wenzetu wa magharibi ndio maana wakaja na msemo wa Silence is Golden.
Tatu,wataalamu wa afya wanasisitiza sana kuhusu kifungua kinywa(breakfast). Huo ndio mlo muhimu zaidi katika siku. Ni wazi kwamba ukiamka mapema, utapata muda mzuri wa kuandaa na kisha kupata kifungua kinywa kwa utaratibu unaofaa bila papara kitu ambacho ni muhimu kwa afya yako. (more…)
Bila shaka umeshawahi kusikia msemo wa wenzetu wa magharibi usemao “Time is Money”. Yawezekana kwamba msemo huo,kwa tafsiri ya moja kwa moja, unamaanisha kwamba muda ni pesa. Lakini ninavyoelewa mimi msemo huo unaongelea au unajaribu tu kuonyesha jinsi gani muda ni kitu cha thamani! Jinsi unavyoutumia muda wako hivi leo ni ishara tosha ya jinsi kesho yako itakavyokuwa.
Kwa upande mwingine umeshawahi kusikia mtu au watu fulani fulani wakilalamika kwamba “hawana muda” wa kufanya kitu fulani. Sababu itolewayo mara nyingi ni kwamba wapo “bize”. Wapo ‘bize” na ndio maana hawana muda wa kujitolea katika shughuli mbalimbali za kijamii.Ndio maana hawana muda wa kikao cha harusi cha rafiki,ndugu au jamaa.Hawana muda wa kuhudhuria msiba wa mtu. Wapo “bize” na ndio maana hawakuweza kukupigia simu nk.
Sasa inakuwaje mtu mmoja awe na muda na wakati huo huo mtu mwingine asiwe kabisa na muda wakati sote tunaishi kwenye dunia moja na siku ina masaa yale yale 24? Sababu zinaweza kuwa nyingi. Zingine zinaweza kuwa ni za visingizio tu.Zingine zinaweza kuwa za kweli na za uhakika.
Pamoja na hayo, jinsi unavyotumia muda wako, jinsi unavyopangilia mambo yako, ratiba zako nk, ni sababu ya kutosha kama una muda wa ziada wa kufanya mambo mengine mengi uyapendayo ikiwemo mapumziko, muda wa kukaa na wanafamilia yako, kufuatilia maendeleo ya watoto shuleni na lolote lile ambalo unapenda kulifanya lakini umekuwa hulifanyi kwa sababu au kisingizio cha ukosefu wa muda.
Leo tutaangalia baadhi ya mambo ambayo unaweza kuyafanya ili kuokoa muda ili kujipatia muda unaohitaji kwa sababu ambazo nimezitaja hapo juu;
- Anza siku yako mapema: Hili ni la msingi sana.Amka mapema. Ukiianza siku yako mapema, sio tu kwamba kuna faida za kiafya kama ambavyo tutakuja kuziongelea katika siku za mbeleni, bali unakuwa na muda wa ziada wa kuiandaa ratiba kamili ya siku yako. Kwa ujumla binadamu anatakiwa kulala kwa muda wa masaa nane. Siri ya kuamka mapema inaanza na kwenda kulala katika muda unaofaa ili upate hayo masaa manane. Kumbuka siku njema huonekana asubuhi.Ipe siku yako mwanzo mzuri.
-
Orodhesha mambo unayotaka kufanya: Ushasikia msemo usemao; Mali bila daftari hupotea bila kujua. Hali ni hiyo hiyo hata katika suala zima la muda. Unapoianza siku hakikisha umeorodhesha mahali kwenye kikaratasi au kidaftari chako cha kumbukumbu mambo yote ambayo umedhamiria kuyafanya katika siku inayokukabili.Katika zama hizi za sayansi na tekinolojia,simu nyingi za viganjani zina huduma ya kalenda ambayo unaweza kuitumia kuorodhesha mambo unayotaka kufanya kesho,mwezi ujao au hata mwakani.Zitumie.Andika pia na muda ambao ni lazima utimize mambo hayo.
Faida za kuorodhesha mambo unayotaka kufanya ni kwamba kwanza orodha hiyo itakuwa inakusuta. Itakuwa inakuuliza,ulisema leo utafanya hivi imekuwaje? Pili orodha hiyo hiyo itakupa pia nguvu au ari ya kutimiza malengo yako. Tatu na muhimu zaidi kama mada yetu ya leo inavyodai, utaokoa muda. Utafanya kila jambo kutokana na muda uliojipangia kwani orodha itakuwa inakuonyesha kwamba siku bado haijaisha na mengine yanakungoja.
