MY TANZANIA   |   PLACES TO GO   |   MEDIA   |   ONLINE ENTERTAINMENT    

123Kawawa

Mzee Rashid Mfaume Kawawa,amefariki! Kwa mujibu wa vyanzo mbalimbali vya habari zikiwemo blogs,Mzee Kawawa amefikwa na mauti katika Hospitali ya Rufaa ya Muhimbili ambako alikuwa amelazwa.

Rashid Mfaume Kawawa alikuwa Waziri Mkuu wa kwanza nchini Tanzania na baadaye kuwa Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi.Alizaliwa mwaka 1926 katika kijiji cha Matepwende Wilaya ya Songea Mkoani Ruvuma Tanzania. Alianza elimu ya Msingi huko Liwale -Lindi mnamo 19411942 na kuendelea na masomo ya sekondari katika shule ya Dar es Salaam Secondary School.

Ni hivi karibuni tu Mzee Kawawa alizindua kitabu kinachoelezea maisha yake.

Kawawa12

Majuzi Rais Kikwete na mkewe Salma Kikwete,walikwenda Muhimbili kumuona Mzee Kawawa.Laiti wangelijua kwamba hawatomuona tena Mzee Kawawa akiwa hai!

Kwa mujibu wa ratiba ya mazishi ambayo imetolewa,Mzee Rashid Mfaume Kawawa anatarajia kuzikwa Jumamosi nyumbani kwake Madale nje kidogo ya jiji la Dar-es-salaam.

You need to a flashplayer enabled browser to view this YouTube video

Mwili wa marehemu Mzee Rashid Mfaume Kawawa ukitolewa katika hospitali ya rufaa ya Muhimbili kwenda kuhifadhiwa katika hospitali ya jeshi ya Lugalo.Anayesikika akilia kwa uchungu ni mkewe Asina Kawawa.

KawawaEnzi

Rashid Mfaume Kawawa enzi za ujana wake.

KawawaMuungano

Utumishi wa Mzee Rashid Mfaume Kawawa kwa taifa letu ni wa siku nyingi.Pichani kulia anaonekana akishuhudia Hayati Mwalimu Julius Kambarage Nyerere akichanganya michanga ya ardhi ya Tanganyika na Zanzibar kuashiria Muungano.Hiyo ilikuwa ni mwaka 1964

KIMDJ mkongwe na maarufu nchini Tanzania,DJ Young Kim, amefariki dunia. Kwa mujibu wa blog ya Issa Michuzi, DJ Kim amefariki dunia akiwa katika hospitali moja ya binafsi inayojishughulisha zaidi na tiba za magonjwa ya moyo iliyopo Manzese jijini Dar-es-salaam.

DJ Young Kim ni miongoni mwa DJs waliochangia sana maendeleo ya disco na mashindano ya kucheza muziki(disco) ambapo ndipo yalipoibuka majina maarufu katika muziki kama vile Black Moses(RIP),Ommy Sidney,Othman DigaDiga na wengine wengi.

Pia kwa wale ambao wanafuatilia chimbuko la muziki ambao leo hii tunauita wa kizazi kipya,mchango wa DJ Kim kupitia mashindano ya Yo Rap Bonanza ,ulikuwa ni chachu muhimu katika mwanzo au mwendelezo wa muziki wa hip hop nchini Tanzania.Pumzika kwa amani DJ Young Kim.

Miss World

Kwa mara nyingine tena, Tanzania imetoka patupu katika kuwania taji la Miss World. Taji la mwaka huu limekwenda kwa mrembo kutoka nchi ndogo ya Gibraltar, Kaiane Aldorino(23). Mashindano ya mwaka huu ambayo yalijaa vionjo vya ngoma na wanenguaji wa kiasili,zilifanyikia nchini Afrika Kusini.

Nafasi ya pili ilikwenda kwa Miss Mexico,Perla Beltran Acosta huku ya tatu ikienda kwa Miss South Africa, Tatum Keshwar ambaye ndiye alishangiliwa zaidi pengine kwa kuzingatia kwamba yeye alikuwa anachezea katika “uwanja wa nyumbani”.

Jumla ya washiriki 112 walishiriki katika shindano hilo ambapo Tanzania ilikuwa inawakilishwa na Miriam Gerald mrembo kutoka jijini Mwanza,kaskazini mwa Tanzania.

Ukitaka kujua zaidi kuhusu nchi anayotoka Miss World mpya bonyeza hapa.

You need to a flashplayer enabled browser to view this YouTube video

TW

Mcheza golf maarufu ulimwenguni,Tiger Woods,kutoka nchini Marekani, ametangaza kupitia mtandao wake kwamba anachukua likizo isiyo na muda maalumu kutoka katika mchezo huo ili kujaribu kurekebisha mambo yake.

Katika siku za hivi karibuni,habari za Tiger Woods kupitia vyombo mbalimbali vya habari,amekuwa akihusishwa na habari mbalimbali za “ukosefu wa uaminifu” kwa ndoa na mke wake kwa kuwa na vimada mbalimbali.

