
Miezi michache iliyopita, Rais Jakaya Kikwete, alifanya mabadiliko na teuzi kadhaa za mabalozi wetu katika nchi mbalimbali. Miongoni mwa mabadiliko hayo ni pamoja na yale ya kumhamisha Balozi Peter A.Kallaghe kutoka nchini Canada kwenda kuwa Balozi mpya wa Tanzania nchini Uingereza.
Wakati akijiandaa kuondoka nchini Canada kuelekea katika kituo chake kipya cha kazi nchini Uingereza,BC ilipata nafasi ya kufanya naye mahojiano maalum utakayoyasoma hivi punde.
Balozi Peter Kallaghe anaelekea nchini Uingereza kuchukua nafasi iliyoachwa na Balozi Mwanaidi Maajar ambaye amehamishiwa nchini Marekani. Fuatana nasi katika mahojiano haya;
BC: Mheshimiwa Balozi,asante sana kwa kukubali kufanya nami mahojiano haya.Nafahamu kwamba una mambo mengi mengine ya kufanya hususan wakati huu unapojiandaa kuondoka hapa Canada.Kwa hiyo nashukuru sana kwa kunipatia fursa hii.
Kwa kuanzia na kwa sababu wewe ni Balozi wa kwanza kufanya nasi mahojiano,ningependa kukuuliza swali ambalo bila shaka lipo katika vichwa vya wasomaji na wafuatiliaji wetu.Ilikuwaje mpaka ukafikia hatua ya kuteuliwa kuwa Balozi?Katika historia yako ya utumishi wa umma(Public Service) umepitia ngazi zipi,milima na mabonde yapi?Hapa ninamaanisha ulisomea wapi,ukakulia wapi na nini kilikusukuma katika ajira ya serikalini au utumishi wa umma kwa ujumla?
Balozi Peter Kallaghe: Historia yangu kielimu ni kwamba nimehama hama sana shule, kwa sababu baba yangu, Marehemu Balozi Cecil A. Kallaghe, alikuwa mtumishi wa umma na alipata kufanya kazi nje ya nchi kama Balozi.
Kwa ufupi nilisoma elimu ya msingi katika shule za OysterBay na Arusha School katika miaka ya sitini. Na nilipata elimu ya sekondari katika shule ya Pugu Secondary School. Chuo Kikuu nilisomea Kieve State University ambapo nilihitimu na degree ya M.A. in International Relations. Aidha nina Post-Graduate Diploma kwenye Diplomacy, Negotiatiations and Strategic Communications.
Kikazi maisha yangu yote nimefanya kazi katika Wizara ya Mambo ya Nje na Ikulu, hususani kama msaidizi wa Rais kwa kipindi kirefu.
Niliteuliwa Balozi kwa mara ya kwanza mwaka 2004 nikiwa pale Ikulu, na mwaka 2007 niliteuliwa Balozi nchini Canada. Mwaka 2010 nimeteuliwa kuwa Balozi wa Tanzania nchini Uingereza (UK).
Kuteuliwa kwangu kuwa balozi nakuchukulia kama fursa ya kipekee niliyopewa ya kutoa mchango wangu katika kulitumikia Taifa letu la Tanzania na watu wake. Na ninafanya hivyo nikitambua uzito wa dhamana hii hasa kwa nchi ambayo bado inakabiliana na changamoto nyingi za kimaendeleo.
BC: Sasa kama sikosei hii ilikuwa ni mara yako ya kwanza kuteuliwa kuwa Balozi kamili. Je,ulikuwa na matarajio gani kabla hujafunga safari kuja Canada? Je, ulichokitarajia ndicho ulichokutana nacho? (more…)
MBUNGE wa Kasulu Magharibi, Kilontsi Mporogomyi (CCM) amefikishwa katika Mahakama ya Wilaya ya Mkoa wa Dodoma kwa tuhuma za kugonga na kuua papo hapo mwenda kwa miguu ambaye hakufahamika jina mara moja.
Akimsomea mashitaka yake jana mbele ya Hakimu Mkazi Hassan Momba, Mwendesha Mashitaka wa Polisi Beatrice Nsana, alisema mtuhumiwa huyo alitenda kosa hilo Julai 11 mwaka huu saa 5.30 usiku eneo la Wajenzi, mjini hapa.
Nsana alisema mtuhumiwa Mporogomyi alikuwa akiendesha gari namba T288ASJ aina ya Toyota Land Cruiser akashindwa kusimama amruhusu mwenda kwa miguu huyo avuke barabara, akamgonga.
