
Kwa faida ya msomaji ambaye, kwa sababu moja au nyingine hawezi kuwatambua waliopo pichani; Kutoka kushoto ni Kenneth Kaunda,maarufu kama KK(Rais wa Zambia kuanzia mwaka 1964 mpaka 1991),Julius Kambarage Nyerere(Baba wa Taifa la Tanzania na Rais wake kuanzia mwaka 1964 mpaka 1985),Jomo Kenyatta(Rais wa Kenya kuanzia mwaka 1964 mpaka 1978.),Milton Obotte (Rais wa Uganda kuanzia mwaka 1966 mpaka 1971 na kisha mwaka 1980 mpaka 1985)
Je,wewe binafsi unajifunza au umejifunza nini katika kufuatilia jinsi walivyoendesha maisha yao,utumishi wao kwa umma nk? Unadhani kuna yepi ya msingi ambayo sisi kama wananchi na pia viongozi wetu wa hivi sasa tunaweza kujifunza kutoka kwa watu hao?Kumbuka mazuri na mabaya yao kwani kama tulivyo sote,they were not perfect,no one is!
Habari kubwa iliyopo kurasa za mbele za vyombo vya habari ulimwenguni hivi leo ni kuhusu hotuba ya Rais wa Marekani,Barack Obama hapo jana usiku.Wenyewe wanaiita State Of The Union. Kama hukuiona,unaweza kuitazama hotuba nzima katika video hiyo hapo chini.
Kwa mtazamo wangu hotuba hii ni nzuri na ambayo viongozi mbalimbali duniani(hata katika nchi zetu za Afrika) wanaweza pia kuitumia kama kioo katika uongozi wao.Kuna mahali Obama alisema ukishachaguliwa kuwa kiongozi basi ufanye kweli kazi ya kuongoza(leadership) na kutengeneza kesho ya kizazi kijacho(next generation) na sio tu kwa sababu unataka kushinda uchaguzi ujao(next election). Alitia pia msisitizo wa kukumbuka kwamba upo hapo ulipo kwa sababu waliokutangulia,waliandaa mazingira mazuri kwa ajili yako.Bravo Obama!

Rais wa Zanzibar Dr Karume ametangaza kutogombea tena uraisi katika uchaguzi ujao mwakani kwa kuwa katiba ya Zanzibar haimruhusu yeye kufanya hivyo.
Raisi ameyasema hayo hapo jana kwenye hotuba yake Kwenye sherehe za Miaka 46 ya Mapinduzi Zanzibar zilizofanyika kwenye viwanja vya Gombani Pemba ambazo zilihudhuriwa na na viongozi mbalimbali wa chama na serikali akiwemo Rais Jakaya Mrisho Kikwete,Rais Mstaafu Benjamini William Mkapa,Rais Mstaafu Mzee Alhaj Hassan Mwinyi,Waziri Mkuu Mheshimiwa Mizengo Pinda,Waziri Mkuu Mstaafu Edward Lowassa,Mwenyekiti wa Chama cha Wananchi Cuf Sheif Sharrif Hamad pamoja na Lipumba,Waziri Kiongozi wa serikali ya mapinduzi Zanzibar Mheshimiwa Nahodha na Wakuu wa Majeshi na vyombo vingine vya Ulinzi na Usalama.
Je unadhani nini itakuwa ni hatma ya Chama Cha Mapinduzi huko Zanzibar? Wakati wa CUF umewadia?Nani atamrithi Karume?
Source: Charaz
Leo ni mwaka mpya.Hongera kwa kuiona 2010.Kama ilivyo ada au desturi,mwaka mpya huenda sambamba na salamu kutoka kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Ni salamu kutoka kwa Jakaya Mrisho Kikwete.
Ninachoweza kukuambia ni kwamba,hizi huwa sio salamu tu bali mwelekeo mzima wa nchi. Kama unataka kujua tulipo,tulipotoka na tunapoelekea,basi huna budi kuzisoma salamu za Mheshimiwa Rais. Sio lazima uzisome zote kwa mkupuo.Unaweza kusoma taratibu kifungu baada ya kifungu. Kila la kheri.
