Katikati ya mwaka jana,mwanamuziki Kelly Rowland kutoka nchini Marekani alikuwa na ziara ndefu ya barani Africa kwa hisani ya MTV kwa ajili ya kutembelea na kujionea harakati mbalimbali za kupambana na ugonjwa wa ukimwi.Alipitia sehemu nyingi ikiwemo Tanzania.Alifika mpaka “Uwanja wa Fisi”.Hii hapa ni Diary yake kuhusiana na safari hiyo.
Diary of Kelly Rowland from mtv staying alive on Vimeo.
Tafadhali naomba usinichoke kwa kupenda kutundika masuala/hotuba za Obama.Nafanya hivyo kwa kuamini kwamba kila siku binadamu tunajifunza au tunatakiwa tujifunze mambo mapya.Hotuba za Obama zawezekana kuwa hazikufunzi mambo mapya ila kwa mapana na marefu naaamini zinatukumbusha mambo mbalimbali.Pia namfuatilia Obama kwa sababu angalau yeye ndio mwanasiasa ambaye namuona hapendi “kuongopa waziwazi”.Obama hawezi kukuambia kesho atakujengea daraja wakati moyoni mwake anajua kabisa hela za daraja alishakula. Hawezi pia kutoa ahadi za maisha bora kwa wote bila kukumbusha kwamba kazi ndio msingi wa maendeleo.
Obama anaweza kuwa anaongea na kundi fulani tu la watu lakini akawa anatoa ujumbe mkali kwa jamii mbalimbali.Cha msingi labda ni kusikiliza kwa makini na kufanya tathmini makini. Hivi majuzi Obama alialikwa na kutoa hotuba wakati wa kusherekea miaka 100 ya chombo muhimu cha Wamarekani Weusi kinachoitwa NAACP(National Association for the Advancement of Colored People)
Katika hotuba yake,Obama aliongelea mengi.Muhimu zaidi ambalo naamini hata sisi watanzania tunaweza kujihusisha nalo ni suala la elimu kwa watoto wetu,jamii zetu. Ulimwengu wa leo,wa ushindani wa namna hii,unahitaji elimu makini.Je tunafanyaje katika hilo? Viongozi wetu wanatupeleka wapi? Hebu tujiulize, tangu marais wetu waliofuatia baada ya J.K.Nyerere wametusaidia kujenga maktaba ngapi? Hivi unajua jiji la Dar-es-salaam lina maktaba ngapi?

Umewahi kusoma makala zake,vitabu vyake na pia kusikiliza muziki wake.Jina lake sio geni.Nimeshawahi kufanya naye mahojiano. Anaitwa Freddy Macha,mtanzania mwandishi,mwanamuziki mwenye makazi jijini London nchini Uingereza.
Mwezi wa Mei mwaka huu,Freddy aliitikia wito wa kurudi nyumbani Tanzania na kugawana na wengine ujuzi mbalimbali alionao katika masuala ya uandishi,fasihi, muziki, maisha ya ughaibuni, mazoezi,afya na chakula bora. Alifanya hivyo kupitia semina mbalimbali alizoziendesha pale British Council,Soma Cafe(Mikocheni), Shule ya Sekondari Mwandege na Nyumba ya Sanaa.
Semina alizozifanya Macha ziliandaliwa na Jarida jipya la Lucky-Ideas For Living.Freddy anatarajiwa kurudi tena Tanzania mwezi Septemba mwaka huu ili kuendesha semina zingine.Usikose

Freddy Macha akiongelea uandishi wa vitabu na makala.Hapa ilikuwa Nyumba ya Sanaa jijini Dar-es-salaam.

Freddy akimuelekeza mmoja miongoni mwa waliohudhuria semina jinsi ya kufanya mazoezi ya tumbo.

Ni wazi kwamba tukiuliza swali kwamba kwanini Tanzania bado ni nchi ambayo,pamoja na rasilimali zote ilizonazo,bado haijaweza kupata maendeleo ya kiuchumi inayostahili,majibu yatakuwa ni mengi na pengine yanayotofautiana sana.Pamoja na tofauti ambazo zinaweza kujitokeza tunapojadiliana, mijadala ya namna hiyo ni muhimu kufanyika kwani inatupa mwanga wa nini pengine kifanyike ili tusije warithisha wanetu nchi ambayo hata wakitaka kuiuza,wasipate mnunuzi.
Miongoni mwa watu ambao wanatarajiwa kuchochea mijadala kama hiyo ni pamoja na wasomi mbalimbali tulionao.Haishangazi basi kusikia kwamba leo Prof.Issa Shivji(pichani) anatarajiwa kuzindua kitabu kinachoainisha mambo mbalimbali yanayosababisha nchi yetu kutopata maendeleo makubwa ya kiuchumi tangu tupate uhuru miaka arobaini na ushee iliyopita.Kwa habari zaidi bonyeza hapa.