Mwendesha mashitaka huyo alidai kuwa Mbunge huyo anakabiliwa na mashitaka mawili; kuendesha gari kwa uzembe na kusababisha kifo.
Alidai kuwa upelelezi wa kesi hiyo haujakamilika; mshitakiwa alikana mashitaka na kusema hamfahamu marehemu wala makazi yake.
Mtuhumiwa alipata dhamana baada ya kukidhi masharti ya Sh milioni 5 na kesi hiyo iliahirishwa hadi Agosti 5 mwaka huu itakapotajwa.
Source:Habari Leo.
Photo Courtesy: Tanzania Parliament Website.
Upo msemo usemao “Biashara au mali bila daftari,hupotea bila habari”.Msemo huo naweza kuufananisha na ugumu wa kuendesha kitu kama nchi bila bajeti.Haiwezekani. Pengine hiyo ndio sababu kubwa kwamba kila mwaka,Waziri wa Fedha,pamoja na majukumu mengine aliyonayo, huwa pia ana jukumu la kuwasilisha bungeni Bajeti ya mwaka unaofuata wa fedha na uchumi.
Tarehe 10 Juni mwaka 2010 ilikuwa ni siku ya kuwasilishwa kwa Bajeti ya nchi yetu kwa mwaka 2010/2011. Pengine umeshapata nafasi ya kuisoma au kuipitia. Nimeona ni jambo jema niiweke hapa BC bajeti hiyo kwa kuzingatia mambo kadhaa yakiwemo; Huu ni Mwaka wa Uchaguzi.Ukitaka kujua tunapoelekea katika miaka kadhaa ijayo,basi huna budi kuisoma kwa makini bajeti hii.
Pili,baada ya kuyumba kwa uchumi wa dunia,ni muhimu kujua nchi zinazoendelea kama yetu ya Tanzania zimejipanga namna gani kukabiliana na hali halisi ya “ahadi za misaada na mikopo” ambazo ni dhahiri zitakuwa ngumu kutekelezeka. Je,tumejiandaaje? Tunalenga kuingiza kiasi gani kama pato la taifa na tunapanga kukopa kiasi gani kutoka kwa wafadhili? Tunapanga kutumia kiasi gani? Mwaka uliopita ulikuwaje? Kwa majibu ya maswali kama hayo na mengineyo mengi,hii hapa ni Bajeti nzima kwa mwaka 2010/2011 kama ilivyowasilishwa Bungeni na Waziri wa Fedha,Mheshimiwa Mustafa H.Mkulo(pichani) hivi karibuni;
HOTUBA YA WAZIRI WA FEDHA NA UCHUMI, MHE. MUSTAFA HAIDI MKULO (MB.), AKIWASILISHA KATIKA BUNGE MAPENDEKEZO YA SERIKALI KUHUSU MAKADIRIO YA MAPATO NA MATUMIZI KWA MWAKA 2010/2011, TAREHE 10 JUNI, 2010
UTANGULIZI
1. Mheshimiwa Spika, naomba kutoa hoja kwamba Bunge lako Tukufu likubali kujadili na kupitisha makadirio ya mapato na matumizi ya Serikali kwa mwaka wa fedha 2010/2011. Pamoja na hotuba hii, vipo vitabu vinne vinavyoelezea kwa kina takwimu mbalimbali za bajeti. Kitabu cha Kwanza kinahusu makisio ya mapato. Kitabu cha Pili na cha Tatu ni vya makisio ya matumizi ya kawaida kwa Wizara, Idara zinazojitegemea, Mikoa na Mamlaka za Serikali za Mitaa. Kitabu cha Nne kinaelezea makadirio ya matumizi ya maendeleo kwa Wizara, Idara zinazojitegemea, Mikoa pamoja na Mamlaka za Serikali za Mitaa. Aidha, upo Muswada wa Sheria ya Fedha wa mwaka 2010 ambao ni sehemu ya bajeti hii.