Pia wakati unaandika orodha yako, kumbuka kuweka pamoja mambo ambayo yanaweza kufanyika kwa pamoja au katika muda huo huo.Kwa mfano, leo umepanga kwenda katika benki fulani kuomba mkopo wa biashara.Wakati huo huo umepanga kwenda kwa chakula cha mchana na rafiki yako anayefanya kazi katika benki hiyo hiyo. Hayo unaweza kuyatimiza kwa pamoja. Unaweza kumuona meneja wa mikopo wa benki na kisha baada ya kumaliza ukaenda na rafiki yako kupata chakula. Hakikisha tu kwamba rafiki yako sio huyo huyo tena ndio meneja wa mikopo.Hapo kutakuwa na harufu ya ufisadi.Unajua tena jinsi mambo yalivyo nchini mwetu hivi sasa.Kuwa makini. (more…)
Ujasiriamali ndio neno jipya. Kila mtu anaongelea habari za ujasiriamali. Pengine hii inatokana na wengi wetu kutambua kwamba nyakati zimebadilika na ujasiriamali ndio njia iliyo sahihi zaidi kama mtu anatamani mafanikio ya kweli maishani.Vijana ndio chachu zaidi ya ujasiriamali au naweza kusema ndio wanategemewa zaidi kuendeleza ujasiriamali hususani katika ulimwengu wa leo wa sayansi na tekinolojia.
Pamoja na nia nzuri walizonazo vijana, pengine ukiwemo wewe unayesoma makala hii, kipo kizingiti ambacho ni lazima watu wajifunze mbinu mpya za kukivuka. Kizingiti hicho ni aina ya elimu itolewayo mashuleni. Kwa bahati mbaya elimu zitolewazo mashuleni bado hazijawekwa katika msingi unaomuwezesha kijana kujiajiri au kwa maneno mengine kuwa mjasiriamali pindi amalizapo masomo yake.
Bado tupo katika ule mfumo wa kikoloni. Ukimaliza shule unachotakiwa ni kuanza kutafuta kazi. Zunguka jijini Dar-es-salaam kwa mfano, utakutana na vijana wengi wasomi waliohitimu katika vyuo vikuu mbalimbali nchini wakiwa wamebeba vyeti vyao kwenye vijifuko vya plastiki wakizurura kusaka ajira. Hakuna anayefiria kujiajiri kwa kutumia elimu aliyoipata chuoni. Kwanini? Ndivyo ilivyo. Elimu aliyopewa haikumuandaa.Utakutana na engineer wa umeme ambaye hajawahi kubadilisha hata balbu!(nimeongeza chumvi kidogo hapa lakini kuna ukweli ndani yake!) Amesomea nadharia zaidi ya vitendo. Utakutana na mwanafunzi mhitimu wa masomo ya kilimo na mazingira ambaye hajui shamba ni nini.Hilo ni kosa katika mfumo wetu wa elimu. Ni lazima serikali ichukue jukumu la makusudi kubadili mfumo huo.
Lakini wapo wengine wengi ambao wana nia ya kweli ya kuwa wajasiriamali. Wana nia ya kujiajiri. Leo tutaangalia jinsi gani mjasiriamali chipukizi aanzishe kampeni yake. Si ushasikia kwamba biashara siku hizi ni kujuana? Ujasiriamali pia. Ni muhimu sana kujua ni nani au ni wapi uende endapo mambo yatakwama. Siongelei wapi uende kutoa au kupokea rushwa.La. Nataka kuongelea kitu kinachoitwa na wenzetu wa magharibi “networking”.Kwetu sisi hiki ndicho tunachoita “mtandao”.Mitandao ya kijamii kama vile facebook,twitter,myspace nk ni sehemu nzuri ya kutengeneza network.Itumie vizuri.
Ni muhimu kutengeneza mtandao mzuri kama unataka kuwa mjasiriamali makini na hususani kama unataka kufanikiwa. Kumbuka kwamba hapa hatuongelei kubadilishana business cards peke yake bali kumjua mtu kwa nia njema ya kusaidiana.Kumbuka neno ni “kusaidiana” na sio wewe pekee kupokea msaada.Lazima pawe na nia njema ya kusaidiana.
