
Zipo habari kuhusu celebrities wetu ambazo huwa nikizisikia kinachonijia kwanza ni masikitiko.Huwa nasikitika ninapoona kwamba watu fulani ambao ni role-models kwa vijana wetu,wanakuwa wanafanya mambo ambayo sio tu yanawavunjia heshima wao wenyewe,bali pia yanaporomosha maadili ya kiungwana na kiutu.
Bila shaka mpaka hivi sasa umeshasikia habari za mcheza kikapu Hasheem Thabeet kumpiga au kupigana na mwanamuziki nyota TID wikiendi iliyopita pale Club Bilicanas jijini Dar. Baada ya vita ya mikono na mateke,vita sasa imebakia kuwa ya maneno.
Kila mmoja, Hasheem na mwenzie TID amekuwa akitoa maelezo tofauti tofauti kuhusu kilichojiri pale Bilicanas.Kwa mujibu wa Gazeti la Amani(la Global Publisherz), Hasheem anasema alichokozwa kupita kiasi na TID. Na TID anasema,kupitia blog yake,kwamba hajui kwanini Hasheem aliamua kumtenda alivyomtenda.TID haweki wazi sana kilichotokea.Anachosema yeye ni kama vile Hasheem aliamua tu kumfanyia “ubabe” na kumdunda.
Katika vita ya maneno,wakati mwingine ni vigumu kupata ukweli.Ukweli halisi wanao Hasheem na TID. Cha msingi kilichopo mbele ni kwamba kwa kuonyeshana ubabe au ego zenu mbele ya kadamnasi,nyote mmekosea. Kama ulichokozwa Hasheem you could have handled it differently. Verbal violence doesn’t have to end with physical violence. Na TID,kama maelezo aliyoyatoa Hasheem katika gazeti la Amani ni ya kweli,tabia ya kupenda kununua ugomvi,haikujengi bali inakubomoa na kukushushia heshima.
Hasheem maliza likizo yako urudi Marekani kuendeleza mchezo wako.You are a role model to many youngsters.Be one.TID zingatia kazi yako muhimu ya kuburudisha,kuelimisha na kuonya jamii kupitia muziki wako.Pamoja.

Kwa faida ya msomaji ambaye, kwa sababu moja au nyingine hawezi kuwatambua waliopo pichani; Kutoka kushoto ni Kenneth Kaunda,maarufu kama KK(Rais wa Zambia kuanzia mwaka 1964 mpaka 1991),Julius Kambarage Nyerere(Baba wa Taifa la Tanzania na Rais wake kuanzia mwaka 1964 mpaka 1985),Jomo Kenyatta(Rais wa Kenya kuanzia mwaka 1964 mpaka 1978.),Milton Obotte (Rais wa Uganda kuanzia mwaka 1966 mpaka 1971 na kisha mwaka 1980 mpaka 1985)
Je,wewe binafsi unajifunza au umejifunza nini katika kufuatilia jinsi walivyoendesha maisha yao,utumishi wao kwa umma nk? Unadhani kuna yepi ya msingi ambayo sisi kama wananchi na pia viongozi wetu wa hivi sasa tunaweza kujifunza kutoka kwa watu hao?Kumbuka mazuri na mabaya yao kwani kama tulivyo sote,they were not perfect,no one is!
Naweza kusema nimeshazoea kuhoji wenzangu.Kuhoji watu ambao ndio chachu hasa ya BC bila kusahau msomaji ambaye ni wewe.Kumbe wakati nawawinda watu wa kufanya nao mahojiano,wapo wenzangu(wenzangu katika habari na mawasiliano) ambao pia huniangazia macho ili kufanya nami mahojiano.
Naomba nikiri kwamba hiyo hutokea mara chache.Naweza kukumbuka vizuri kabisa idadi ya mahojiano rasmi ambayo nimeshawahi kuyafanya.Sio kwamba sioni thamani ya mahojiano,la!Ni kwamba hupendelea tu kuwa upande mwingine wa kamera.Usinihoji sana kwanini kwa sababu sidhani kama nina jibu moja.Tutakesha.
Hivi karibuni Freddy Macha alifanya nami mahojiano ambayo yalichapishwa kwenye gazeti la Mwananchi mwishoni mwa wiki iliyopita. Kwa bahati nzuri nilishawahi kufanya mahojiano na Freddy Macha kuhusu kazi zake za uandishi,muziki na historia nzima ya maisha yake.Unaweza kusoma mahojiano yangu kwenda kwake kwa kubonyeza hapa na hapa.Kwa hiyo haikuwa kazi nzito sana aliponieleza nia yake ya kufanya nami mahojiano.Freddy ni mtu mcheshi,muungwana na mvumilivu.