2. Mheshimiwa Spika, awali ya yote ningependa kuchukua nafasi hii kueleza kuwa, Bajeti ya mwaka wa fedha 2009/2010 unaomalizika mwezi huu, inakamilisha kipindi cha miaka mitano cha Serikali ya Awamu ya Nne iliyoingia madarakani Desemba 2005. Katika kipindi hiki, Bajeti imetumika kama chombo muhimu katika kutekeleza Sera na Malengo ya Uchumi na Maendeleo ya Jamii kwa kuzingatia Ilani ya Uchaguzi ya Chama Tawala cha CCM. Kwa hiyo, bajeti ya mwaka wa fedha 2010/11 inalenga kuendelea na utekelezaji wa sera na malengo ya kiuchumi na kijamii. Katika kipindi hiki, yamekuwepo mafanikio ya kuridhisha katika kutoa huduma bora kwa wananchi na kuimarisha miundombinu ili kuwezesha uchumi kukua na kupunguza umaskini. (more…)

Leo imetimia miaka 26 tangu Tanzania ilipoondokewa na aliyekuwa Waziri Mkuu, Hayati Edward Moringe Sokoine,aliyefariki kwa ajali ya gari nje kidogo ya mji wa Morogoro akiwa safarini kutokea mkoani Dodoma yalipo makao makuu ya chama na serikali kuhudhuria kikao cha Bunge.
Sokoine,alionekana kuwa tegemeo la watu,ndoto ya kweli ya wanyonge.Bahati mbaya ni kwamba ajali ile ndio ilihitimisha safari yake hapa duniani na kuwaacha wengi wakiamini kwamba endapo angeishi zaidi,huenda Tanzania tunayoiona leo,ingekuwa tofauti.
Je ni kitu gani kinafanya imani kwamba angeendelea kuishi angeibadili sura ya Tanzania?Ni kauli zake,vitendo vyake au imani tu ya mwananchi wa kawaida? Na je unadhani angekuwa hai hivi leo angepambana vipi na “ufisadi”? Mungu aendelee kuilaza pema peponi roho yake.

Kwa faida ya msomaji ambaye, kwa sababu moja au nyingine hawezi kuwatambua waliopo pichani; Kutoka kushoto ni Kenneth Kaunda,maarufu kama KK(Rais wa Zambia kuanzia mwaka 1964 mpaka 1991),Julius Kambarage Nyerere(Baba wa Taifa la Tanzania na Rais wake kuanzia mwaka 1964 mpaka 1985),Jomo Kenyatta(Rais wa Kenya kuanzia mwaka 1964 mpaka 1978.),Milton Obotte (Rais wa Uganda kuanzia mwaka 1966 mpaka 1971 na kisha mwaka 1980 mpaka 1985)
Je,wewe binafsi unajifunza au umejifunza nini katika kufuatilia jinsi walivyoendesha maisha yao,utumishi wao kwa umma nk? Unadhani kuna yepi ya msingi ambayo sisi kama wananchi na pia viongozi wetu wa hivi sasa tunaweza kujifunza kutoka kwa watu hao?Kumbuka mazuri na mabaya yao kwani kama tulivyo sote,they were not perfect,no one is!
Leo ni mwaka mpya.Hongera kwa kuiona 2010.Kama ilivyo ada au desturi,mwaka mpya huenda sambamba na salamu kutoka kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Ni salamu kutoka kwa Jakaya Mrisho Kikwete.
Ninachoweza kukuambia ni kwamba,hizi huwa sio salamu tu bali mwelekeo mzima wa nchi. Kama unataka kujua tulipo,tulipotoka na tunapoelekea,basi huna budi kuzisoma salamu za Mheshimiwa Rais. Sio lazima uzisome zote kwa mkupuo.Unaweza kusoma taratibu kifungu baada ya kifungu. Kila la kheri.
SALAMU ZA MWAKA MPYA ZA RAIS WA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA, MHESHIMIWA JAKAYA MRISHO KIKWETE, KWA WATANZANIA,
TAREHE 31 DESEMBA, 2009
Utangulizi
Ndugu Wananchi;
Kama ilivyo ada naomba nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutujaalia uhai na kutuwezesha kufika siku ya leo ya kuuaga mwaka 2009 na kuukaribisha mwaka 2010. Wapo wenzetu wengi tulioanza nao mwaka lakini hawakujaaliwa kuwa nasi siku hii ya leo kwa kuwa wametutangulia mbele ya haki. Tunamuomba Mwenyezi Mungu awape mapumziko mema. Kwa wenzetu wanaougua tuwaombee awape nafuu ya haraka ili waendelee kutoa mchango wao katika maendeleo yao, jamii zao na taifa zima kwa jumla. Aidha, tuendelee kuomba rehema za Mola wetu atujaalie afya njema na umri mrefu ili tuweze kuushuhudia mwaka wote wa 2010 na miaka mingine mingi ijayo.
Ndugu Wananchi;
Kama wote mlivyosikia, leo, siku ya mwisho ya mwaka 2009, Taifa letu lilipata msiba mkubwa wa kuondokewa na Mzee wetu, Mzee Rashid Mfaume Kawawa, Makamu wa Rais na Waziri Mkuu Mstaafu.