Mpaka hivi sasa wanawake 13 wameshajitokeza na kudai walikuwa na uhusiano wa kimapenzi na Tiger Woods wakati tayari bingwa huyo wa golf duniani akiwa ni mwanandoa kwa mwanamitindo kutoka Sweden, Elin Nordegren.Wengi miongoni mwa wasichana hao wamekuwa wakijitokeza na ushahidi wa kueleweka zikiwemo text messages,voicemails ,e-mails na hata risiti za malipo.

Mapema hivi leo,ziliibuka habari kwamba Tiger Woods amewahi hata kujihusisha kimapenzi na malaya wa kulipia ambapo inasemekana alitumia zaidi ya dola $60,000 kwa huduma hizo.

“Baada ya kufanya tafakuri ya kina,nimeamua kuchukua mapumziko. Nahitaji kuelekeza nguvu zangu katika kuwa mume,baba na mtu bora zaidi” amesema Tiger Woods.

tiger-woods-and-elin-nordegren

Tiger na mkewe, Elin walioana miaka mitano iliyopita na wana watoto wawili;wa kwanza wa kike ambaye ana umri wa miaka miwili na wa kiume ambaye ana miezi kumi.Kuna habari kwamba Tiger Woods na mkewe wameamua kwenda nchini Sweden ili kurekebishia mambo yao huko. Mkewe ameripotiwa kununua jumba lenye thamani ya dola milioni 2 huko Sweden ambalo wadaku wanadai huenda ndio ikawa nyumba yao ya kuishi kwa hivi sasa.

Habari kwamba huenda Elin akaomba talaka kutoka kwa Tiger zimekanushwa na marafiki wa karibu wa wanandoa hao.

president

Rais wa Marekani Barack Hussein Obama ametangazwa kuwa mshindi wa Tuzo ya Amani ya Nobel kwa mwaka 2009. Hiyo ndio habari kubwa iliyopo kwenye vyombo vingi vya habari vikubwa ulimwenguni hivi leo.Hongera Obama.

Kwa undani zaidi wa habari hii unaweza kubonyeza hapa na hapa na hapa.

mpakanjia

Habari ambazo zimeingia punde na pia kupitia vyanzo mbalimbali vya habari vinapasha kwamba mfanyabiashara maarufu wa jijini Dar-es-salaam,Mohamed Mpankanjia maarufu kama Medi Mpakanjia, amefariki dunia hapo jana katika hospitali ya jeshi ya Lugalo jijini Dar-es-salaam.

Mohamed Mpakanjia alikuwa mume wa Marehemu Amina Chifupa,Mbunge kijana aliyefariki dunia miaka takribani miwili iliyopita katika mazingira ambayo yalikuwa ya kutatanisha.

Habari hii inaendelea na hivyo tutaendelea kukupasha kadri zinavyozidi kuingia.

hasheemt1bc

Kama uliwahi kutabiri kwamba siku moja mtanzania Hasheem Thabeet atakuja kuchezea katika ligi ya mpira wa kikapu ya NBA, unayo sababu ya kujidai kwani utabiri wako umetimia jioni hii(saa za New York).Hasheem Thabeet amechaguliwa kujiunga na timu ya Memphis Grizzlies yenye makao yake makuu huko Memphis katika jimbo la Tennessee nchini Marekani.

Hasheem anakuwa mtanzania wa kwanza kufikia hatua hiyo.Kama nchi tuna kila sababu ya kufurahia mafanikio yake na kumtakia kila la kheri. Hivi sasa anakuwa,bila shaka, “balozi” wetu katika ulimwengu wa michezo hususani mpira wa kikapu. Kila la kheri Hasheem.

michael-jackbc

Habari za uhakika ambazo BC imezipata zinapasha kwamba Mfalme wa muziki wa Pop,Michael Jackson,amefariki dunia huko Los Angeles nchini Marekani mchana huu.

Mfalme huyo wa Pop alikimbizwa hospitali mchana huu baada ya kuzimia akiwa nyumbani kwake maeneo ya Holmby Hills huko Los Angeles alizimia baada ya kupatwa na mshtuko wa moyo kitu ambacho kinasemekana ndicho kilichomaliza uhai wa Michael Jackson katika Kituo Cha Afya cha UCLA ilipotimia saa nane na dakika ishirini na sita (2:26pm) kwa saa za Los Angeles.

mj-jackson_1972b

Michael Jackson akiwa na umri wa miaka 13

Michael Jackson alizaliwa huko Gary,Indiana nchini Marekani tarehe 29 August mwaka 1958 akiwa ni mtoto wa saba kati ya watoto tisa wa Joseph na Katherine Jackson(wazazi wao). Alianza  kujishughulisha na masuala ya muziki akiwa na umri wa miaka minne(4) katika kundi la familia lililojulikana na kutamba kama Jackson 5(pichani).

jackson5

Kabla ya kufikwa na mauti,Michael Jackson, alikuwa anapanga kufanya show za mwisho huko London mwezi July mwaka huu.Tiketi kwa ajili ya show hizo zilikuwa zimeshakwisha(sold out)!

garyindianabc

Pichani ni nyumbani alipozaliwa Michael Jackson na ndugu zake huko Gary,Indiana nchini Marekani.Nilipiga picha hii December mwaka 2006 nilipotembelea maeneo hayo ili kujionea alipozaliwa Mfalme wa Pop.Mtaa ilipo nyumba hii unaitwa Jackson Street.