Kabla sijaanza kuorodhesha mbinu mbalimbali za kutengeneza ‘mtandao’ wako, naomba nikwambie kwamba siri ya kwanza ya kuanza kuwa mjasiriamali ni maandalizi.Jiandae kwa mtaji,elimu(ya darasani na mtaani),mbinu za kibiashara nk. Pili hakikisha kwamba una mapenzi ya dhati na hicho unachotaka kufanya.Usiingie kwenye biashara au ujasiriamali kwa sababu tu umemuona fulani amefanya hivyo.Kuna umuhimu mkubwa wa kujitambua katika suala zima la ujasiriamali. Baada ya kusema hivyo,sasa tuingie kwenye maeneo ya kutengeneza mtandao wako kama mjasiriamali;
- Washindani wako: Biashara ni ushindani lakini sio uadui.Kama unataka kuwa mjasiriamali mwenye mafanikio ni vizuri sana ukawajua washindani wako wa kibiashara.Pata vipeperushi vyao,tembelea tovuti zao,wajue wateja wao na kwanini hao watu ni wateja wao.Kisha jitambulishe kwao.Najua hapa unasema;nijitambulishe?!! Ndio,jitambulishe.Kama nilivyosema ni washindani lakini sio maadui zako. Mshindani wako anaweza kukufaa pia.Anaweza kuzidiwa na kazi akakusukumia zingine.Jitambulishe,jenga uhusiano mzuri wa kibiashara.Isitoshe nyote mpo kwenye biashara moja,sekta moja.Ya kesho hamyajui.Kama kuna chama au ushirika wa watu waliomo kwenye eneo lako la ujasiriamali,jiunge. (more…)
Natumaini kwamba hujambo na unaendelea na mapambano ya maisha kwa ujasiri,bila woga wala dalili za kukata tama.Hivyo ndivyo inavyotakiwa.Kumbuka kwamba penye nia pana njia.Jifunze jambo jipya kila siku.Usipoteze muda bure.
Uchumi wa dunia bado haujatengemaa.Bado habari za makampuni kufungwa,kupunguza wafanyakazi,kufilisika na mambo kama hayo,tunazisikia na tutaendelea kuzisikia.Hatujui lini uchumi utarudia hali yake ya kawaida au tuseme ilivyokuwa miaka kadhaa iliyopita.Hakuna anayejua kwa hakika.Hata Rais Obama hajui. Kilichobakia hivi sasa ni imani tu kwamba huenda kesho ikawa bora kuliko jana.Imani.
Kwa sababu ya kuyumba huko kwa uchumi,wengi wameshapoteza kazi zao na wengi zaidi wapo mbioni kupoteza.Lakini kupoteza kazi sio mwisho wa maisha.Kwa ufupi ukipoteza kazi uliyonayo hivi leo,huo ni mwanzo wa mbio za kutafuta kazi nyingine.
Kwa maana hiyo wengi wanaopoteza,kuachishwa au kuanza kutafuta kazi hivi leo,wanahitaji mbinu za kushinda mtihani wa usaili(interview). Leo nitaongelea jinsi ya kujiandaa kwa ajili ya usaili,jinsi ya kujiongoza wakati wa usaili nk.
Kabla sijakuambia ninachotaka kukuambia,naomba nikwambie jambo moja la msingi.Ushindi katika jambo lolote hutokana na jinsi unavyojiamini.Kujiamini hata wakati wa usaili ni jambo la msingi na ambalo lazima ulizingatie.Lakini kumbuka kujiamini hakumaanishi kiburi,majivuno au maringo.Ninaposema kujiamini ninamaanisha kuwa na uhakika na unachokisema na kuonyesha kwamba una uhakika bila majigambo wala kiburi.
Umepata barua au simu kuhusu usaili.Zingatia yafuatayo;
-
Hakikisha umepata taarifa za kutosha: Mara nyingi upatapo barua au simu inayokuita kwenye usaili,mtu yeyote hujawa na furaha au msisimko wa ajabu.Ni ruksa kufurahi lakini kumbuka kuchukua taarifa muhimu(hususani kama habari hii inakujia kwa njia ya simu) kuhusu mahali utakapofanyiwa usaili(anuani,namba ya chumba,gorofa ya ngapi nk),muda na kama usaili huo utakuwa na watu zaidi ya mmoja au la.Taarifa kama hizo zitakusaidia katika kujiandaa.
-
Fanya uchunguzi kuhusu shirika/kampuni husika: Kabla ya kwenda kwenye usaili hakikisha kwamba umefanya uchunguzi wa kutosha kuhusu kampuni au shirika husika(research).Wanashughulika na nini,wateja wao ni kina nani,linamilikiwa na nani,lilianzishwa lini na kwa malengo gani.