Ni mahojiano mafupi lakini muhimu kiasi kwani unaweza kujua kile ninachokiwaza ninapokuwa nawaza na pia ninachofikiri kuhusu suala zima la blogs na maendeleo ya ulimwengu wa habari na mawasiliano ambapo siku hizi wewe msomaji na mchangiaji ndiye mshika tochi wa habari.Unaweza kuyasoma mahojiano hayo kwa kubonyeza hapa.

Hivi majuzi,Mzee wetu, Rashid Mfaume Kawawa, alizindua kitabu kinachoelezea maisha yake.Kitabu hicho ambacho kimeandikwa chini ya usimamizi wa Mkuu wa Chuo Cha Mwalimu Nyerere Cha Kivukoni,Prof.John Magoti,kimepewa jina la Kawawa.Uzinduzi huo ulifanyikia Ikulu jijini Dar-es-salaam.
Ingawa tunaweza kusema imemchukua muda mrefu sana Mzee Kawawa kuandika kitabu chake,ni lazima tumpongeze sana kwa uamuzi wake huo ambao sio tu wa busara bali pia ni mfano wa kuigwa.
Tulipofanya mahojiano na Mheshimiwa Zitto Kabwe mwaka juzi,tuliliongelea suala la kuandika vitabu na kujisomea.Mh.Kabwe alionekana kukerwa na tabia ya viongozi wetu(na hata sisi wananchi wa kawaida) kutopenda kusoma achilia mbali kuandika! Ni utamaduni ambao tupende tusipende hatuna budi kuiga.
Uandishi ukisindikizwa na usomaji ni msingi mzuri wa maendeleo.Wenzetu katika nchi zilizoendelea ni mabingwa wa kujisomea.Miji ya wenzetu imezungukwa na maktaba. Ukiingia kwenye ndege,treni au basi sio ajabu kukuta watu kadhaa wakijisomea vitabu,magazeti nk.Kwanini wanapenda kusoma?Jibu ni rahisi;wanapenda kuongeza ujuzi,kujielimisha na hivyo kuendelea kuwa mbele katika suala zima la maendeleo.
Miongoni mwa watu mashuhuri waliohudhuria uzinduzi wa kitabu cha Kawawa ni pamoja na maraisi wastaafu Ally Hassan Mwinyi na Benjamin William Mkapa. Swali ambalo lilibakia kichwani kwangu ni kwamba viko wapi vitabu vyao? Ni lini tutasoma kitabu cha Mwinyi,Mkapa,Warioba au hata Edward Lowassa na wengineo?
Ni matumaini yetu kwamba Kawawa amefungua tu njia na kwamba wengine watafuata.Hongera sana Mzee Kawawa.
Pichani ni Mzee Kawawa na Rais Kikwete wakati wa uzinduzi wa kitabu hicho.Kwa nyuma unaweza kumuona Rais Mstaafu B.W.Mkapa.Picha kwa hisani ya Ikulu.

Hatimaye siku 365 za mwaka 2008 zimefikia ukingoni.Ninavyoandika ujumbe huu tayari kuna sehemu mbalimbali za dunia ambapo tayari sekunde za mwisho za mwaka huu zimeshahesabiwa na tayari takwimu mpya zimeshaandikwa.Kwa maana hiyo leo ni mwaka mpya. Kwa heri mwaka 2008 karibu mwaka 2009.Kwa wengi leo huwa ni siku nzuri kwa maazimio mapya ndani ya matumaini mapya.Kwa jinsi hali ya uchumi duniani ilivyoishia mwaka tunaoupa kisogo,basi sio ajabu kwamba malengo ya wengi ni kulinda zaidi mifuko yetu kwa kuwa makini zaidi na matumizi hesabu za mapato na matumizi na pia kulinda zaidi kazi zinazotuingizia kipato.Nakutakia kila la kheri katika hilo.
Bila kujali hali ya kiafya,kiuchumi,kisiasa wala kijamii, ukweli kwamba mwaka mpya umewadia huku wewe na sisi sote hapa BC tukiwa hai, ni jambo la kufurahia na kumshukuru Muumba.Ukivuka mwaka unakuwa umeandika historia mpya katika maisha yako. Vitabu vya kumbukumbu vitaandika kwamba uliuona mwaka 2009! Ni jambo la kumshukuru muumba kwani ni wazi wapo wengi sana waliotamani kuuona mwaka huu na wasifanikiwe.Kama huamini, fikiria kidogo tu ni watu wangapi ambao umehudhuria mazishi yao au kusikia habari juu ya misiba yao?Unaona? Hatuna budi kumshukuru Mungu.