BC inapenda kutoa pole kwa wote ambao wameguswa kwa njia moja au nyingine na msiba huu.Tunaamini kwamba Michael Jackson alikuwa sio tu mwanamuziki maarufu ulimwenguni bali muziki wake uligusa wengi.Wengi walicheza,wanacheza na wataendelea kucheza miziki yake.

Hapa chini unaweza kusikiliza simu iliyopigwa kutoka nyumbani ikwake kwenda kwa watu wa huduma za dharura(Emergency)

Audio clip: Adobe Flash Player (version 9 or above) is required to play this audio clip. Download the latest version here. You also need to have JavaScript enabled in your browser.

 

chengebc1Mbunge wa Bariadi Mashariki,Andrew Chenge “Mzee wa Vijisenti” yupo matatani…tena.Safari hii ni kwa kupata ajali ya barabarani(kugonga) na kusababisha vifo vya watu wawili ambao walikuwa ndani ya usafiri maarufu kama “Bajaji”.Waliofariki inasemekana ni wanawake wawili ambao ndio walikuwa abiria katika Bajaj hiyo.Dereva wa Bajaj hajulikani alipo.

Tukio hilo limetokea alfajiri ya leo katika maeneo ya Oysterbay(karibu na nyumbani kwake).Kwa mujibu wa taarifa ya Kamanda wa Kanda Maalumu ya Polisi Dar-es-salaam, Afande Kova, Chenge alikuwa akiendesha gari aina ya Pick Up-Hilux yenye namba ya usajili T512 ACE.Bajaj iliyohusika kwenye ajali ina namba za usajili T736 AXE na imeorodheshwa kama mali ya Zuwena Feith Nassoro wa SLP 2595 Dar-es-salaam.

Baada ya tukio hilo,Mheshimiwa Chenge alijisalimisha katika kituo cha Polisi Oysterbay na anaendelea kuisaidia polisi.Habari hii bado inaendelea…

nyirendabc1

Kwa huzuni na masikitiko makubwa tumezipokea habari za msiba wa Major Alex Gwebe Nyirenda.Huyu ndiye shujaa aliyepandisha bendera ya Tanganyika huru na Mwenge wa Uhuru kileleni Mlima Kilimanjaro usiku ule wa mkesha wa Uhuru miaka 47 iliyopita.

Marehemu Nyirenda ambaye alikuwa akisumbuliwa na ugonjwa wa kansa kwa muda sasa, amefariki jana majira ya saa moja jioni(saa za Afrika Mashariki) katika hospitali ya taifa Muhimbili alikokuwa amelazwa.Mapema mwaka huu Major Nyirenda alipelekwa nchini India kwa matibabu zaidi kufuatia kudhoofika kwa afya yake.

Marehemu Nyirenda anatarajiwa kuzikwa siku ya jumatano ijayo katika makaburi ya Kinondoni jijini Dar-es-salaam.Msiba upo nyumbani kwake huko Mbezi Beach,Flats za National Milling karibu na njia panda ya kwenda Africana.

Ni siku chache tu zilizopita ambapo tuliweka mahojiano tuliyofanya na Major Nyirenda kuhusiana na harakati za uhuru,zoezi zima la sherehe za uhuru nk.Unaweza kuyasoma mahojiano hayo kwa kubonyeza hapa.

Katika mahojiano yale,Major Nyirenda aliongelea mambo mengi.Lakini katika mengi hayo pengine ushauri au usia aliotuachia wa kujitolea,uvumilivu na uaminifu ndio ambao hatuna budi kuufanyia kazi ipasavyo kwa minajili ya kumuenzi Major Nyirenda na pia kwa maendeleo yetu binafsi na jamii zetu.

nyirenda-3

Katika picha hii iliyopigwa mwezi wa pili (February) mwaka huu,inamuonyesha Major Nyirenda akiwa hospitali jijini Dar-es-salaam akihudumiwa na mkewe.Hii ilikuwa ni kabla serikali haijaingilia kati na kumpeleka nchini India kwa matibabu zaidi.Picha na Mpoki Bukuku.

Tunapenda kuungana na ndugu,jamaa,marafiki na watanzania wote kwa ujumla katika wakati huu mgumu wa kuondokewa na shujaa wetu,Major Alex Gwebe Nyirenda.Mungu ailaze pema roho yake milele na milele.Rest in Peace Major Nyirenda.


Read the Next Page →

↑ Go Back to Top of Page