Kama unamjua mtu au rafiki ambaye aliwahi kufanya kazi katika shirika au kampuni hiyo,mtumie ili kupata taarifa za ndani zaidi.Ufahamu wako kuhusu kampuni au shirika utawaonyesha wanaokufanyia usaili shauku uliyonayo kuhusu kampuni/shirika. Kumbuka tu kutojifanya unajua kupita kiasi.Bakia kwenye kiwango kinachostahili. (more…)
Leo naomba nianze kwa kukujulia hali.Natumaini hujambo na unaendelea vyema na maisha.Najua mihangaiko ni mingi.Vikwazo pia haviishi.Lakini hayo ndio maisha.Isingekuwa hivyo pengine wala usingetamani kuishi.Pamoja na mikwaruzo mbalimbali ya maisha,sote tunapenda kuishi.Hatutaki kuiaga dunia kamwe.Mwenzetu mmoja akiiaga dunia tunamlilia kwa uchungu.Ipo sababu.Niijuayo mimi ni matumaini kwamba kesho itakuwa bora kuliko leo na jana.Maisha yanaendelea.
Yupo mwenzetu mmoja ameniandikia na kuniambia kwamba yeye tayari ana kazi ambayo inamlipa kiasi fulani japo sio cha kutosha.Pamoja na kuwa na kazi,mwenzetu analalama kwamba amefanya kazi kwenye kampuni anayofanyia kwa miaka takribani kumi na hajapandishwa cheo.Anatamani kupandishwa cheo.Afanyeje ili apandishwe cheo?
Kama ilivyo kwa mwenzetu aliyeuliza swali, wengi tunapenda vyeo.Ndio hulka ya binadamu. Kuna kuridhika fulani kunakotokana na kuwa na cheo kikubwa.Wakati mwingine haijalishi hata kama cheo alichonacho mtu hakiendani na kipato anachopata.Anachojali yeye ni kwamba yeye ndio Rais,Mkurugenzi Mkuu,Mkuu wa Mkoa,Mwenyekiti,Meneja nk. Kila mahali pana vyeo…hata jela kuna mfungwa mkuu nk.
Kwa wengi,cheo humaanisha kuongezeka kwa kipato.Cheo humaanisha mazingira mazuri zaidi ya kazi.Kama alikuwa kwenye kajiofisi kadogo basi anajua akipata cheo ina maanisha kuwa na ofisi kubwa na pengine hata kitanda cha kupumzika akichoka achilia mbali kuwa na luninga ofisini na mambo mengine kede.
Sasa ufanyeje ili upandishwe cheo.Leo tutaangalia mambo 7 ambayo mtu anaweza kufanya ili kupandishwa cheo.Lakini kabla sijaenda mbali sana,naomba nikutahadharishe kwamba mbinu ninazokupa zisiwe ndio muongozo wako.Lazima ujivike uhalisia(naturality) kwanza. Mbinu hizi ni kukusaidia tu.Ukizifuata kwa kanuni mpaka ukajisahau kwamba wewe ni nani na unatoka wapi,utatumbukia shimoni.
-
Fanya Kazi Yako Vizuri: Najua kwa wengi hili linaonekana kuwa wazi.Kama hufanyi kazi vizuri basi huwezi kupandishwa cheo.Au sio? Jibu ni kwamba ingawa huo ndio ukweli wapo watu wengi ambao hawafanyi kazi “vizuri” na badala yake wanafanya tu kazi ili mradi siku iishe aondoke zake akasubiri mwisho wa mwezi apate mshahara.
Kwa bahati mbaya,waajiri na watu walio na mamlaka ya kukupandisha cheo huwa wanaona hili kwa urahisi sana.Ipende kazi yako,ipende kampuni unayofanyia kazi. Weka uadilifu na maarifa ya ziada katika kazi zako.Cheo kitakuja.
-
Onekana: Kisichopo machoni ni vigumu kuwepo moyoni pia.Huo ni msemo mzuri na unaoweza kukumbusha umuhimu wa kuonekana.Unapokuwa kazini hakikisha kwamba watu(hususani wakuu wako wa kazi) wanakuona na wanaona kazi unayoifanya.