SALAMU ZA MWAKA MPYA ZA RAIS WA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA, MHESHIMIWA JAKAYA MRISHO KIKWETE, KWA WATANZANIA,
TAREHE 31 DESEMBA, 2009
Utangulizi
Ndugu Wananchi;
Kama ilivyo ada naomba nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutujaalia uhai na kutuwezesha kufika siku ya leo ya kuuaga mwaka 2009 na kuukaribisha mwaka 2010. Wapo wenzetu wengi tulioanza nao mwaka lakini hawakujaaliwa kuwa nasi siku hii ya leo kwa kuwa wametutangulia mbele ya haki. Tunamuomba Mwenyezi Mungu awape mapumziko mema. Kwa wenzetu wanaougua tuwaombee awape nafuu ya haraka ili waendelee kutoa mchango wao katika maendeleo yao, jamii zao na taifa zima kwa jumla. Aidha, tuendelee kuomba rehema za Mola wetu atujaalie afya njema na umri mrefu ili tuweze kuushuhudia mwaka wote wa 2010 na miaka mingine mingi ijayo.
Ndugu Wananchi;
Kama wote mlivyosikia, leo, siku ya mwisho ya mwaka 2009, Taifa letu lilipata msiba mkubwa wa kuondokewa na Mzee wetu, Mzee Rashid Mfaume Kawawa, Makamu wa Rais na Waziri Mkuu Mstaafu.
Kama nilivyoeleza wakati nalitangazia taifa kifo chake, huu ni msiba mkubwa kwa Taifa letu. Tumepoteza mmoja wa viongozi mashuhuri. Marehemu alijitoa muhanga kupigania uhuru na maendeleo ya nchi yetu. Wakati wote wa uhai wake alitumia uwezo wake na vipaji vyake alivyojaaliwa na Mola wake kujenga, kuendeleza na kutetea maslahi ya Taifa lake na Chama chake CCM na TANU kabla yake. Mzee Kawawa alikuwa mhimili mkubwa kwa Taifa letu na Chama cha Mapinduzi hata baada ya kustaafu uongozi. Sote tutaendelea kumkumbuka kwa moyo wake wa ubinadamu na mchango wake usiokuwa na kifani kwa nchi yetu na watu wake. Tuendelee kumuombea kwa Mwenyezi Mungu ailaze roho yake mahali pema peponi. Amin.
Nchi Salama na Tulivu
Ndugu Wananchi,
Ni jambo la faraja na kuonea fahari kwamba tunaumaliza mwaka 2009 taifa letu likiwa salama na kwamba amani na utulivu viliendelea kutawala. Aidha, taifa letu limeendelea kuwa moja na watu wake wameendelea kuwa wamoja, licha ya kuwepo kwa changamoto za hapa na pale zilizotokana na harakati za vyama vya siasa na kauli za baadhi ya wanasiasa na viongozi wa kijamii wakiwemo wale wa dini. (more…)

Zimebaki siku chache tuumalize mwaka 2009 na kuingia mwaka 2010 ambao kwa mujibu wa katiba ya nchi yetu,ni mwaka wa kupiga kura ili kumchagua tena mtu atayeongoza jahazi la nchi yetu kwa miaka mingine mitano.Tunauita mchakato huo “demokrasia”.
Tunapoelekea kwenye mwaka wa uchaguzi,tayari vibweka vya wanasiasa vimeshaanza kujitokeza.Nimesahau sio wanasiasa tu,hata wanajimu kama kina Sheikh Yahya.Wanasiasa wameanza kujitokeza na kumkingia kifua Rais aliyepo madarakani,Jakaya Mrisho Kikwete. Hawataki aguswe.Hawataki kusikia mtu anasema Kikwete alitoa “ahadi hewa” aliponadi sera ya maisha bora kwa kila mtanzania. Alijua haiwezekani lakini hakujali.Akajivika ngozi ya ukweli ya uanasiasa.Longolongo.Mageuzi huhitaji muda ati!
Miongoni mwa wanasiasa waliojitokeza ni Augustine Lyatonga Mrema. Anasema kama watu wanataka kumpinga JK basi waanzishe vyama vya siasa ili wawe wapinzani.Huna haki ya kumpinga Rais kama hujavaa kofia ya upinzani! Kuwa mwananchi,mzalendo,msema kweli na mpenda maendeleo haitoshi.Anzisha chama.