Kama nilivyoeleza wakati nalitangazia taifa kifo chake, huu ni msiba mkubwa kwa Taifa letu. Tumepoteza mmoja wa viongozi mashuhuri. Marehemu alijitoa muhanga kupigania uhuru na maendeleo ya nchi yetu. Wakati wote wa uhai wake alitumia uwezo wake na vipaji vyake alivyojaaliwa na Mola wake kujenga, kuendeleza na kutetea maslahi ya Taifa lake na Chama chake CCM na TANU kabla yake. Mzee Kawawa alikuwa mhimili mkubwa kwa Taifa letu na Chama cha Mapinduzi hata baada ya kustaafu uongozi. Sote tutaendelea kumkumbuka kwa moyo wake wa ubinadamu na mchango wake usiokuwa na kifani kwa nchi yetu na watu wake. Tuendelee kumuombea kwa Mwenyezi Mungu ailaze roho yake mahali pema peponi. Amin.
Nchi Salama na Tulivu
Ndugu Wananchi,
Ni jambo la faraja na kuonea fahari kwamba tunaumaliza mwaka 2009 taifa letu likiwa salama na kwamba amani na utulivu viliendelea kutawala. Aidha, taifa letu limeendelea kuwa moja na watu wake wameendelea kuwa wamoja, licha ya kuwepo kwa changamoto za hapa na pale zilizotokana na harakati za vyama vya siasa na kauli za baadhi ya wanasiasa na viongozi wa kijamii wakiwemo wale wa dini. (more…)

Kesho ni 9 Desemba.Bila shaka unaelewa umuhimu wa siku hiyo kwa nchi yetu.Kama historia ya nchi imekupitia kushoto,naomba nikukumbushe.Ni siku ya kukumbuka siku mkoloni alipoamua kukubali yaishe na kuirudisha nchi kwa wenye nchi yaani wananchi.Uhuru.
Sitaki kuhesabu ni miaka mingapi imepita tangu mwenge ule ulipopandishwa kileleni Kilimanjaro.Nina sababu zangu.
Wakati wa kumbukumbu kama hizi za Uhuru,kinachoendelea ni hotuba,ahadi za uongo na kweli na mambo kama hayo.Tunatakiana kheri pia.Kwa kipi?Sina uhakika.Hapo ndipo katika pitapita yangu mtandaoni,kwenye wavuti na blogs mbalimbali,nikakutana na ya Mubelwa akiwa pale Laurel,MD nchini Marekani.Yeye anasema,wakati anawatakia watanzania wote kila la kheri katika kusheherekea miaka— ya Uhuru,ana maswali 10 kwenda kwa Rais Jakaya Mrisho Kikwete.Bonyeza hapa uyasome.
Mubelwa,sidhani kama atajibu.Hulka hiyo bado haipo.Ninachoweza kukuhakikishia ni kwamba atayasoma.Kama sio yeye basi “miongoni mwao”.

Viongozi wengi wa Africa wapo jijini Cairo nchini Misri kuhudhuria kongamano kuhusu ushirikiano baina ya nchi zao na China.Rais wetu,Jakaya Kikwete,ni miongoni mwa viongozi wanaohudhuria kongamano hilo.
Sasa kama unavyojua,uhusiano wa China na nchi za Africa ikiwemo yetu ya Tanzania una historia ndefu.Kuna ambao wanasema China ndio nchi pekee duniani ambayo imekuwa “true darling” wa bara la Africa.Wanaosema hivyo wanaangalia vitu kama misaada kutoka China,unafuu wa kufanya biashara na China,masharti nafuu ya misaada na mambo kama hayo.
Lakini katika siku za karibuni,uhusiano baina ya nchi za Africa na China umekuwa ukiongelewa katika namna tofauti.Masuala ya biashara,masoko,misaada nk ndio yameshika hatamu badala ya habari za udugu na ujamaa zilizokuwepo enzi zile kina Nyerere na Mao walipokuwa wakipanda mbegu za ushirikiano wa China na Tanzania.Hapo ndipo suala la kujadili au kufanya tathmini za uhusiano au ushirikiano huu linapokuwa na umuhimu wa aina yake.
Mijadala mbalimbali inazuka kila kukicha.Swali lililopo katika kichwa cha habari hapo juu ndilo linasumbua.Nani anafaidika zaidi na mahusiano haya? Je China wanafaidika zaidi au Africa ikiwemo nchi yetu ya Tanzania ndio inafaidika? Na bila kuficha wala kukwepesha macho,mtanzania wa kawaida ndiye anayefaidika au zaidi na uhusiano huo au ni viongozi wetu?Naomba kufungua mjadala.