Wakati huu tunapoingia mwaka mpya wa 2009,tungependa kwanza kukutakia kila la kheri wewe msomaji,mtembeleaji au mchangiaji wetu.Mwenyezi Mungu akuongoze na kukubariki katika kila jambo utakalolifanya ndani ya mwaka huu wa 2009.Kama mwaka 2008 haukuwa wenye mafanikio kwako au haukutimiza malengo yako,usikate tama.Fungua ukurasa mpya huku ukiwa na fikra chanya zaidi na utaona mabadiliko.
Tungependa pia kukupa shukrani zetu za pekee kwa kuwa mtembeleaji,msomaji au mchangiaji mzuri wa BC.Kama kuna mafanikio yoyote ambayo tumeyapata tangu kuanzishwa kwa blog/site hii,ni wazi kabisa kwamba mafanikio hayo yametokana na mchango wako wewe msomaji,mtembeleaji na mchangiaji wetu.
Shukrani nyingi ziwaendee celebrities mbalimbali ambao bila maringo,kinyongo wala ngendembwe walikubali aidha kufanya nasi mahojiano au kutokuwa na kinyongo nasi pale tulipoweka picha zao na kukaribisha mvua ya maoni kutoka kwa wasomaji huku wengine wakiwa chanya na wengine hasi.Celebrities kama hao wanakuwa wametambua vyema nafasi au mchango wao katika jamii.Wametambua pia kwamba haiwezekani kuwa bondia ulingoni halafu ukawa unaogopa ngumi za uso.Tunawashukuru na kuwaomba tuendelee kushirikiana.
Shukrani za pekee ziwafikie bloggers wenzetu mbalimbali,vyombo mbalimbali vya habari ndani na nje ya Tanzania,wapiga picha mbalimbali na wengineo wote ambao wanaendelea kushirikiana nasi katika jukumu hili zito la habari na mawasiliano.Asanteni sana.Bila ninyi,haiwezekani.BC inathamini sana mchango wenu.
Kama binadamu inawezekana kabisa kuna wakati tunatokea kutoelewana au hata kukwazana.Bila shaka hata sisi hapa BC inawezekana kuna wakati tulikukwaza.Yawezekana hatukuweka maoni yako kwa sababu moja au nyingine,yawezekana tulichelewa kuruhusu maoni yako yaonekane,yawezekana wewe ni celebrity na tuliruhusu maoni ambayo kimsingi uliona kama umetusiwa nk.Mifano ipo mingi.Lakini kwa wote hao,tunaomba samahani.Yote hayo ni katika kujitahidi kuitenda vyema kazi yetu.
Tunapouanza mwaka mpya wa 2009,tunakusihi uendele kututembelea,kuchangia,kutukosoa tunapokosea na pia kumwambia mwenzako kuhusu uwanja huu ili naye asipitwe na yanayojiri.Tunakutakia kila la kheri.HAPPY NEW YEAR 2009.
Historia ya muziki wa kizazi kipya au Bongo Flava kama unavyojulikana miongoni mwa wengi hivi leo una historia ndefu. Ni historia ndefu kiasi kwamba hivi leo wengi hatukumbuki tena hata muziki huu ambao hivi leo umetokea kuwa kipenzi cha wengi ulianzaje,ukapitia hatua na harakati gani mpaka kufikia hapa ulipo hivi leo.
Miongoni mwa mashuhuda wa mwanzo wa harakati za mwanzo kabisa za muziki wa bongo flava ni aliyewahi kuwa DJ maarufu nchini Tanzania kwa jina Mike Pesambili Mhagama(pichani).Mike sio tu miongoni mwa mashuhuda wa mwanzo bali pia ni miongoni mwa watu wachache walioamini katika muziki wa kizazi kipya tokea mwanzo.Kumbuka hizo ni zile enzi ambapo muziki huo ulikuwa ukichukuliwa kama “uhuni” tu na sio aina mpya ya muziki au burudani.Ni watu wachache sana walioweza kutabiri hatua ambazo muziki huo ungepiga miaka kumi au kumi na tano baadaye.
Lakini pia Mike amekuwa akikerwa na jinsi ambavyo kumekuwepo na upotoshwaji au upindishwaji wa vipengele fulani fulani muhimu vya historia ya muziki huo. Katika kujaribu kuiweka vyema historia hiyo,Mike Mhagama ameandika kwa mapana na utulivu wa kina kuhusu harakati za mwanzo za muziki wa kizazi kipya,suluba walizopitia yeye na watangazaji wenzake katika kuutambulisha muziki huo,wadau mbalimbali anaowakumbuka katika harakati hizo,wanamuziki wenyewe,promoters wa muziki nk.
