MY TANZANIA   |   PLACES TO GO   |   MEDIA   |   ONLINE ENTERTAINMENT    

Mhadhiri mshiriki wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM) Profesa Jwani Timothy Mwaikusa, mpwawe na jirani yake wameuawa na majambazi usiku wa kuamkia leo nyumbani kwake maeneo ya Salasala jijini Dar-es-salaam.

Sambamba na mauaji ya Profesa Mwaikusa, majambazi hayo pia yaliua mtoto aliyekuwamo ndani ya nyumba ya Profesa huyo, Gwamaka Daudi na jirani John Mtui.

Polisi wamethibitisha kutokea kwa tukio hilo na kusema kuwa jirani huyo ambaye alikuwa na bastola aliuawa alipokuwa akienda kutoa msaada kwa Profesa huyo.

Jumuia ya wafanyakazi na wanafunzi wa UDSM walikumbwa na simanzi kuu leo baada ya kupokea taarifa hizo ingawa wanafunzi walikuwa wakiendelea na mitihani ya kumaliza mwaka.

Mkuu wa Kitivo cha Sheria(Faculty of Law) Chuoni hapo Profesa Palamagamba Kabudi, alisema kifo cha Profesa Mwaikusa siyo tuu pigo kwa chuo hicho bali tasnia nzima ya sheria na taifa kwa ujumla.

Kwa mujibu wa Profesa Kabudi, mpaka wakati kifo kinamkuta Profesa Mwaikusa alikuwa, Profesa Mshiriki katika idara ya Sheria za Umma (Public Law).

Alisema Profesa Mwaikusa alizaliwa Julai 21 mwaka 1952, na kuwa aliajiriwa kama mhadhiri msaidizi na chuo hicho mwaka 1986. Alisomea sekondari ya Mirambo, Tabora.

Career:

* Professor of Law, Faculty of Law, University of Dar es Salaam 1999
* Mkono & Co Advocates since 1998
* Advocate, High Court of Tanzania since 1988
* Managing Editor of the Tanzania Law Reports.

Qualifications:

* Ph.D., School of Oriental & African Studies, University of London, UK, 1995
* LL.M, University of Birmingham, UK, 1985
* LL.B (Hons), University of Dar es Salaam, Tanzania, 1981.


Chama cha Mapinduzi(CCM) leo kimemchagua rasmi Jakaya Mrisho Kikwete kuwa mgombea wake katika Uchaguzi Mkuu mwezi Octoba mwaka huu.

Baada ya mashauriano na Kamati Kuu ya Chama Cha Mapinduzi, Rais Kikwete amemteua Dr.Mohammed Gharib Bilal, kuwa mgombea mwenza.Kwa maana hiyo tiketi ya CCM itabebwa na Jakaya Mrisho Kikwete na Dr.Mohammed Gharib Bilal.

Dr.Gharib Bilal alizaliwa tarehe 6 Februari,1945 huko Unguja. Dr.Bilal ni mwanasayansi aliyepata stashahada ya kwanza katika sayansi ya nuklia kutoka Chuo Kikuu cha Howard nchini Marekani mwaka 1967. Alipata Masters Degree katika masuala hayo hayo ya sayansi ya nuklia kutoka Chuo Kikuu Cha California mwaka 1969 kabla ya kupata PhD katika fizikia kutoka chuo hicho hicho cha California mwaka 1976. Kuanzia mwaka 1976 mpaka mwaka 1990 alikuwa Lecturer(mkufunzi) katika Chuo Kikuu Cha Dar-es-salaam-Idara ya Fizikia

Kati ya mwaka 1990 na 1995 alikuwa Katibu Mkuu katika Wizara ya Sayansi,Tekinolojia na Elimu ya Juu katika serikali ya Muungano.Mwaka 1982 alikuwa Mkuu wa Kitivo Cha Sayansi,Chuo Kikuu cha Dar-es-salaam.

