Msanii mkongwe wa sanaa ya maigizo na filamu,Mzee Fundi Said almaarufu kama Mzee Kipara,hatunaye tena!

 

Habari za uhakika ambazo BC imezipata,zinapasha kwamba Mzee Kipara amefariki dunia majira ya saa tatu na nusu asubuhi ya leo nyumbani kwake maeneo ya Kigogo jijini Dar-es-salaam.

 

Msanii huyo maarufu ambaye alitamba tangu enzi za maigizo kupitia radio(Radio Tanzania) mpaka kwenye luninga(hususani ITV) akiwa na kundi la sanaa za uigizaji la Kaole,amekuwa akisumbuliwa na maradhi mbalimbali kwa muda sasa.Ilifikia mpaka wakati pakaitishwa harambee ya kujaribu kunusuru afya yake ambapo wasanii kadhaa walijitokeza katika kusaidia.

 

Kwa namna yoyote ile,hili ni pigo sio tu kwa familia yake bali kwa tasnia nzima ya filamu na uigizaji nchini Tanzania.Tunaungana na wote katika kuwatakia faraja ndugu,jamaa na marafiki wa Marehemu Mzee Kipara.Mwenyezi Mungu aiweke roho ya marehemu mahali pema peponi.Amin

 

Taarifa za uhakika ambazo BC imezipata zinapasha kwamba msanii maarufu wa muziki wa bongo fleva, Abel Motika almaarufu kama Mr.Ebbo amefariki dunia jana majira ya saa tatu usiku akiwa hospitalini jijini Arusha alipokuwa amelazwa.

Mr.Ebbo ambaye pamoja na kuwa msanii pia alikuwa producer na mmiliki wa Motika Records iliyopo jijini Tanga,atakumbukwa na wapenzi wengi wa muziki ndani na nje ya Tanzania kwani ni miongoni mwa wasanii wachache ambao waliweza sio tu kuipeperusha vyema bendera ya Tanzania kimataifa kupitia muziki bali kuimba kwake katika lafudhi ya kimasai kulimfanya kuwa wa kipekee sana(unique).Baadhi ya nyimbo zake zilizowahi kupendwa sana ni pamoja na ile ya Mi Mmasai ambaye tunaweza kabisa kusema ndio iliyomtoa Mr.Ebbo.Nyingine ni kama vile Mbando,Kamongo na Maneno Mbofu Mbofu kwa kuzitaja chache tu.

Bado mipango ya mazishi haijajulikana wazi ila habari zilizopo ni kwamba anatarajiwa kuzikwa huko kwao Arusha.Tutaendelea kuwapatia taarifa rasmi pindi tutakapoipata.Pumzika kwa amani Mr.Ebbo

Habari ambazo BC imezikamata muda mfupi uliopita zinapasha kwamba Waziri wa Maji na Umwagiliaji,Prof.Mark Mwandosya(pichani) amerejea jijini Dar-es-salaam kutoka nchini India alipokuwa amelazwa kwa matibabu.Prof.Mwandosya amerejea nchini kwa kutumia ndege ya Shirika la Ndege la Emirates.

Haikuweza kufahamika mara moja kama Prof.Mwandosya amepona kabisa na hivyo kurejea kazini mara moja au bado atakuwa akiendelea na matibabu taratibu.BC inamtakia kila la kheri katika kuendelea kuimarisha afya yake.

Mtangazaji wa siku nyingi nchini Tanzania  na mwasisi wa Shirika la Utangazaji la Tanganyika Broardcasting Cooparation (TBC) enzi hizo na Mkurugenzi wa kwanza mzawa wa Radio Tanzania Dar es salaam (RTD) Mzee David Wakati amefariki dunia alfajiri ya wa kuamkia leo jijini Dar-es-salaam katika hospitali ya Regency iliyopo maeneo ya Upanga,imefahamika.
Kwa mujibu wa taarifa ambazo BC imezipata na kuweza kuthibitisha kutoka kwa ndugu wa karibu wa Mzee Wakati,mtangazaji huyo mkongwe,amefariki kutokana na maradhi ya kiarusi ambayo amekuwa akisumbuliwa nayo tangu mwaka jana.Mungu aiweke roho ya marehemu David Wakati mahali pema peponi AMEN
Tutaendelea kuwapeni taarifa kuhusu msiba huu kadiri zitakavyokuwa  zinapatikana.

