
Zipo habari ambazo huwa mara nyingine sipendi hata kuziandika.Lakini kwa sababu kuandika na kukupa wewe msomaji taarifa mbalimbali hususani zinazowahusu “celebrities” wa kwetu na hata wa pande zingine za dunia,ndilo jukumu mama la BC,sina budi.Ni wajibu.
Mojawapo ya habari hizo ni hii ifuatayo.Kwa mujibu wa vyanzo mbalimbali vya habari, mrembo wa Tanzania kwa mwaka wa 2009(Miss Tanzania 2009),Miriam Gerald pamoja na rafiki yake wa kiume(boyfriend) anayeitwa Kennedy, leo wamepandishwa kizimbani katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Wilaya ya Kinondoni wakikabiliwa na shtaka la kufanya vurugu na kuharibu mali za Bendi ya muziki ijulikanayo kama Volcano Sound ambayo inamilikiwa na Taji Mbaraka(mtoto wa gwiji la muziki Tanzania,Hayati Mbaraka Mwaruka Mwinshehe). Vurugu hiyo ilifanyika katika ukumbi wa TPDC uliopo Mikocheni.
Mashtaka dhidi ya mrembo huyo aliyetuwakilisha kule nchini Afrika Kusini miezi kadhaa iliyopita katika kipute cha urembo wa dunia(Miss World) ilifunguliwa katika kituo cha polisi cha Oysterbay na kupewa jalada lenye namba za kumbukumbu OB/RB/2267/010 likiwa limepambwa na shtaka la Kuharibu Mali na Shambulio.
Miss Tanzania 2009 Miriam Gerald(kulia) na boyfriend Kennedy wakiwa mahakamani hivi leo.Picha na Mroki Mroki
Ingawa kila mshtakiwa hana makosa mpaka hapo mahakama itakapothibitisha(innocent until proven guilty) ni wazi kwamba habari kama hizi sio nzuri kwa sio tu Kamati ya Miss Tanzania inayoongozwa na Uncle Hashim Lundenga,bali pia kwa umma wa watanzania na hususani vijana wadogo ambao wanawaangalia celebrities wetu kama role models. Tusubiri tuone itakuwaje.

Wakati mbio za kumsaka mrembo wa Tanzania(Miss Tanzania) ndio zimeshaanza kupamba moto, nadhani utakubaliana nasi kusema kwamba miongoni mwa warembo ambao Tanzania iliwahi kutoa na kisha kukazuka mjadala mkali ni Miss Tanzania 2007,Richa Adhia.Rangi halisi(true colours) za wengi wetu zilijitokeza pale.
Pichani ni Miss Tanzania 2007, Richa Adhia(kushoto) akiwa na mama yake mzazi,Maria walipokuwa wakifuatilia uzinduzi wa video za muziki hapo juzi jijini Dar-es-salaam.
Picha kwa hisani ya John Bukuku

Miezi kadhaa tu imebakia kabla mrembo mpya wa Tanzania(Miss Tanzania 2009) hajapatikana. Tayari mashindano ya vitongojini yameshaanza huku matumaini yakiwa makubwa zaidi kutokana na kuongezwa kwa udhamini mzito wa kampuni ya simu za viganjani ya Vodacom.
Kwanini Hatushindi? Hilo ni swali ambalo bado litaendelea kuumiza vichwa.Lakini huenda mwaka huu tukatoka kwani habari nilizonazo ni kwamba umakini na weledi wa hali ya juu umejumuishwa katika zoezi zima la kumpata mshindi.
Pichani ni Miss Tanzania 2008,Nasreem Karim, ambaye pamoja na kuwa na viwango vya kutosha tu,hakufua dafu katika mashindano yaliyopita!

Mbio za kumsaka mrithi wa taji la Miss Tanzania zimeanza tena.Wadhamini wa shindano hilo,kampuni ya simu za mkononi Vodacom,wameingia mkataba mpya na Kamati ya Miss Tanzania.Kwa habari zaidi unaweza kusoma hapa.
Pichani kutoka kulia kwenda kushoto ni Hashimu Lundenga,Mkurugenzi wa Kampuni ya Lino Agency International ambao ndio wasimamizi wakuu wa shindano hilo,Miss Tanzania 2008,Nasreem Karim na George Rwehumbiza,Mkuu wa Kitengo Cha Udhamini na Mawasiliano Vodacom.