Baada ya Uchaguzi Mkuu wa mwaka 1995, aliteuliwa na Rais Salmin Amour kuwa Waziri Kiongozi wa Zanzibar. Mwaka 2000 aligombea Urais wa Zanzibar bila mafanikio. Mwaka huu alikuwemo miongoni mwa waliojitokeza kuomba ridhaa ya CCM kusimama kama mgombea Urais Zanzibar lakini bahati hiyo ikamuangukia Dr.Ali Mohammed Shein.Badala yake na kwa maana hii,atasimama na Kikwete kama mgombea mwenza na hivyo,endapo watashinda,atakuwa Makamu wa Rais wa serikali ya Muungano.

Photo/Francis Godwin

Bila shaka umezipata habari ambazo zimeshaenea sehemu mbalimbali ulimwenguni kuhusu kukamatwa na kisha kuachiwa kwa dhamana(kajiwekea mwenyewe mdhamana)Msanii mkongwe wa muziki wa Hip Hop nchini Tanzania, Joseph Mbilinyi aka Mr. II alias Sugu.

Kwa mujibu wa vyombo mbalimbali vya habari vikiwemo blogs ya Issa Michuzi na Da,Subi(wavuti dot com) sababu za kukamatwa kwake leo na maafisa wa jeshi la Polisi akiwa katika ofisi za Baraza la Sanaa la Taifa (BASATA) wakati wa kikao cha kuongelea masuala ya muziki, ni kufuatia mmoja wa viongozi wa kituo kimoja  cha redio ya jijini Dar Es Salaam kumshitaki kuwa anamtishia maisha kwenye wimbo mmoja ambapo Mr. II anasikika akisema “I wanna kill you”. Wimbo huo na nyinginezo zinapatikana katika albamu ya ‘Anti-Virus’ inayosambazwa bure mtaani.

Katika utetezi wake,Mr. II ambaye alitarajiwa kutangaza nia yake ya kuwania Ubunge mkoani Mbeya kwa tiketi ya CHADEMA,anasema jambo hilo limemshangaza kwa kuwa maneno yaliyotumika katika wimbo huo ni ya kisanii zaidi na yanaweza kuwa na maana zaidi ya moja.

Amedai alikamatwa na kuhojiwa na maofisa wa Polisi kutoka Makao Makuu ya jeshi hilo kwa saa kadhaa na kisha kuachiwa kwa dhamana ya kujidhamini mwenywe, na ametakiwa kuripoti kituoni hapo kesho kutwa.

Mr. II pamoja na wasanii wengine wamerekodi nyimbo kadhaa na kuweka kwenye albamu moja ambayo wameiita Anti-Virus, wakielezea hisia zao mbalimbali za kimaisha na kadhia la muziki wa Tanzania.

Je,hii na haki na sahihi(kwa Sugu kufikishwa katika mkono wa sheria)  au ni uonevu? Ni kweli kwamba inawezekana Sugu amekamatwa kutokana na juhudi zake mpya katika ulimwengu wa siasa ambapo hivi karibuni yeye na baadhi ya wasanii walitangaza rasmi kujiunga na Chama Cha Demokrasia na Maendeleo(CHADEMA)?

KIMDJ mkongwe na maarufu nchini Tanzania,DJ Young Kim, amefariki dunia. Kwa mujibu wa blog ya Issa Michuzi, DJ Kim amefariki dunia akiwa katika hospitali moja ya binafsi inayojishughulisha zaidi na tiba za magonjwa ya moyo iliyopo Manzese jijini Dar-es-salaam.

DJ Young Kim ni miongoni mwa DJs waliochangia sana maendeleo ya disco na mashindano ya kucheza muziki(disco) ambapo ndipo yalipoibuka majina maarufu katika muziki kama vile Black Moses(RIP),Ommy Sidney,Othman DigaDiga na wengine wengi.

Pia kwa wale ambao wanafuatilia chimbuko la muziki ambao leo hii tunauita wa kizazi kipya,mchango wa DJ Kim kupitia mashindano ya Yo Rap Bonanza ,ulikuwa ni chachu muhimu katika mwanzo au mwendelezo wa muziki wa hip hop nchini Tanzania.Pumzika kwa amani DJ Young Kim.

president

Rais wa Marekani Barack Hussein Obama ametangazwa kuwa mshindi wa Tuzo ya Amani ya Nobel kwa mwaka 2009. Hiyo ndio habari kubwa iliyopo kwenye vyombo vingi vya habari vikubwa ulimwenguni hivi leo.Hongera Obama.

