
Kwa faida ya msomaji ambaye, kwa sababu moja au nyingine hawezi kuwatambua waliopo pichani; Kutoka kushoto ni Kenneth Kaunda,maarufu kama KK(Rais wa Zambia kuanzia mwaka 1964 mpaka 1991),Julius Kambarage Nyerere(Baba wa Taifa la Tanzania na Rais wake kuanzia mwaka 1964 mpaka 1985),Jomo Kenyatta(Rais wa Kenya kuanzia mwaka 1964 mpaka 1978.),Milton Obotte (Rais wa Uganda kuanzia mwaka 1966 mpaka 1971 na kisha mwaka 1980 mpaka 1985)
Je,wewe binafsi unajifunza au umejifunza nini katika kufuatilia jinsi walivyoendesha maisha yao,utumishi wao kwa umma nk? Unadhani kuna yepi ya msingi ambayo sisi kama wananchi na pia viongozi wetu wa hivi sasa tunaweza kujifunza kutoka kwa watu hao?Kumbuka mazuri na mabaya yao kwani kama tulivyo sote,they were not perfect,no one is!
Leo ni mwaka mpya.Hongera kwa kuiona 2010.Kama ilivyo ada au desturi,mwaka mpya huenda sambamba na salamu kutoka kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Ni salamu kutoka kwa Jakaya Mrisho Kikwete.
Ninachoweza kukuambia ni kwamba,hizi huwa sio salamu tu bali mwelekeo mzima wa nchi. Kama unataka kujua tulipo,tulipotoka na tunapoelekea,basi huna budi kuzisoma salamu za Mheshimiwa Rais. Sio lazima uzisome zote kwa mkupuo.Unaweza kusoma taratibu kifungu baada ya kifungu. Kila la kheri.
SALAMU ZA MWAKA MPYA ZA RAIS WA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA, MHESHIMIWA JAKAYA MRISHO KIKWETE, KWA WATANZANIA,
TAREHE 31 DESEMBA, 2009
Utangulizi
Ndugu Wananchi;
Kama ilivyo ada naomba nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutujaalia uhai na kutuwezesha kufika siku ya leo ya kuuaga mwaka 2009 na kuukaribisha mwaka 2010. Wapo wenzetu wengi tulioanza nao mwaka lakini hawakujaaliwa kuwa nasi siku hii ya leo kwa kuwa wametutangulia mbele ya haki. Tunamuomba Mwenyezi Mungu awape mapumziko mema. Kwa wenzetu wanaougua tuwaombee awape nafuu ya haraka ili waendelee kutoa mchango wao katika maendeleo yao, jamii zao na taifa zima kwa jumla. Aidha, tuendelee kuomba rehema za Mola wetu atujaalie afya njema na umri mrefu ili tuweze kuushuhudia mwaka wote wa 2010 na miaka mingine mingi ijayo.
Ndugu Wananchi;
Kama wote mlivyosikia, leo, siku ya mwisho ya mwaka 2009, Taifa letu lilipata msiba mkubwa wa kuondokewa na Mzee wetu, Mzee Rashid Mfaume Kawawa, Makamu wa Rais na Waziri Mkuu Mstaafu.
Kama nilivyoeleza wakati nalitangazia taifa kifo chake, huu ni msiba mkubwa kwa Taifa letu. Tumepoteza mmoja wa viongozi mashuhuri. Marehemu alijitoa muhanga kupigania uhuru na maendeleo ya nchi yetu. Wakati wote wa uhai wake alitumia uwezo wake na vipaji vyake alivyojaaliwa na Mola wake kujenga, kuendeleza na kutetea maslahi ya Taifa lake na Chama chake CCM na TANU kabla yake. Mzee Kawawa alikuwa mhimili mkubwa kwa Taifa letu na Chama cha Mapinduzi hata baada ya kustaafu uongozi. Sote tutaendelea kumkumbuka kwa moyo wake wa ubinadamu na mchango wake usiokuwa na kifani kwa nchi yetu na watu wake. Tuendelee kumuombea kwa Mwenyezi Mungu ailaze roho yake mahali pema peponi. Amin.