Hakuna ubishi kwamba kijana Hamis Mwinjuma au maarufu kama MwanaFalsafa(MwanaFA) ni miongoni mwa wanamuziki wa muziki wa kizazi kipya ambao wamefanikiwa.MwanaFA amefanikiwa sio tu kufikisha ujumbe alioukusudia kwa jamii bali pia kuwa na uwezo wa kuendesha maisha yake kupitia muziki.Miziki yake imekuwa ikiimbwa na watu wa rika mbalimbali.Hayo nayo ni mafanikio.
Pamoja na mafanikio ya kimuziki au kisanii aliyonayo MwanaFA,anabakia kuwa mfano wa kuigwa linapokuja suala zima la elimu,muziki na maisha.Hivi karibuni alithibitisha hilo pale alipoamua kurejea tena shule.Safari hii ameelekea nchini Uingereza.
Nini kinamsukuma kijana huyu katika nyanja ya elimu? Na je hivi karibuni alipoachia wimbo unaokwenda kwa jina “Msiache Kuongea” alikuwa anamjibu Inspekta Haruni?Anazungumziaje maisha ya nchini Uingereza?Fuatana nasi katika mahojiano haya mafupi na MwanaFA
BC: Pamoja na mafanikio mazuri katika muziki kule Bongo bado umeamua kurudi tena shule.Nini kinakusukuma?Hapo UK umeenda kusomea nini na katika chuo gani?
FA: Kuna mengi yanafanya nifanye nnachofanya.Lakini kubwa na la msingi zaidi ni kuwa na nguzo nyingine kwa ajili ya maisha ninayoishi(Plan B).Kama unavyojua muziki pamoja na kuwa unakwenda vizuri lakini hautabiriki sana.Ni ngumu kujihakikishia nafasi ya moja kwa moja kwa angalau miaka 10 ijayo.