Marehemu David Wakati(wa kwanza kushoto) akiwa na waandishi na wanahabari wengine Ikulu jijini Dar-es-salaam walipokwenda kumuaga Mwalimu Julius Kambarage Nyerere alipotangaza kustaafu mwaka 1985.

UNITED REPUBLIC OF TANZANIA
DIRECTORATE OF PRESIDENTIAL COMMUNICATIONS
TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete leo, Jumanne, Novemba 29, 2011, ametia saini Muswada wa Sheria ya Mabadiliko ya Katiba ya Mwaka 2011.

Hatua hiyo ya Mheshimiwa Rais kutia saini Muswada huo inakamilisha safari ya kutungwa kwa Sheria ya Mabadiliko ya Katiba ya Mwaka 2011 baada ya Bunge kuwa limepitisha Muswada huo uliowasilishwa na Serikali katika kikao kilichopita cha Bunge.

Aidha, kutiwa saini kwa Muswada huo ili uwe Sheria ni hatua kubwa na muhimu katika safari ya kutungwa kwa Katiba mpya ya Tanzania kama ilivyoahidiwa na Mheshimiwa Rais Kikwete katika salamu zake za Mwaka Mpya kwa wananchi Desemba 31, mwaka jana, 2010.

Pamoja na kutiwa saini hiyo bado Serikali itaendelea kusikiliza maoni na mawazo ya wadau na wananchi mbalimbali kuhusu namna ya kuboresha sheria hiyo.

Hivyo, Mheshimiwa Rais Kikwete anatoa wito kwa mwananchi yoyote mwenye maoni ama mawazo ya namna ya kuboresha Sheria hiyo, ajisikie yuko huru kutoa maoni yake na Serikali itasilikiza na kuchukua hatua zipasazo.

Imetolewa na:

Kurugenzi ya Mawasiliano ya Rais,
Ikulu,
DAR ES SALAAM.

29 Novemba, 2011

Mkurugenzi Mkuu wa zamani wa Shirika la Ndege Tanzania(ATCL),David Mataka akitoka katika chumba cha Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu jijini Dar es Salaam leo ambapo alisomewa jumla ya mashitaka matatu likiwemo la kushindwa kutoa taarifa sahihi za matumizi ya vitu mbalimbali vya shirika hilo.

Bw.Mataka ameachiwa kwa Dhamana ya Sh. Mil.20 kutoka kwa wadhamini wawili tofauti ambao kila mmoja amemdhamini kwa sh.Mil. 10.

Mkurugenzi Mkuu wa zamani wa Shirika la Ndege Tanzania(ATCL),David Mataka akisindikizwa na askari Polisi wakati akitoka kwenye chumba cha Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu jijini Dar es Salaam leo alikosomewa mashtaka matatu likiwemo la kushindwa kutoa taarifa sahihi za matumizi ya vitu mbalimbali vya shirika hilo.

Picha na Francis Dande

Habari mbalimbali ambazo zinazidi kusambaa mtandaoni na pia katika vyombo mbalimbali vya habari vikiwemo vile vya kimataifa kama vile CNN, The Guardian UK,Reuters,AFP,Al Jazeera nk zinasema kwamba aliyekuwa Rais wa Libya,Moammar Ghadhafi, amefariki dunia baada ya kushambuliwa na kuumizwa vibaya katika mapambano makali yaliyotokea katika mji aliozaliwa wa Sirte kati ya waasi(National Transitional Council-NTC) na majeshi yake.

Kwa mujibu wa msemaji wa NTC,Abdel Majid Mlegta,Ghadhafi ambaye aliitawala Libya kwa miaka takribani 42, amefariki kutokana na kuumizwa vibaya kichwani wakati wa mashambulizi hayo na wakati akijaribu kukimbia.