Nchi Salama na Tulivu
Ndugu Wananchi,
Ni jambo la faraja na kuonea fahari kwamba tunaumaliza mwaka 2009 taifa letu likiwa salama na kwamba amani na utulivu viliendelea kutawala. Aidha, taifa letu limeendelea kuwa moja na watu wake wameendelea kuwa wamoja, licha ya kuwepo kwa changamoto za hapa na pale zilizotokana na harakati za vyama vya siasa na kauli za baadhi ya wanasiasa na viongozi wa kijamii wakiwemo wale wa dini. (more…)

Kesho ni 9 Desemba.Bila shaka unaelewa umuhimu wa siku hiyo kwa nchi yetu.Kama historia ya nchi imekupitia kushoto,naomba nikukumbushe.Ni siku ya kukumbuka siku mkoloni alipoamua kukubali yaishe na kuirudisha nchi kwa wenye nchi yaani wananchi.Uhuru.
Sitaki kuhesabu ni miaka mingapi imepita tangu mwenge ule ulipopandishwa kileleni Kilimanjaro.Nina sababu zangu.
Wakati wa kumbukumbu kama hizi za Uhuru,kinachoendelea ni hotuba,ahadi za uongo na kweli na mambo kama hayo.Tunatakiana kheri pia.Kwa kipi?Sina uhakika.Hapo ndipo katika pitapita yangu mtandaoni,kwenye wavuti na blogs mbalimbali,nikakutana na ya Mubelwa akiwa pale Laurel,MD nchini Marekani.Yeye anasema,wakati anawatakia watanzania wote kila la kheri katika kusheherekea miaka— ya Uhuru,ana maswali 10 kwenda kwa Rais Jakaya Mrisho Kikwete.Bonyeza hapa uyasome.
Mubelwa,sidhani kama atajibu.Hulka hiyo bado haipo.Ninachoweza kukuhakikishia ni kwamba atayasoma.Kama sio yeye basi “miongoni mwao”.

Viongozi wengi wa Africa wapo jijini Cairo nchini Misri kuhudhuria kongamano kuhusu ushirikiano baina ya nchi zao na China.Rais wetu,Jakaya Kikwete,ni miongoni mwa viongozi wanaohudhuria kongamano hilo.
Sasa kama unavyojua,uhusiano wa China na nchi za Africa ikiwemo yetu ya Tanzania una historia ndefu.Kuna ambao wanasema China ndio nchi pekee duniani ambayo imekuwa “true darling” wa bara la Africa.Wanaosema hivyo wanaangalia vitu kama misaada kutoka China,unafuu wa kufanya biashara na China,masharti nafuu ya misaada na mambo kama hayo.
Lakini katika siku za karibuni,uhusiano baina ya nchi za Africa na China umekuwa ukiongelewa katika namna tofauti.Masuala ya biashara,masoko,misaada nk ndio yameshika hatamu badala ya habari za udugu na ujamaa zilizokuwepo enzi zile kina Nyerere na Mao walipokuwa wakipanda mbegu za ushirikiano wa China na Tanzania.Hapo ndipo suala la kujadili au kufanya tathmini za uhusiano au ushirikiano huu linapokuwa na umuhimu wa aina yake.
Mijadala mbalimbali inazuka kila kukicha.Swali lililopo katika kichwa cha habari hapo juu ndilo linasumbua.Nani anafaidika zaidi na mahusiano haya? Je China wanafaidika zaidi au Africa ikiwemo nchi yetu ya Tanzania ndio inafaidika? Na bila kuficha wala kukwepesha macho,mtanzania wa kawaida ndiye anayefaidika au zaidi na uhusiano huo au ni viongozi wetu?Naomba kufungua mjadala.
Pichani ni Rais Jakaya Kikwete akiwa na Rais wa Misri,Hosni Mubarak huko Misri ambapo Rais Kikwete yupo kuhudhuria Kongamano la Ushirikiano baina ya China na Africa.Picha na Freddy Maro-Ikulu)
Wiki hii mwanasiasa aliyevuma zaidi ni Rais wa Jamhuri ya Muungano ya Tanzania,Jakaya Mrisho Kikwete.Kama umefuatilia vizuri kwenye vyombo mbalimbali vya habari,habari kubwa ilikuwa kuhusu utaratibu mpya aliouanzisha Rais Kikwete wa kuongea na wananchi na pia kuwapa nafasi ya kuuliza maswali ya papo kwa hapo.
Ingawa wananchi wengi wakiwemo pia viongozi wa vyama vya upinzani kama vile Mhe.Dr.Slaa,wanasema Rais Kikwete alipinga chenga au kujibu juu juu sana maswali ya wananchi,mimi nampongeza kwa kuanzisha utaratibu huu. Kama utadumu na kama utakuwa huru(kunawezwa wekwa mamluki wa kuuliza maswali;hakuna linaloshindikana karne hii),naamini ni njia nzuri ya Rais kuwasiliana na wananchi na japo kujua kwa mbali,yanayowakera.Hongera JK! Bado tu kufungua blog na account za twitter,facebook na myspace.Watanzania wengi sana siku hizi wanatumia zana hizo za mawasiliano.Obama yeye anazo zote tayari.