Usidanganywe na mtu anayekuambia kwamba ukionekana onekana unakuwa kama unajipendekeza.Hapana.Kama wewe ni mtu wa kujifichaficha,inaonyesha wazi kwamba hujiamini na hivyo hata ukipandishwa cheo kuna ulakini kama utayaweza madaraka yako mapya.Kwa maneno mengine,ondoa soni.Onekana. (more…)
Kuanzia wiki hii BC inaanzisha kitu kitakachokuwa chini ya kipengele cha BC MAARIFA.Kila mwisho wa wiki(jumamosi au jumapili)kutakuwa na makala kuhusu mambo mbalimbali ya maendeleo ya kimaisha na kibinadamu katika nyanja mbalimbali kama vile mahusiano,kazi,pesa,afya,familia nk.Kutakuwa kunatolewa dondoo mbalimbali zinazohusiana na maendeleo binafsi ya mtu(Personal Development.
Nia ni kupeana maarifa au ujuzi fulani fulani ambao unaweza kutusaidia sote kama watu binafsi au jamii.
Naomba tu niweke wazi kwamba hii ni Pilot Project kwa maana ya kwamba ni kitu ambacho tunakifanyia majaribio.Kama unapenda kipengele cha namna hii,tungefurahi kama utatuambia aidha kwa kupitia kwenye sehemu ya maoni au kwa kutuandikia e-mail.Kuendelea kwake kutategemea sana mchango wako.
Pia kama wewe ni mwandishi na ungependa kuandika katika mtindo huu huu wa Tips for Personal Development,usisite kutuandikia.Leo tunaanza na mada iliyopo hapo chini.Asante kwa ushirikiano.
KWANINI SIFANIKIWI VYA KUTOSHA?
Tamaa ya mafanikio katika maisha ni safari ndefu. Kwa wengi wetu ni safari ya kudumu. Kila mara tunataka zaidi. Tunataka kuwa kama fulani au fulani.Tunatamani kuwa na kiasi cha fedha kama au kuliko fulani.Kuwa na mke au mume mzuri na mwenye heshima kama fulani. Na kwa wale ambao maisha yao huendeshwa na tamaa za kuwa maarufu basi kila leo huwa wanataka kuwa kama mwanamuziki,muigizaji filamu,mwanasiasa fulani na vitu kama hivyo.
Ingawa ni vigumu sana kwa binadamu kufikia mahali ambapo anaweza kusema kwamba amesharidhika vya kutosha na alichonacho na hataki nyongeza yeyote zaidi,yawezekana kabisa mtu akafikia mahali pa kuridhisha ingawa hiyo haimaanishi kwamba akipata nafasi ya kupata zaidi hatoitumia. Hapa tunaweza kusema mtu anakuwa ameridhika kwa kiasi cha hali ya juu.
Lakini kwanini basi baadhi yetu tunashindwa kufikia japo robo tu ya mafanikio tunayoyatamani? Ni mambo gani yanatukwamisha? Leo nimeona tuongelee kidogo sababu kadhaa ambazo zinatufanywa wengi wetu tukwame na hata kuishia kulaumu watu wengine bila kutambua kwamba yawezekana sababu sio ukosefu wa elimu ya kutosha,mtaji wala chochote kile bali sisi wenyewe;
-
Hujiamini vya kutosha: Ukijaribu kuangalia au kufuatilia maisha ya watu ambao sote tunaamini kwamba wana mafanikio zaidi yetu utagundua jambo moja muhimu;Wanajiamini.
Wanaamini kwamba wanalo jambo au mambo ya msingi wanayoweza kuchangia katika jamii. Wanajiamini na wana madhumuni ya makusudi kuhakikisha kwamba jamii itawakumbuka.
Watu hao pia huwa ni wajuzi wa kuketi chini wakajikosoa wenyewe na kisha kusonga mbele zaidi na zaidi.
Je wewe hapo ulipo una kitu gani cha kipekee? Unayo maarifa au ujuzi (skill or talent) gani maalumu ambao hujaufanyia kazi kwa sababu ya kutojiamini tu? Kwanini usiamke leo ukaanza kujiamini zaidi kisha uone jinsi utakavyobadilisha muelekeo? (more…)

Happy New Year! Kheri Ya Mwaka Mpya! Naam ni mwaka 2010,karne ya 21.Binafsi napenda kukupa pongezi kwa kuumaliza mwaka 2009 na kuingia mwaka 2010.
Nakupa hongera nikiwa na sababu nyingi.Baadhi yake ni kwamba,kwa wengi mwaka 2009 ulikuwa ni mgumu kupita kiasi.Hali mbaya ya kiuchumi iliyoikumba dunia,ni sababu tosha ya kuufanya mwaka 2009 kuwa mgumu.