Pia Mike Mhagama,anaweka wazi kitu ambacho watu wengi wamekuwa wakijiuliza;Nini chanzo cha neno Bongo Flava? Nani mwanzilishi wake?Kwa jibu hilo na historia nzima,kwa jinsi anavyoikumbuka Mhagama, msome kuanzia hapo chini,kwa maneno yake mwenyewe, kama tulivyoyanakili kutoka katika blog yake(kwa ruhusa na baraka maalumu).Habari imegawanyika katika sehemu nne ili iwe rahisi kwako kuzisoma na kuelewa vyema anachokizungumzia Mike Mhagama. Mwenyewe anasema yawezekana kabisa asiwe sahihi kwa asilimia zote na ndio maana anapenda kukaribisha hoja,maoni na masahihisho yoyote kutoka kwako msomaji.Mike Mhagama hivi sasa anaishi huko Los Angeles,California nchini Marekani.
CHIMBUKO LA MUZIKI WA KIZAZI KIPYA TANZANIA NA MAANA HALISI YA NENO BONGO FLAVA.
Na Mike Mhagama-Los Angeles,Marekani.
SEHEMU YA KWANZA
Moja kati ya mambo niyapendayo mno maishani ni muziki.Nimekuwa mfuatiliaji mzuri sana wa muziki si tu ule wa nje lakini kwa karibu ule wa nyumbani hasa muziki wa dansi na ule wenye umaarufu sana hivi sasa ujulikanao kama Bongo Flava (Muziki wa Kizazi Kipya).Katika mapenzi hayo imekuwa kama bahati kuwa mmoja wa vijana wengi tuliobahatika kuuona muziki huu wa kizazi kipya ukizaliwa na pengine bahati zaidi bila kusita kusema;kuwa mmoja kati ya wale tulioanzisha kusukuma gurudumu la muziki huu kufikia hapa ulipo na nafasi yake kutambulika si tu Afrika Mashariki bali pia kwa sasa duniani kwa ujumla.
Kama ilivyo kwa aina zingine za muziki Tanzania,mfano muziki wa dansi basi utakuwa mkosefu wa fadhila bila kujumuisha majina kama Patrick Balisidya,Mbaraka Mwaruka Mwinshehe,Salum Abdalah na hata Remmy Ongara.Hawa ni vinara na walifanya kila wawezalo kuja na ubunifu si tu kuvutia wateja wao bali kuutangaza muziki wao ndani na nje ya nchi na kuipa Tanzania kitambulisho chake kwenye jukwaa la sanaa ya muziki.Kazi za wanamuziki hawa zilifana sana kwa ushirikiano mkubwa na chombo ambacho kwa Tanzania ni muhimu sana katika kueneza au kutambulisha kitu kipya,RADIO.Watangazaji kama Mzee Ibrahim Chimgege,Enock Ngombale,Timothy Pata,Abisai Stephen,Seif Salum Nkamba na Julius Nyaisangah chini ya ma-bwana mitambo mahiri kama akina James Mhilu na Crispin Lugongo wanastahili pongezi kwa kiasi kikubwa katika kurekodi na kusimamia mitambo wakati wanamuziki hawa wakitafuta majina na namna ya kujitambulisha kwa jamii itakayosikiliza muziki wao.Bahati mbaya huwasikii sana watu hawa katika zinazoitwa historia kwa sababu wengi ni rahisi kuwasahau lakini mchango wao ni mkubwa sana na unastahili heshima hasa unapoandika au kuizungumzia historia ya muziki wa dansi Tanzania. (more…)

Binti aliye pichani hapo juu anaitwa Megan Fox.Kwa mapana na marefu sio bongo celebrity.Yawezekana kabisa kwamba hata Bongo hajawahi kuisikia!
Kwanini basi tumemuweka hapa leo? Sababu ni kwamba binti huyu ndiye ambaye kwa mwaka huu wa 2008, jarida maarufu la FMH, lilimtaja kama mwanamke nambari wani mwenye mvuto zaidi miongoni mwa wanawake 100 iliyowaorodhesha kama wanawake wenye mvuto zaidi duniani.