Pichani ni Rais Jakaya Kikwete akiwa na Rais wa Misri,Hosni Mubarak huko Misri ambapo Rais Kikwete yupo kuhudhuria Kongamano la Ushirikiano baina ya China na Africa.Picha na Freddy Maro-Ikulu)
Wiki hii mwanasiasa aliyevuma zaidi ni Rais wa Jamhuri ya Muungano ya Tanzania,Jakaya Mrisho Kikwete.Kama umefuatilia vizuri kwenye vyombo mbalimbali vya habari,habari kubwa ilikuwa kuhusu utaratibu mpya aliouanzisha Rais Kikwete wa kuongea na wananchi na pia kuwapa nafasi ya kuuliza maswali ya papo kwa hapo.
Ingawa wananchi wengi wakiwemo pia viongozi wa vyama vya upinzani kama vile Mhe.Dr.Slaa,wanasema Rais Kikwete alipinga chenga au kujibu juu juu sana maswali ya wananchi,mimi nampongeza kwa kuanzisha utaratibu huu. Kama utadumu na kama utakuwa huru(kunawezwa wekwa mamluki wa kuuliza maswali;hakuna linaloshindikana karne hii),naamini ni njia nzuri ya Rais kuwasiliana na wananchi na japo kujua kwa mbali,yanayowakera.Hongera JK! Bado tu kufungua blog na account za twitter,facebook na myspace.Watanzania wengi sana siku hizi wanatumia zana hizo za mawasiliano.Obama yeye anazo zote tayari.
Pamoja na sifa hizo,kuna kitu ambacho kinanifanya nigune kidogo.Kwanini Mheshimiwa Rais amesubiri mpaka umebakia mwaka mmoja kabla ya uchaguzi ndio aanzishe utaratibu huu?Nia ni kusikia kweli hoja na maswali ya wananchi au ndio “kujiweka sawa” kabla ya uchaguzi?
Nini maoni yako kuhusiana na utaratibu huu mpya wa Rais Kikwete?Na je kama uliangalia zoezi zima la hotuba,maswali na majibu,unasemaje?Unampa alama gani Mheshimiwa Rais?A,B,C,D au…?
Kama lipo jambo ambalo liliamsha hisia tofauti kwenye ulingo wa siasa,basi ni tamko au kitendo cha mwanasiasa kijana,Zitto Kabwe,kutangaza nia ya kugombea uenyekiti wa Chama Cha Demokrasia na Maendeleo(CHADEMA)
Zitto Kabwe ambaye hivi sasa anashikilia nafasi ya Naibu Katibu Mkuu katika chama hicho,anasema pamoja na kwamba anaamini na kuafiki kwamba Mwenyekiti wa sasa wa chama hicho,Freeman Mbowe,ni kiongozi mzuri na kwamba amekitoa mbali chama hicho,wakati umefika wa kuwa na mabadiliko.Zitto anasema chama kimetawaliwa na “kufukuzana” uanachama. Jambo hilo lazima lifikie kikomo,anasema Zitto.
Kisha anasema lazima CHADEMA kijiandae kuchukua dola. Kwa maana hiyo labda tunaweza kusema Zitto anamaanisha kwamba CHADEMA ilivyo hivi sasa,hakiwezi au hakistahili kushika dola.Kinahitaji maandalizi!Hapa ni muhimu kukumbuka kwamba uchaguzi mkuu ni 2010 na sio 2011 au 2012.
Kama utakumbuka,miezi kadhaa iliyopita Zitto Kabwe alitangaza nia yake ya kutogombea tena nafasi ya Ubunge wa Kigoma Kaskazini anayoishikilia.Alisema anataka kujikita zaidi kwenye taaluma yake na hivyo kuachana kidogo na mambo ya siasa.Sasa tunajua kwamba hakuwa akimaanisha alichokuwa anakisema.Alijivika uhalisi wa siasa.
Je unasemaje kuhusiana na uamuzi wa Zitto Kabwe kutaka kugombea nafasi ya Uenyekiti wa CHADEMA?Unadhani atakuwa ni nahodha bora wa chama hicho cha upinzani zaidi ya Mwenyekiti aliyepo madarakani hivi sasa?
***Niliwahi kufanya mahojiano na Zitto Kabwe takribani miaka miwili iliyopita.Bonyeza hapa usome mahojiano yale ili pengine upate picha zaidi juu ya Zitto Kabwe.