Mrema anatumia mbinu ya utaratibu.Anasema kama upo ndani ya CCM na unataka kumkosoa Rais,basi fuata utaratibu wa vikao vya chama na sio hadharani.Vikao vya chama huwa vinafanyika in closed doors! Kwa Mrema,hiyo ndio demokrasia ya kweli.Hajali kitu kinachoitwa Uhuru wa Habari na Uhuru wa Kujielezea.
Huyu ndie mpinzani ambaye huenda akawania Urais hapo mwakani!Ni Mwenyekiti wa chama cha upinzani cha Tanzania Labor Party(TLP).Watabiri wa masuala ya siasa wanasema Mrema keshakwisha kisiasa.Sasa anatapatapa.Ujumbe wangu kwa Mrema ni kwamba Mzee hatuendi hivyo.Wacha watu waseme,wajielezee.Kama JK kakosea,lazima aambiwe.
DAVID Kafulila, mwanachama mpya wa NCCR-Mageuzi, ambaye amekuwa akitumia uhusiano wake binafsi na Mbunge wa Kigoma Kaskazini, Kabwe Zitto, kama kete ya kisiasa katika ugomvi wake na uongozi wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), amesema Zitto ni mzushi.
Kafulila, ambaye alikuwa Ofisa Habari wa CHADEMA kabla hajavuliwa cheo hicho na kukimbilia NCCR-Mageuzi, alisema hayo jana Dar es Salaam, wakati akijibu taarifa kuwa mbunge huyo amekanusha kumsaidia magari matatu ya kufanyia harakati za kujijenga kisiasa mkoani Kigoma baada ya kujiunga na NCCR-Mageuzi.
Msukumo wa Kafulila kumshutumu Zitto umetokana na tetesi kwamba amekuwa anatumia barua pepe ya mbunge huyo kusambaza taarifa zinazoleta chokochoko katika CHADEMA, kwa kuwa anajua neno siri la anuani ya barua pepe ya mbunge huyo ambaye amekuwa anamtumia kama msaidizi wake katika masuala mengi walipokuwa CHADEMA.Bonyeza hapa kwa habari kamili.
Ingawa yeye mwenyewe amejitahidi kuwa kimya tangu alipomaliza muda wake wa Urais kwa mujibu wa Katiba ya Jamhuri ya Muungano ya Tanzania,jina lake limeendelea kuongoza vichwa vya habari mara kwa mara.Kwa bahati mbaya,amekuwa akitajwa kwa mambo ambayo hayapendezi au kutarajiwa kwa kiongozi mstaafu wa nchi inayoimba vita vya umasikini kama Tanzania.Tunamzungumzia Rais Mstaafu wa Awamu ya Tatu,Benjamin William Mkapa.
Amekuwa akitajwa na kuhusishwa na matumizi mabaya ya madaraka na kufanya biashara akiwa Ikulu mahali ambapo Baba wa Taifa,Hayati Mwalimu Julius Kambarage Nyerere(mwezi huu tunakumbuka kifo chake) alionya kwamba pale sio mahali pa kufanya biashara wala kujipatia utajiri.Baadhi ya Mawaziri wa serikali yake(nakumbuka alipoingia aliwaita “askari wa miamvuli”) tayari wameshafikishwa mahakamani wakikabiliwa na tuhuma mbalimbali nzito za matumizi mabaya ya madaraka na ufisadi kitu ambacho kinazua maswali kama vile,kwanini yeye bado na ikiwa ni msafi,alikuwa wapi wakati mawaziri wake wakitumia vibaya madaraka?
Wiki hii,jina lake limetawala tena vyombo vya habari.Kuna wanaosema wakati umefika sasa kwa Rais Mkapa kufikishwa mahakamani ili “akajisafishe” mwenyewe kwa tuhuma mbalimbali ambazo zimekuwa zikimkabili na kuna ambao(hususani viongozi wa serikali inayotawala-CCM) wanaosema kwamba Mkapa alikuwa kiongozi muadilifu na hivyo hana sababu za kufikishwa mahakamani ukizingatia pia kwamba,kama Rais mstaafu,anayo kinga ya kisheria na kikatiba ya kutokufikishwa mahakamani kwa mambo/hujuma ambazo zilitokea wakati akiwa madarakani.Baadhi ya viongozi wa vyama vya upinzani kama Dr.Slaa wanasisitiza sio tu kwamba ni lazima Mkapa afikishwe mahakamani kujibu tuhuma bali pia anatoa ufafanuzi wa kikatiba kwamba kinga inayosemekana anayo Mkapa,haipo kikatiba.