Kwa bahati nzuri au mbaya,vyombo vya habari kama hivi vikishirikiana na vitu kama filamu,muziki nk ndivyo ambavyo hivi leo vina ushawishi mkubwa kuhusiana na suala zima la uzuri,urembo au mvuto.Vikisema fulani ndio mwenye mvuto zaidi basi mabilioni ya watu wanaamini hivyo.Matokeo yake ndio watu wengi(hususani wanawake) huanza safari ndefu ya kujinyima chakula ili wapunguze saizi za miili yao na kufanana na huyo aonekanaye “mzuri” kwa mujibu wa jarida fulani.Wengine hufanya kila wawezalo ili wawe na nywele,rangi ya mwili,kucha nk kama za huyo aonekanaye “mzuri” nk.Kwa bahati mbaya hata mengi ya majarida yaliyopo au yanayoanzishwa nchini Tanzania,yanafuata mkondo huo huo wa “kutafsiri” urembo,uzuri na mvuto.
Je urembo,uzuri,mvuto ni vitu gani?Ni kweli kwamba uzuri au urembo uko katika mboni ya jicho la mtazamaji au kutoka katika akili na macho ya mhariri wa jarida?Nini kifanyike ili kumfanya kila mtu aridhike na jinsi alivyo ili kupunguza mahangaiko,watu kupoteza maisha wakati wa zoezi la kujikondesha nk?

Katika anga za siasa duniani hivi leo,lipo jina ambalo dunia nzima inaendelea kulizungumzia.Hilo si lingine bali lile la Rais wa Zimbabwe, Robert Gabriel Mugabe.Kwa wengine mtu huyu ni shujaa,kwa wengine mtu huyu ni kinyume kabisa cha neno shujaa.Kwako wewe je?Je viongozi wa Afrika wanaohudhuria kikao cha Umoja wa Afrika huko Misri(na Mugabe naye anahudhuria) wataweza kumnyoshea vidole Mugabe?Nini hatma ya siasa za Afrika?
Pichani ni Rais Mugabe akiwa na mkewe,Grace Mugabe.Wengi wanasema wakati wao wanatafuna keki,wananchi wengi wa Zimbabwe wanakufa njaa.
Photo/New York Times


Leo ni mwaka mpya. Baada ya siku zaidi ya 365, mwaka 2007 umekatika.Leo tunaukaribisha rasmi mwaka 2008! Duniani kote shamrashamra za kuukaribisha mwaka mpya zimepamba moto. Ni muda wa maazimio mapya,matumaini mapya,misukosuko mipya na kwa vyovyote vile;tarakimu na takwimu mpya.
Bila kujali hali ya kiafya,kiuchumi,kisiasa wala kijamii, ukweli kwamba mwaka mpya umewadia huku wewe na sisi sote hapa BC tukiwa hai, ni jambo la kufurahia na kumshukuru Muumba.Ukivuka mwaka unakuwa umeandika historia mpya katika maisha yako. Vitabu vya kumbukumbu vitaandika kwamba uliuona mwaka 2008! Ni jambo la kumshukuru muumba kwani ni wazi wapo wengi sana waliotamani kuuona mwaka huu na wasifanikiwe.Kama huamini, fikiria kidogo tu ni watu wangapi ambao umehudhuria mazishi yao au kusikia habari juu ya misiba yao?Unaona? Hatuna budi kumshukuru Mungu.
Wakati huu tunapoingia mwaka mpya wa 2008,tungependa kwanza kukutakia kila la kheri wewe msomaji,mtembeleaji au mchangiaji wetu.Mwenyezi Mungu akuongoze na kukubariki katika kila jambo utakalolifanya ndani ya mwaka huu wa 2008.Kama mwaka 2007 haukuwa wenye mafanikio kwako,usikate tama.Fungua ukurasa mpya huku ukiwa na fikra chanya zaidi na utaona mabadiliko.
Tungependa pia kukupa shukrani zetu za pekee kwa kuwa mtembeleaji,msomaji au mchangiaji mzuri wa BC.Kama kuna mafanikio yoyote ambayo tumeyapata tangu kuanzishwa kwa blog/site hii,ni wazi kabisa kwamba mafanikio hayo yametokana na mchango wako wewe msomaji,mtembeleaji na mchangiaji wetu.
Maoni yako,michango yako,mapendekezo yako, mwitiko(feedback) wako nk. ndio mambo ambayo yanatufanya tuendelee kujitahidi kukidhi haja yako ya kupata habari mbalimbali,kujua kwa undani kidogo juu ya maisha na mienendo ya celebrities wetu nchini Tanzania na kila inapobidi, celebrities wengine barani Afrika na hata ulimwenguni kote. Tunaendelea kuamini kwamba habari na mienendo ya watu maarufu/mashuhuri katika jamii yeyote,ni vitu vyenye ushawishi fulani(kama sio mkubwa) kwa jamii husika.Hii ni pamoja na Tanzania yetu. (more…)