Pamoja na sifa hizo,kuna kitu ambacho kinanifanya nigune kidogo.Kwanini Mheshimiwa Rais amesubiri mpaka umebakia mwaka mmoja kabla ya uchaguzi ndio aanzishe utaratibu huu?Nia ni kusikia kweli hoja na maswali ya wananchi au ndio “kujiweka sawa” kabla ya uchaguzi?
Nini maoni yako kuhusiana na utaratibu huu mpya wa Rais Kikwete?Na je kama uliangalia zoezi zima la hotuba,maswali na majibu,unasemaje?Unampa alama gani Mheshimiwa Rais?A,B,C,D au…?
Kama lipo jambo ambalo liliamsha hisia tofauti kwenye ulingo wa siasa,basi ni tamko au kitendo cha mwanasiasa kijana,Zitto Kabwe,kutangaza nia ya kugombea uenyekiti wa Chama Cha Demokrasia na Maendeleo(CHADEMA)
Zitto Kabwe ambaye hivi sasa anashikilia nafasi ya Naibu Katibu Mkuu katika chama hicho,anasema pamoja na kwamba anaamini na kuafiki kwamba Mwenyekiti wa sasa wa chama hicho,Freeman Mbowe,ni kiongozi mzuri na kwamba amekitoa mbali chama hicho,wakati umefika wa kuwa na mabadiliko.Zitto anasema chama kimetawaliwa na “kufukuzana” uanachama. Jambo hilo lazima lifikie kikomo,anasema Zitto.
Kisha anasema lazima CHADEMA kijiandae kuchukua dola. Kwa maana hiyo labda tunaweza kusema Zitto anamaanisha kwamba CHADEMA ilivyo hivi sasa,hakiwezi au hakistahili kushika dola.Kinahitaji maandalizi!Hapa ni muhimu kukumbuka kwamba uchaguzi mkuu ni 2010 na sio 2011 au 2012.
Kama utakumbuka,miezi kadhaa iliyopita Zitto Kabwe alitangaza nia yake ya kutogombea tena nafasi ya Ubunge wa Kigoma Kaskazini anayoishikilia.Alisema anataka kujikita zaidi kwenye taaluma yake na hivyo kuachana kidogo na mambo ya siasa.Sasa tunajua kwamba hakuwa akimaanisha alichokuwa anakisema.Alijivika uhalisi wa siasa.
Je unasemaje kuhusiana na uamuzi wa Zitto Kabwe kutaka kugombea nafasi ya Uenyekiti wa CHADEMA?Unadhani atakuwa ni nahodha bora wa chama hicho cha upinzani zaidi ya Mwenyekiti aliyepo madarakani hivi sasa?
***Niliwahi kufanya mahojiano na Zitto Kabwe takribani miaka miwili iliyopita.Bonyeza hapa usome mahojiano yale ili pengine upate picha zaidi juu ya Zitto Kabwe.
Kama tulivyoanza wiki iliyopita,wiki hii tena tunagusa kwenye anga za siasa. Kama umekuwa ukifuatilia kwa makini yaliyojiri wiki hii, kubwa zaidi lilikuwa suala la Mheshimiwa Spika,Samuel Sitta, kukingiwa kifua na wapinzani kutokana na kile ambacho CCM(chama chake Sitta) wamekiona kama “kuwageuka” baada ya kuruhusu masuala ya mijadala ya ufisadi iendelee bungeni. Walimtishia kumpokonya kabisa uanachama kama asiposikiliza.
Kinadharia wanachosema CCM ni kwamba ukiwa mwanachama au mbunge kupitia CCM,basi sio haki kunyooshea vidole mambo “mbofu mbofu” yanayoweza kuwa yanaendelea ndani ya CCM. Wanadai kama kuna kutofautiana,basi mambo hayo yamalizwe katika vikao vya chama na sio mahali pa wazi kama vile bungeni.
Wao CCM wanasema ni haki yao kumhoji au kumkemea Spika kwani yeye ni mwanachama wa CCM kama walivyo wengine. Anayesema hivyo ni Katibu Mkuu wa CCM,Yusuph Makamba. Kisha anasema bunge ni mali ya chama tawala cha CCM!