Kwa mujibu wa maelezo ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais anayeshughulikia Utawala Bora,Sophia Simba,sasa kuna shinikizo kubwa kutoka nje ya nchi(bila shaka kutoka kwa nchi wahisani) linalotaka Rais Mkapa ashitakiwe.
Je,nini maoni na mtazamo wako?Rais mstaafu Benjamin William Mkapa afikishwe mahakamani ili apate kujibu shutuma mbalimbali ambazo zinaelekezwa kwake?Kama kuna kipengele cha katiba ambacho kinamkingia kifua, je wakati umefika kwa kipengele hicho kurekebishwa?
Photo/Ayoub Mzee
Mojawapo ya mambo ambayo viongozi mbalimbali wa dunia hupenda kufanya wanapokutana ni kupiga picha.Katika nchi za magharibi kitu hicho huitwa Photo Opps au photo opportunity.Picha moja ni sawa na maneno elfu moja.Viongozi hulitambua hilo.Huwa ni nafasi ya kuwaonyesha wananchi mambo mbalimbali kwa kutumia picha.Wanaposalimiana na kujitega kwa picha huku wakiwa wanatabasamu,mwananchi wa kawaida atatafsiri kitu hicho kama amani,upendo na urafiki miongoni mwa viongozi hao na hivyo inamaanisha kwamba nchi zao zipo katika urafiki fulani ambao una manufaa kwa nchi husika.Yaweza kuwa kweli na pia yaweza kuwa sio kweli.
Photo Opps ni masuala ya kihistoria.Yamekuwepo tangu enzi na enzi.Ni masuala ya kidiplomasia.Viongozi kushikana mikono(kwa ishara ya kusalimiana),kutabasamu huku wakiwa wameelekeza nyuso zao upande walipo wapiga picha,ni mambo yaliyozoeleka.
Tangu Rais wa Marekani,Barack Obama aweke historia ya kuwa Rais wa kwanza wa Marekani mwenye asili ya Afrika au mweusi na kutokana na jinsi yeye na mkewe Michelle Obama walivyoiteka dunia,hakuna kiongozi ambaye hutaka kubakia nyuma linapokuja suala la kupiga picha nao.Bila shaka utakumbuka jinsi viongozi wa G20 walivyokuwa wanahangaika kupiga picha na Obama kule nchini Ujerumani mapema mwaka huu.
Majuzi jijini New York na kule Pittsburgh hali ilikuwa ni hiyo hiyo.Viongozi wetu wa Afrika nao hawako nyuma katika suala la picha na kina Obama.Kina Obama nao bila shaka ni wapenzi wa masuala ya picha na kwa sababu wao ndio walikuwa wenyeji kidiplomasia iliwabidi.Hizi hapa ni baadhi ya picha wakiwa na viongozi mbalimbali wa Afrika akiwemo Rais wetu,Jakaya Mrisho Kikwete.

Rais Kikwete (katikati) akiwa na Rais Obama(kulia) na US First Lady,Michelle Obama.Bila shaka picha hii ingependeza zaidi kama Mama Salma Kikwete angekuwepo.Mtizamo binafsi.

Kutoka kulia kwenda kushoto,Rais Barack Obama,Waziri Mkuu wa Kenya,Raila Odinga,US First Lady,Michelle Obama na mke wa PM Odinga,Mama Ida Raila Odinga.

Kutoka kulia kwenda kushoto,Rais Obama,Rais wa Uganda,Yoweri Kaguta Museveni,US First Lady,Michelle Obama na Ugandan First Lady,Janet Museveni

Kutoka kulia kwenda kushoto,Rais Obama,Rais Paul Biya wa Cameroon,US First Lady,Michelle Obama na First wa Cameroon,Mrs.Chantal Biya.Tayari kumeshazuka maneno katika blogs mbalimbali hususani nchini Marekani kuhusu wig alilovaa Mrs.Chantal Biya.Soma hapa.
