Waziri Mkuu wa zamani wa Uingereza, Margaret Thatcher, amefariki dunia. Taarifa kutoka kwa msemaji wake ambayo imesambazwa na kuripotiwa na vyombo mbalimbali vya habari ulimwenguni, inasema kwamba Bi. Margaret Thatcher amefariki kutokana na ugonjwa wa kiharusi (stroke). Alikuwa na umri wa miaka 87.
Thatcher ambaye kutokana na uhodari na ushapavu wake uliomfanya awe mwanamke wa kwanza kushika wadhifa wa Waziri Mkuu nchini humo alijulikana miongoni mwa wengi kama “Iron Lady” jina ambalo alipachikwa na vyombo vya habari vya Urusi. Aliiongoza Uingereza kuanzia mwaka 1979 mpaka mwaka 1990 akiwa pia kiongozi wa chama cha Conservative chama ambacho alikiongoza tangu mwaka 1975 wakati huo kikiwa ni chama cha upinzani.
Bi.Margaret Thatcher alijiuzulu rasmi kutoka katika siasa na maisha ya utumishi wa umma mwaka 2002 baada ya kupatwa na ugonjwa wa kiharusi. Tangu hapo amekuwa akionekana kwa nadra hadharani na hata mwaka 2010 alishindwa kutokea katika sherehe maalumu ya siku ya kuzaliwa kwake aliyokuwa ameandaliwa na Waziri Mkuu wa sasa wa Uingereza, David Cameron. Mwishoni mwa mwaka jana alilazwa hospitali na kufanyiwa upasuaji wa kuondoa uvimbe katika kibofu cha mkojo.
Margaret Thatcher alizaliwa tarehe October, 1925 katika mji mdogo wa Grantham(mashariki ya Uingereza). Baba yake alikuwa ni mfanyabiashara wa bidhaa ndogo ndogo za majumbani na baadae Mayor wa Grantham. Alisoma masomo ya Kemia katika chuo kikuu maarufu cha Oxford. Baadae alisomea Sheria.
Mume wake alikuwa Denis Thatcher, ambaye kwa pamoja walikuwa na watoto mapacha, Mark na Carol waliozaliwa mwaka 1953. Mumewe alifariki Juni 2003.
Mazishi yake ya kitaifa yanatarajiwa kufanyikia St.Paul Cathedral London na baadae katika shughuli ya faragha ya kifamilia, atazikwa kwa mwili wake kuchomwa moto.
Mungu ailaze roho yake mahali pema peponi.
Mkutano wa Dharura ulioitishwa na wanachama wa klabu ya Simba umeung’oa uongozi wa juu wa klabu hiyo unaoongozwa na Mwenyekiti Ismail Aden Rage aliyepo kwenye matibabu nchini India.
TARATIBU ZA KIMAHAKAMA ZAMKWAMISHA KURUDI NYUMBANI LEO!
Mahakama Kuu ya Tanzania mchana huu imeweka wazi masharti ya dhamana ya msanii wa filamu anayejulikana zaidi kwa jina la Lulu,. Lulu ambaye jina lake halisi ni Elizabeth Michael anakabiliwa na mashtaka ya kuua bila kukusudia ya msanii mwenzake(ambaye inasemekana walikuwa na mahusiano ya kimapenzi), Steven Charles Kanumba, kilichotokea April mwaka jana huko Sinza-Vatican jijini Dar-es-salaam.
Kwa mujibu wa chanzo chetu kilichokuwepo mahakamani mchana huu, dhamana ya mwigizaji Lulu ipo wazi endapo tu atatimiza masharti aliyotengewa ambayo ni
- Kuwasilisha au kukabidhi hati yake ya kusafiria(passport)
- Kutosafiri nje ya Dar es salaam.
- Kuripoti mahakamani kila siku ya kwanza ya kila mwezi
- Kuwa na wadhamini wawili ambao kila mmoja atamdhamini kwa shilingi milioni 20 za kitanzania.
Pamoja na kwamba familia ya Lulu walikuwa wameshajiandaa kukabiliana na kutimiza masharti hayo, Lulu amerudi rumande leo kutokana na kwamba watumishi wawili wa serikali(Mahakama) ambao wanahusika na sehemu ya dhamana hiyo kwa upande wa sahihi za kimahakama, hawakuwepo Mahakamani hapo kutokana na kuwa safarini mkoani Pwani kikazi. Hata hivyo, kwa mujibu wa mawakili wanaomwakilisha Lulu, masharti yote ya dhamana wameshayatimiza na kinachosubiriwa ni huo uthibitisho na utaratibu wa kimahakama ili Lulu arejee nyumbani na kuendelea kukabiliana na kesi hiyo akiwa uraiani.
Kwa maana hiyo, uwezekano ni wazi kabisa kwamba Lulu ataachiwa rasmi kesho January 29, 2013.
Habari ambazo zimetufikia hivi punde zinapasha kwamba muigizaji na mwanamuziki, Hussein Ramadhan Mkieti almaarufu kama Sharo Milionea,amefariki dunia kutokana na ajali ya gari iliyotokea mida ya saa mbili usiku katika eneo la Maguzoni Songa katikati ya Segera na Muheza mkoani Tanga.