Isitoshe,tumepoteza wapendwa wetu wengi,ndugu,jamaa na marafiki.Mfano ni hivi leo,tunaomboleza kifo cha Mzee wetu,Rashid Mfaume Kawawa. Maradhi mbalimbali,mengine yakiwa mapya kama vile H1N1 (homa ya mafua ya nguruwe),yaliikumba dunia na kuleta mtikisiko wa aina yake.Hofu ikatanda ulimwenguni.Wengi wamepoteza maisha katika vita na mashambulizi ya kigaidi na kujitoa mhanga.
Wakati bado tunatafakari yaliyojiri katika mwaka 2009,naukumbuka msemo wa wahenga wetu.Yaliyopita si ndwele,tugange yajayo.Ni mwaka mpya na ni nafasi nyingine ya kuanza upya,kuweka malengo mapya,kumalizia ya zamani.Ni wakati wa kujipanga upya kuzikabili upya changamoto mbalimbali za maisha na ubinadamu.
Unapouanza mwaka mpya na kama unataka au umeshajiwekea malengo, kumbuka yafuatayo;
- Orodhesha malengo yako. Tafuta mahali penye utulivu.Chukua kalamu na karatasi kisha orodhesha malengo yako.Kisha pembeni ya malengo,orodhesha mambo ambayo unatakiwa kufanya(actions) ili kutimiza malengo uliyoorodhesha.Jaribu kuorodhesha malengo machache.Kumbuka mtaka yote,hukosa yote.
- Weka malengo halisi.Je malengo uliyoorodhesha hapo juu ni halisi? Ninaposema halisi namaanisha weka malengo yanayokabilika.Usiweke malengo yaliyozidi kiwango au yasiyotimia kimsingi.Kwa mfano,ukiweka malengo kwamba mwaka huu unataka kuwa tajiri kupita watu wote duniani wakati hivi leo akiba yako benki ni ya kiwango duni,utakuwa unaweka malengo yasiyo halisi.
- Jiamini kwamba unaweza kutimiza lengo/malengo yeyote uliyojiwekea.Kujiamini kunaenda sambamba na imani.Ukiamini kwamba inawezekana,utaweza.Kama sio leo basi kesho.Piga taswira kichwani kwako jinsi itakavyokuwa ukitimiza malengo yako.
- Fanya tathmini ya mara kwa mara juu ya malengo yako na mwenendo mzima wa kuyatimiza.Ukiona hauelekei kuyatimiza,usiingiwe na hofu ya kuyafanyia marekebisho.Siku hazifanani na mazingira hubadilika.Malengo pia yanaweza kubadilika.
- Mwambie ndugu au rafiki wa karibu kuhusu malengo yako.Naelewa…unataka malengo yako ya mwaka huu yabakie siri.Ninachotaka kukuambia ni kwamba unapomwambia ndugu au rafiki yako wa karibu unayemwamini kuhusu malengo yako,unakuwa umejipatia msaada.Ndugu au rafiki huyo atakuwepo kukukumbusha au kukusaidia,kwa njia moja au nyingine,kutimiza malengo yako.Isitoshe,kwa kumwambia ndugu au rafiki,unakuwa umejitilia chachu ya kutimiza malengo yako.Utaonekanaje kama mwisho wa mwaka utakuwa hujatimiza yale uliyotaka kutimiza? Binadamu tumeumbwa na soni.Itumie.
- Orodhesha watu wa kukusaidia. Kutimiza malengo kunaweza kuwa kitu kigumu.Unaweza kuhitaji msaada ili kutimiza malengo.Usisite kufanya hivyo.Weka mahali orodha ya watu ambao unadhani wanaweza kukusaidia pindi utakapohitaji msaada katika kutimiza malengo yako.Wengine wanaweza kukusaidia kimawazo au kimtazamo(role models).Watumie ipasavyo.
- Jipongeze. Kutimiza lengo au malengo ni jambo la furaha.Linastahili pongezi.Kila unapotimiza lengo au malengo fulani,usisahau kujipongeza.
- Usisahau kumweka Muumba mbele. Hata kama huna imani,huamini wala kuabudu kufuatana na dini au dhehebu lolote,bila shaka tunakubaliana kwamba yupo aliye juu,aliyetuumba.Usimsahau.
Nakutakia kila la kheri katika mwaka mpya wa 2010. Enjoy.