Kwa undani zaidi wa habari hii unaweza kubonyeza hapa na hapa na hapa.

mpakanjia

Habari ambazo zimeingia punde na pia kupitia vyanzo mbalimbali vya habari vinapasha kwamba mfanyabiashara maarufu wa jijini Dar-es-salaam,Mohamed Mpankanjia maarufu kama Medi Mpakanjia, amefariki dunia hapo jana katika hospitali ya jeshi ya Lugalo jijini Dar-es-salaam.

Mohamed Mpakanjia alikuwa mume wa Marehemu Amina Chifupa,Mbunge kijana aliyefariki dunia miaka takribani miwili iliyopita katika mazingira ambayo yalikuwa ya kutatanisha.

Habari hii inaendelea na hivyo tutaendelea kukupasha kadri zinavyozidi kuingia.

zombeSheria ina kitu kinasema Every man is innocent until proven guilty. Pengine huo ndio ukweli kwani leo aliyekuwa Mkuu wa Upelelezi  wa Jeshi la Polisi mkoa wa Dar-es-salaam,Abdallah Zombe(pichani) pamoja na wenzake 9 wameonekana hawana hatia katika kesi ya mauaji iliyokuwa inawakabili.

Kwa maana hiyo, Zombe na wenzake leo ni watu huru.Wanarejea makwao kwa familia zao.

Kwa vyovyote vile, kesi hii na uamuzi huu wa Mahakama Kuu, umegusa au utagusa hisia za wengi. Ni wakati mzuri wa kutizama mienendo ya sheria zetu,mahakama zetu na pia ubinadamu wetu. Kwa upande wa kesi yenyewe, je tupo makini katika kukusanya vielelezo au ushahidi wa tukio lenyewe? Tupo namna gani katika suala zima la masuala ya Forensic Investigation? Je jina maarufu(kama la Zombe) linapoingia kwenye vitabu vya mahakama weledi(professionalism) unakuwa ule ule au kidogo panakuwa na mchecheto? Ni maswali ambayo lazima tuyapatie majibu.

Pia lipo swali ambalo Pius Mikongoti ameniuliza hapa muda mfupi uliopita, Unadhani sasa atarejeshwa kazini? Sina uhakika lakini kwa kuzingatia “haki na sheria”, ndio; anastahili.

michael-jackbc

Habari za uhakika ambazo BC imezipata zinapasha kwamba Mfalme wa muziki wa Pop,Michael Jackson,amefariki dunia huko Los Angeles nchini Marekani mchana huu.

Mfalme huyo wa Pop alikimbizwa hospitali mchana huu baada ya kuzimia akiwa nyumbani kwake maeneo ya Holmby Hills huko Los Angeles alizimia baada ya kupatwa na mshtuko wa moyo kitu ambacho kinasemekana ndicho kilichomaliza uhai wa Michael Jackson katika Kituo Cha Afya cha UCLA ilipotimia saa nane na dakika ishirini na sita (2:26pm) kwa saa za Los Angeles.

mj-jackson_1972b

Michael Jackson akiwa na umri wa miaka 13

Michael Jackson alizaliwa huko Gary,Indiana nchini Marekani tarehe 29 August mwaka 1958 akiwa ni mtoto wa saba kati ya watoto tisa wa Joseph na Katherine Jackson(wazazi wao). Alianza  kujishughulisha na masuala ya muziki akiwa na umri wa miaka minne(4) katika kundi la familia lililojulikana na kutamba kama Jackson 5(pichani).

jackson5

Kabla ya kufikwa na mauti,Michael Jackson, alikuwa anapanga kufanya show za mwisho huko London mwezi July mwaka huu.Tiketi kwa ajili ya show hizo zilikuwa zimeshakwisha(sold out)!

garyindianabc

Pichani ni nyumbani alipozaliwa Michael Jackson na ndugu zake huko Gary,Indiana nchini Marekani.Nilipiga picha hii December mwaka 2006 nilipotembelea maeneo hayo ili kujionea alipozaliwa Mfalme wa Pop.Mtaa ilipo nyumba hii unaitwa Jackson Street.