Aliyewahi kuwa Miss Tanzania 2006,Wema Sepetu(pichani) na mwenzake aitwaye Asha Jumbe,wote wakazi wa Tabata Senene jijini Dar-es-salaam wamefikishwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kinondoni wakikabiliwa na tuhuma za kuharibu mali.Kwa undani zaidi wa habari hii,bonyeza hapa.

BALOZI wa REDDS Angela Luballa(pichani) leo aliwashangaza watu alipoamua kurejesha taji hilo wiki moja tangu avalishwe.
Luballa ambaye pia alishika nafasi ya tatu katika shindano la kumsaka Miss Tanzania, amesema kuwa imani yake haimruhusu kuwa Balozi wa REDDS.
“Imani yangu kwa Yesu ni kubwa mno na hainiruhusu mimi kuwakilisha REDDS, hivyo nimeamua kurejesha taji na zawadi za fedha nilizopewa,” alisema Luballa.Tembelea blog ya Lukwangule kwa undani zaidi wa habari hii ambayo kwa vyovyote vile itazua mjadala.Kipi kinakubalika kwa Yesu na kipi hakikubaliki?Imani ni nini hasa?Je ni kweli hakuna shinikizo?Bonyeza hapa.

Baada ya kuwa ulingoni kwa mwaka mzima akiwa kama Miss Tanzania 2007,Richa Adhia(kushoto) sasa amempisha Nasreem Karim(Miss Tanzania 2008,kulia).Nini tutavuna nini mwaka huu kwenye steji ya ulimwengu(Miss World) hapo October 4 huko jijini Kiev,Ukraine?Ni jambo la kusubiri na kuona huku tukitakiana kila la kheri.
Photo/Michuzi

Sambamba na shindano la kumtafuta Miss Tanzania 2008,palikuwepo pia mchakato ulioendeshwa na kampuni ya Global Publishers ili kumpata mrembo ambaye watu mbalimbali waliona ndiye mwenye mvuto zaidi ya wengine.Tutakuwa hatukosei sana tukisema kwamba zoezi hilo lilikuwa ni kama vile kutafuta mrembo ambaye ni People’s Choice.Aliyeibuka mshindi katika hilo ni mrembo Kelly Kamwelu(pichani) ambaye ndiye Miss Ilala 2008.BC inampongeza na kumtakia kila la kheri.
Photo/GP

Zimebaki siku chache tu kabla ya Tanzania kumpata mrembo wake wa mwaka huu (Miss Tanzania 2008). Wadau wa masuala ya urembo tayari wameshaanza kukuna vichwa wakijiuliza ni nani ataibuka mshindi mwaka huu. Mashindano ya Miss World mwaka huu yanatarajiwa kufanyika tarehe 4 October huko jijini Kiev nchini Ukraine.
Sasa wakati tukisubiri kumjua atakayetuwakilisha mwaka huu huko Ukraine, kampuni ya Global Publishers,wanaendesha zoezi ambalo litakuwezesha wewe msomaji na mtembeleaji wa mitandao,kushiriki katika zoezi la kumpata Miss Global Publishers miongoni mwa warembo wanaoshiriki Miss Tanzania mwaka huu.Utakachokuwa unachagua sio Miss Tanzania bali ni Miss Global Publishers.Utakuwa unamchagua mrembo ambaye unadhani ndio mwenye mvuto wa sura kupita wenzake wote.Mshindi wa taji hilo la Miss Global Publishers atajinyakulia taji na pia kitita cha Tshs 500,000. Kwa maelezo zaidi na jinsi ya kupiga kura tembelea tovuti ya Global Publishers kwa kubonyeza hapa. Zoezi hili limepewa baraka na Kamati ya Miss Tanzania.Pichani ni warembo wanaowania taji la Miss Tanzania 2008.

Pichani warembo ambao mwaka huu watakuwa wanawania taji la Miss Tanzania 2008.Warembo hao wameingia kambini hivi leo huko Bagamoyo katika Hoteli ya Paradise tayari kabisa kwa shindano hilo la Miss Tanzania 2008 litakalofanyika August 2 mwaka huu.
Photo/Issa Michuzi