Hizi hapa ni baadhi ya picha ambazo zinazidi kusambaa mtandaoni zinazoonyesha sura ya Moammar Ghadhafi baada ya mashambulizi.Tunaomba radhi kwa picha hizi!

Ghadhafi?

Bado tunaendelea kufuatilia kwa makini habari hizi ambazo zinaendelea kuthibitishwa na pande mbalimbali.Mkutano baina ya waandishi wa habari na kiongozi wa sasa wa Libya,unatarajiwa hivi punde.Stay tuned

UPDATE: Mwili wa Kanali Moammar Ghadhafi umewasili katika mji wa Misratah.Mtoto wa Ghadhafi ajulikanaye kama Mutasim ameuawa pia katika mashambulizi hayo.Alikuwa na baba yake.

UPDATE: Waziri Mkuu wa Libya,Jibril amethibitisha muda mfupi uliopita kwamba Moammar Ghadhafi amefariki au kuuawa na majeshi ya NTC.

Hapa chini tunayo screen shot kutoka Al Jazeera inayoonyesha mwili wa Ghadhafi.Picha hii imepatikana kutoka katika video ya kwenye simu.Bonyeza More kuitazama.Warning: Picha hizi sio nzuri kwa kila mtu.

read more

Tuzo ya Amani ya Nobel (Nobel Peace Prize) kwa mwaka huu imegawanywa kati ya wanawake watatu, Ellen Johnson Sirleaf na Leymah Gbowee wa Liberia na Tawakkul Karman wa Yemen, kamati ya Nobel katika mji mkuu wa Norway, Oslo, imetangaza muda mfupi uliopita.

Wanawake hao wameshinda tuzo hiyo kufuatia juhudi zao za kutafuta amani bila fujo na pia kutetea haki za wanawake na kuwachagisha katika kushiriki kikamilifu katika kazi mbalimbali za kuleta amani katika nchi zao na duniani kote.

Johnson Sirleaf, Rais wa Liberia mwenye umri wa miaka 72 , ni mwanamke wa kwanza barani Afrika kuchaguliwa mkuu wa nchi kidemokrasia. Ujasiri wake wa kisiasa na kutopenda masihara kumemfanya apachikwe jina la “Iron Lady”.

Ili kujua zaidi kuhusu Leymah Gbowee na Tawakkul Karman endelea kusoma zaidi kuhusu habari hii kwa kubonyeza hapa.

Chama Cha Mapinduzi(CCM) kupitia aliyekuwa mgombea wake,Dr.Dalali Kafumu(pichani) kimeibuka mshindi katika uchaguzi mdogo wa Jimbo la Igunga mkoani Tabora.Dr.Kafumu ameshinda kwa kupata jumla ya kura 26,488 huku kikifuatiwa kwa karibu na Chama Cha Demokrasia na Maendeleo(CHADEMA) kilichojipatia kura 23,260.

Nchi yetu Tanzania leo ipo katika msiba mkubwa kufuatia kuzama kwa meli ya LCT MV Spice Islanders visiwani Zanzibar ilipokuwa safarini kutoka Unguja kwenda Pemba alfajiri ya kuamkia leo.Watu wengi wamepoteza maisha yao na wengi wamejeruhiwa.Shughuli za uokoaji zinaendelea kwa ushirikiano mkubwa wa vyombo vyote vya usalama nchini kama vile Jeshi la Wananchi Tanzania na Jeshi la Polisi.Majeruhi wanaendelea kuokolewa na pia miili ya waliopoteza maisha inaendelea kuibuliwa toka majini.

BC inaungana na kila mtanzania,ndugu,jamaa na marafiki zetu popote pale walipo kuwapa pole wote waliopoteza ndugu,jamaa au marafiki na pia kuwatakia uponaji wa haraka wale wote waliojeruhiwa.Mwenyezi Mungu azilaze pema peponi roho za wote waliopoteza maisha.Amina

Read the Next Page →

↑ Go Back to Top of Page