BC inapenda kutoa pole kwa wote ambao wameguswa kwa njia moja au nyingine na msiba huu.Tunaamini kwamba Michael Jackson alikuwa sio tu mwanamuziki maarufu ulimwenguni bali muziki wake uligusa wengi.Wengi walicheza,wanacheza na wataendelea kucheza miziki yake.

Hapa chini unaweza kusikiliza simu iliyopigwa kutoka nyumbani ikwake kwenda kwa watu wa huduma za dharura(Emergency)

Audio clip: Adobe Flash Player (version 9 or above) is required to play this audio clip. Download the latest version here. You also need to have JavaScript enabled in your browser.

 

chengebc1Mbunge wa Bariadi Mashariki,Andrew Chenge “Mzee wa Vijisenti” yupo matatani…tena.Safari hii ni kwa kupata ajali ya barabarani(kugonga) na kusababisha vifo vya watu wawili ambao walikuwa ndani ya usafiri maarufu kama “Bajaji”.Waliofariki inasemekana ni wanawake wawili ambao ndio walikuwa abiria katika Bajaj hiyo.Dereva wa Bajaj hajulikani alipo.

Tukio hilo limetokea alfajiri ya leo katika maeneo ya Oysterbay(karibu na nyumbani kwake).Kwa mujibu wa taarifa ya Kamanda wa Kanda Maalumu ya Polisi Dar-es-salaam, Afande Kova, Chenge alikuwa akiendesha gari aina ya Pick Up-Hilux yenye namba ya usajili T512 ACE.Bajaj iliyohusika kwenye ajali ina namba za usajili T736 AXE na imeorodheshwa kama mali ya Zuwena Feith Nassoro wa SLP 2595 Dar-es-salaam.

Baada ya tukio hilo,Mheshimiwa Chenge alijisalimisha katika kituo cha Polisi Oysterbay na anaendelea kuisaidia polisi.Habari hii bado inaendelea…

mwinyibc

Rais mstaafu,Ally Hassan Mwinyi,leo alikumbwa na jambo ambalo hakuna aliyelitegemea.Mwinyi alikuwa akihutubia wakati wa sherehe za Maulidi zilizofanyikia Diamond Jubilee.Punde si punde akatokea jamaa na kumchapa kibao.Kwa mujibu wa watu walioshuhudia kitendo hicho,kibao kilikuwa cha kushtukiza kwani kila mtu alidhani kijana huyo alikuwa anakwenda kumsalimia Kaimu Mufti Sheikh Suleyman Gorogosi aliyekuwa pembeni ya Mzee Mwinyi.Wengine walidhani kijana ni fundi mitambo na hivyo alikuwa anakwenda kurekebisha kipaza sauti.Tofauti na mawazo ya wengi,kijana huyo aligeuza mkono ghafla na kumnasa kibao Mzee Mwinyi.Kijana huyo ambaye ametambulika kwa jina la Ibrahim Said ana umri wa miaka 26.

Kabla ya kitendo hicho,Mzee Mwinyi,kama ambavyo amekuwa akifanya mara kwa mara,alikuwa akiwaasa waliohudhuria baraza hilo la Maulid kuepukana na ngono zembe kitu ambacho kinachangia sana kuenea kwa ugonjwa wa ukimwi.

mwinyi2

Baada ya hapo jamaa alitolewa nje na walinzi wa Mzee Mwinyi wakisaidiana na waumini huku akipewa kichapo cha nguvu kama inavyoonekana pichani. Baada ya kutolewa nje kijana huyo,Mzee Mwinyi alisimama na kuwahakikishia waliokuwepo kwamba yupo fiti na shughuli inaweza kuendelea!

Pamoja na hayo maswali kadhaa yameshazuka kuhusu jamaa wa usalama.Walikuwa wapi?Na je nini kilipelekea kijana huyo kufanya alichokifanya? Ni maneno yaliyokuwemo kwenye hotuba ya Mzee Mwinyi? Je kijana ana matatizo ya akili? Pole sana Mzee Mwinyi.

Picha kwa hisani ya Dr.Faustine.

Read the Next Page →

↑ Go Back to Top of Page