Je unadhani nini kinaendelea ndani ya CCM? Spika Samuel Sitta yupo sahihi? Makamba yupo Sahihi? Samuel Sitta ndiye mwanasiasa wetu wa wiki hii.
Kuanzia weekend hii,BC inapenda kutambulisha ukurasa mpya.Huu utakuwa ukurasa wa wanasiasa.Kila jumamosi,tutakuwa tukimuweka na kumjadili mwanasiasa mmoja ambaye katika wiki inayokuwa inaaga,amekuwa akigonga vichwa vya habari aidha kwa mambo mazuri ya kujenga au hata mabaya. Kama ni mazuri atastahili sifa, kama ni mabaya ataambiwa ukweli,ataonywa. Kutakuwa pia na nafasi ya kupiga kura za kijamii ili kupata picha pana na mtazamo wa wananchi kuhusiana na suala husika.
Hii itakuwa nafasi nzuri kwako wewe msomaji,mtembeleaji na mchangiaji wa BC kutoa mawazo yako juu ya mwanasiasa,alichokisema,alichokifanya au sera anazozipigia upatu.
Kwa kuanza leo tunaye mwanasiasa mkongwe,Kingunge Ngombale Mwiru. Bila shaka umefuatilia kwa makini malumbano yanayoendelea baina ya mwanasiasa huyo mkongwe na viongozi wa Kanisa Katoliki kufuatia kupinga kwake Waraka wa Kanisa Katoliki.
Kimsingi lilichokuwa likijaribu kufanya kanisa katoliki ni kutoa elimu kwa waumini wake kuhusiana na sifa ambazo inabidi mtu awe nazo ili apate kuchaguliwa. Bila shaka kanisa linakuwa linalenga kuamsha hisia za wananchi na hususani waumini wa kanisa hilo lenye wafuasi wengi kutokana na ukweli kwamba mwakani ni mwaka wa uchaguzi nchini Tanzania.
Kingunge yeye anadai kuunga mkono Waraka huo wa Wakatoliki ni kama kuachana na ilani ya Chama Cha Mapinduzi.
Je unadhani nani yupo sahihi katika suala hili? Je kanisa katoliki limekosea kutoa waraka au muongozo huo kwa waumini wake? Kingunge Ngombale Mwiru(pichani).Huyu ndiye mwanasiasa wetu wa wiki hii.
Photo/Father Kidevu

Hayati Baba wa Taifa,Mwalimu Julius Kambarage Nyerere na mkewe Mama Maria Nyerere wakiwa wameongozana kuelekea kwenye mojawapo ya dhifa za kitaifa enzi hizo.
Picha hii inatoka pale Mtaa Kwa Mtaa. Mtembelee kwa kubonyeza hapa.

Nimeshawahi kusema na leo nitarudia tena; Kama umekosa kabisa jambo au mambo yanayokufanya ujisikie furaha kuwa Mtanzania,basi angalau unaweza kupata ahueni unapoangalia jinsi ambavyo “demokrasia” ya nchi yetu imekuwa mfano wa kuigwa barani Afrika na hata sehemu mbalimbali za ulimwengu.Of course demokrasia yetu ina mapungufu mengi bado lakini ipi ambayo haina?Marekani au?
Mpaka leo,tangu Nyerere ang’atuke,hajatokea mtu akasema anataka kubadili katiba ili aendelee kutawala.Muda ukiisha mtu anaachia madaraka. Lakini kuachia madaraka haitoshi.Lipo suala zima la kuachia madaraka na pia kuendelea kushiriki katika shughuli mbalimbali za kitaifa na hata kimataifa kwa jina la Tanzania. Hali hii ni lazima ilindwe kwani ni wazi kwamba haitokei kama ajali.
Pichani ni Marais wetu,wastaafu Ally Hassan Mwinyi(mwisho kulia),Benjamini William Mkapa(mwisho kushoto) na Rais aliyepo madarakani hivi sasa,Jakaya Mrisho Kikwete(katikati). Kama unavyoona pichani wapo na wake zao au kina mama zetu wa kwanza waliostaafu na aliyepo kwenye uskani hivi sasa.
Sijui kama ni mimi tu ndio nimeona hili au vipi lakini nadhani mpangilio kidogo wa picha hii ulikwenda kombo.Sijui kwanini Mama Anna Mkapa ilibidi awe mbali vile na Mzee na pia Mama Sitti Mwinyi.Sijui.
Picha kwa hisani ya Bodi ya Utalii Tanzania