Pichani ni Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi,Profesa Jumanne Maghembe.Huyu ni miongoni mwa mawaziri ambao wizara zao zimekuwa zikikumbwa na vimbwanga mbalimbali.Utakumbuka mwaka huu jinsi mitihani ya kidato cha nne ilivyovuja.Kwa upande mwingine kumekuwepo na kuongezeka kwa lawama kwamba kiwango cha elimu nchini kinazidi kushuka.Profesa Jumanne Maghembe ni Mbunge wa CCM akiwakilisha Wilaya ya Mwanga iliyopo mkoani Kilimanjaro. Unakubaliana na mtazamo kwamba kiwango cha elimu nchini kinazidi kuporomoka siku baada ya siku?Kama jibu ni ndio,nani unadhani anatakiwa kubebeshwa lawama?Nini kifanyike?
Kama wewe ni msomaji mzuri wa magazeti na majarida mbalimbali kutoka Tanzania,basi sina shaka kabisa kwamba jina Maggid Mjengwa (pichani) litakuwa sio geni kwako! Makala zake za kusisimua,kuchokoza hisia na kujenga hoja za nguvu ni miongoni mwa vivutio muhimu vya wasomaji wa magazeti ndani na nje ya Tanzania. Leo hii tunaweza kabisa kuthubutu kusema kwamba Maggid ni miongoni mwa wanahabari bora tulionao kwani hana uoga wowote pale anapokuwa anaandika au kuongelea jambo ambalo analiamini kwa dhati.
Lakini Maggid,kama ambavyo pengine unafahamu tayari, haishii magazetini tu bali pia ni blogger maarufu hivi sasa. Blog yake ya picha ambayo mwenyewe anaiita “kijiji” na hivyo wasomaji wake na watembeleaji wake “wanakijiji”, imejipatia umaarufu sana kwa kuonyesha au kwenda kule ambapo ndiko kunahesabika kuwa kwenye hali halisi ya maisha ya mtanzania. Ukiitembelea na kuisoma blog yake vizuri kwa kutizama picha lukuki zinazoipamba blog yake,utaweza kuwa jaji mzuri kama “bongo ni tambarare” au bado zile ahadi za uchaguzi uliopita ni mbwembwe za kisiasa tu.Mwenyewe anasema blog yake ni kimbilio na sauti kwa wale ambao kila mara huwa wanasahauliwa!
Maggid pia ni mjasiriamali.Yeye ndiye Mkurugenzi Mtendaji wa kampuni ijulikanayo kama Ikolo Investment Co ambao ndio wachapishaji wa Gozi Spoti; jarida la michezo, sanaa, maisha na burudani linalotoka kila Jumatano. Maggid pia ni mwanamichezo,mpenda michezo na shabiki mkubwa wa soka.
Hivi karibuni,baada ya kumsaka kwa muda mrefu kutokana na ratiba zake za kazi kumbana,tulifanikiwa kupata fursa ya kufanya naye mahojiano utakayoyasoma hivi punde.Kama ambavyo ungetegemea,Maggid anatoa “darasa” katika mahojiano haya.Mbali ya kukupa historia ya maisha yake kwa undani,Maggid anakumbusha vipengele fulani fulani vya historia ya nchi yetu ambavyo ni muhimu. Lakini kwa mapana, anaongelea kuhusu suala la uandishi na pia blog yake bila kusahau changamoto ambazo nchi yetu inakabiliwa nazo hivi leo katika nyanja mbalimbali. Fuatana nasi katika mahojiano yafuatayo; (more…)
Jina lake kamili ni Robert Gathecha Mongi.Wengi hivi leo tunamtambua kama Bobby.Bila shaka kabisa,Bobby ni miongoni mwa wasimamizi mahiri wa shughuli(MC),watangazaji wa radio na televisheni ambao Tanzania ya leo inaweza kujivunia.Awe anasimamia shughuli,radioni au kwenye televisheni ukimsikiliza utagundua jambo moja;anaipenda kazi yake na anaifanya kwa umakini na utulivu wa hali ya juu.Pengine utulivu huo ndio uliomfanya awe ni mtangazaji wa kutegemewa katika vituo mbalimbali vya radio nchini Tanzania na pia msimamizi wa shughuli zenye hadhi za kimataifa.
Pamoja na mafanikio na “soko” ambalo tayari alikuwa ameshajitengenezea,hivi karibuni alifanya uamuzi mgumu wa kuamua kurudi shuleni ili kunoa zaidi kipaji alichonacho.Hivi sasa anasoma katika Chuo Kikuu cha Cape Town nchini Afrika Kusini.Mbali na kuamua kurudi shule,Bobby ndio kwanza alikuwa “amepata jiko” kabla ya kuwa baba mapema baadaye.Mchanganyiko huo wa mambo ndio unaotufanya tuuite uamuzi wake wa kurudi shule kuwa mgumu!How is he handling all these?
Hivi karibuni tulipata nafasi ya kuzungumza naye machache kuhusiana na maisha yake,shule,ndoto zake na mengineyo mengi.Je anasemaje kuhusu Afrika Kusini anaposomea hivi sasa?Anasomea nini?Nini ushauri wake kwa vijana wanaoota kila siku kwenda “bondeni”?Anazungumziaje maendeleo ya muziki na filamu ya Tanzania akilinganisha na Afrika Kusini? Fuatana nasi katika mahojiano yafuatayo; (more…)
Kama wewe ni mfuatiliaji wa maendeleo na mapinduzi mbalimbali katika zana za habari na mawasiliano ya umma,yawezekana umeshawahi kujiuliza maswali kadha wa kadha kuhusu mitandao kama Wikipedia. Wikipedia hivi leo ni mojawapo ya mitandao ambayo ina watembeleaji na wachangiaji lukuki kila siku. Bahati nzuri au mbaya ni kwamba Wikipedia inaendelezwa na watu kama mimi na wewe.Kuna uzuri wake na kuna ubaya wake. Ukweli huo ndio pengine unaufanya mtandao wa Wikipedia kuvutia wachunguzi na watafiti mbalimbali wa zana mpya za mawasiliano ya umma.
Hivi karibuni kituo kimoja cha televisheni cha nchini Uholanzi, VPRO Backlight, wameandaa documentary waliyoipa jina la The Truth According to Wikipedia.Miongoni mwa watu ambao wamehojiwa katika documentary hiyo ni Ndesanjo Macha(pichani) ambaye wengi hivi leo tunamfahamu kama “Mfalme wa Blog za Kitanzania”. Ndesanjo ndiye chachu ya kuanzishwa kwa blog nyingi za watanzania kama tunavyoziona na kuzitembelea hivi leo.
Tunakusihi uitazame documentary hiyo hapo chini kwani tuna uhakika utajifunza mengi na pia kupata majibu mengi ya maswali ambayo pengine umekuwa nayo kuhusu Wikipedia. Baada ya hapo(kama utaona yafaa) usisite kujiunga na Wikipedia katika lugha ya Kiswahili ili nawe uwe mmoja miongoni mwa mamilioni ya wanajumuia(kutoka lugha na mataifa mbalimbali ulimwenguni) walio mstari wa mbele katika kupashana habari, kubadilishana maarifa, kuhifadhi historia mtandaoni nk nk.Ukitaka kusoma mahojiano tuliyowahi kufanya na Ndesanjo Macha siku za nyuma bonyeza hapa.Blog ya Ndesanjo unaweza kuitembelea kwa kubonyeza hapa.