Habari za ajali hii na tukio hili la kusikitisha zimethibitishwa na Kamanda wa Polisi mkoani Tanga, Constantine Masawe. Kwa mujibu wa Kamanda huyo, gari aina ya Toyota Harrier lenye namba za usajili T478 BBR alilokuwa akiendesha marehemu kutokea Dar-es-salaaam kwenda Muheza lilipofika katika eneo hilo liliacha barabara na kupinduka na hivyo kusababisha mauti yake.Mwili wake umehifadhiwa katika chumba cha maiti cha Hospitali Teule ya Muheza.
BC inaungana na wapenzi wote wa sanaa nchini Tanzania kutoa pole za dhati kwa ndugu,jamaa na marafiki wa Sharo Milionea.Pumzika kwa Amani.
Mbunge wa Njombe wa muda mrefu na mwanasiasa wa siku nyingi nchini, Mzee Jackson Myangila Makweta,amefariki dunia jioni hii jijini Dar-es-salaam, kutokana na matatizo ya moyo ambayo yalikuwa yakimsumbua.
Mbali ya kuwa miongoni mwa wabunge walioongoza majimbo yao kwa muda mrefu zaidi katika historia ya Tanzania, Jackson Makweta pia aliwahi kushika nyadhifa mbalimbali katika serikalini ya Tanzania zikiwemo zile za uwaziri(wa wizara mbalimbali),
BC inapenda kuungana na watanzania wote katika kuomboleza msiba huu na kutoa pole nyingi kwa ndugu,jamaa na marafiki na hususani familia yake. Mwenyezi Mungu ailaze roho yake mahali pema peponi.Amen
Habari ambazo zimetambaa, zinasema kwamba mtanzania anayecheza katika ligi ya kikapu nchini Marekani,(NBA) Hasheem Thabeet, atajiunga na timu ya Oklahoma City Thunders kwa mkataba wa miaka miwili.
Kwa mujibu wa Oklahoman, Ingawa mkataba kamili haujawekwa wazi inasemekana kwamba Hasheem ataingia kwa mkataba wa kulipwa mshahara usiopungua $880,000 katika mwaka wa kwanza wa mkataba huo.
Oklahoma City Thunders au OKC kama wanavyofahamika miongoni mwa mashabiki wa mpira wa kikapu na ligi ya NBA, itakuwa ni timu ya nne kwa Hasheem Thabeet kuichezea tangu aliposaini na Memphis Grizzlies kufuatia kuwa wa pili katika NBA Draft mwaka 2009 mbele kwa nafasi moja kutoka kwa mchezaji mwingine anayechezea Thunder hivi sasa,James Harden.
Hata hivyo,Hasheem ameonekana kutokuwa na mwanzo mzuri sana ndani ya NBA tofauti na alipokuwa chuoni Connecticut ambapo aliwahi kuwa Defensive Player Of The Year. Katika michezo 135 ndani ya NBA, Hasheem ana kiwango cha point 2.2, rebound 2.7 na 0.9 blocked shots.
Kwa muda mrefu OKC walikuwa wakimtaka Hasheem na walisikitika mwaka 2009 alipochukuliwa na Memphis.
Ni mwanzo mwingine kwa Hasheem Thabeet na kwa jinsi OKC walivyo,basi huenda tukashuhudia msimu tofauti kabisa wa NBA na bila shaka msimu tofauti kwa Hasheem Thabeet.
Taarifa ambazo zimetufikia muda si mrefu uliopita zinapasha kwamba Mwanasiasa mkongwe nchini,mwanasheria na miongoni mwa waasisi wa Chama Cha Demokrasia na Maendeleo(CHADEMA), Bob Makani, amefariki jioni hii katika hospitali ya Aga Khan jijini Dar-es-salaam.Mwenyezi Mungu aipumzishe roho yake mahali pema peponi.
Tutaendelea kuwaleteeni habari zaidi kadiri tunavyozidi kuzipata.




sending...





















Rais Jakaya Kikwete, Makamu wa Rais Dkt.Mohamed Gharib Bilal na Mwenyekiti wa CHADEMA Freeman Mbowe wakibeba jeneza la marehemu Bob Makani
Rais Jakaya Mrisho Kikwete,makamu wa Rais Dkt.Mohamed Gharib Bilal pamoja na Mama Salma Kikwete leo waliungana na viongozi wa CHADEMA na viongozi wengine wa kitaifa kutoa heshima zao za mwisho kwa mmoja wa waasisi wa CHADEMA marehemu Bob Makani ambayepia aliwahi kushika nyadhifa mbalimbali serikalini ikiwemo ya Naibu Gavana wa Benki kuu katika viwanja vya Karimjee jijini Dar es Salaam.(picha zote na Freddy Maro)
Rais Jakaya Mrisho Kikwete akimpa pole Katibu Mkuu wa CHADEMA Dkt. Wilbroad Slaa katika viwanja vya Karimjee kufuatia msiba wa muasisi wa Chama hicho Bob Makani