Kwa picha zaidi bonyeza hapa
Katika anga za siasa wiki hii tunayoimaliza,ilitawaliwa na viongozi wa dunia kupigana vijembe,kufanyiana dhihaka,kuonyesha hasira zao nk kupitia hotuba walizozitoa katika mkutano wa Baraza la Umoja wa Mataifa. Miongoni mwa wanasiasa hao,yawezekana kabisa kukawa hakuna mwanasiasa aliyeongelewa,kujadiliwa na kuzua mijadala mikali zaidi ya Rais wa Libya,Muammar Gaddafi kufuatia hotuba aliyoitoa katika mkutano wa Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa huko jijini New York. Ni kwa sababu hiyo ndio maana leo tunavuka mipaka katika ukurasa huu wa “Mwanasiasa wa Wiki” na kumweka Gaddafi.Rais wetu,Jakaya Mrisho Kikwete,naye alihudhuria kikao hicho na alihutubia.
Kwanini “Mwasiasa wa Wiki” hapa BC awe Kanali Gaddaffi? Sababu ni nyingi.Lakini kwa uchache,Muammar Gaddafi ni mwafrika.Hivi sasa anashikilia cheo cha Mwenyekiti wa Umoja wa Afrika.Kwa hiyo,kwa mapana na marefu,alikuwa akituwakilisha waafrika.Hii ilikuwa ni mara yake ya kwanza kuhutubia Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa na mara yake ya kwanza kutembelea/kufika Marekani.
Safari ya Gaddafi ya kuelekea New York ilikumbana na vikwazo vingi.Kwanza alikataliwa sehemu kadhaa kuweka hema lake ambalo amekuwa akisafiri nalo kila mahali anapokwenda.Huwa hafikii hotelini.Anachohitaji yeye ni sehemu ya kuwekeza hema lake.Ulinzi wake huwa ni wa ma-bodyguard wanawake watupu.Maandamano kadhaa kutoka jumuiya mbalimbali yakipinga Gaddafi kupewa ruhusa ya kuweka hema yalifanyika.”Hatumtaki katika mji wetu wala mtaa wetu” Gaddafi ni dikteta.Mabango kadhaa yaliweka wazi sababu za kumkatalia “mgeni”Ilibidi afikie katika “ofisi” ya kidiplomasia ya Libya.
Yote tisa.Kumi ni pale alipolikwaa jukwaa la Umoja wa Mataifa na kuanza kuhutubia.Gaddafi alihutubia muda mfupi tu baada ya Rais wa Marekani,Barack Obama, ambaye naye ilikuwa ni mara yake ya kwanza kuhutubia baraza hilo.Gaddafi alikuwa ametengewa dakika 15 za kuhutubia.Alihutubia kwa zaidi ya dakika 90! Wengine walidhani alikuwa akielekea kuweka rekodi ya dunia.Hakuweza kwani mpaka leo mtu ambaye anashikilia rekodi ya kuhutubia Baraza la Umoja wa Mataifa kwa muda mrefu zaidi ni aliyekuwa Rais wa Cuba,Fidel mwana wa Castro.Alihutubia kwa zaidi ya masaa manne(4).
Baada ya hotuba ya Gaddafi,swali kubwa lililobakia miongoni mwa wafuatiliaji wengi wa mambo ya siasa ni “What was he talking about?”. Wengi hawakumuelewa alipotaka,kwa mfano,uchunguzi wa kina ufanyike kutokana na vifo vya aliyekuwa Rais wa Marekani,John F.Keneddy na mwanaharakati maarufu Mchungaji Martin Luther King.Uchunguzi leo hii? Gaddafi alionekana kutokuwa na maandalizi ya kile alichotaka kukiongelea.Hili hata mimi nililiona.Alipanda na vipande chungu mbovu vya makaratasi na mara kadhaa alionekana kusahau alichotaka kusema au alikiandika kwenye kipande gani cha karatasi.Mara kadhaa alijichanganya hususani alipokuwa anaongelea homa ya mafua ya nguruwe ya Swine Flu.
Pamoja na “hitilafu” hizo,yapo mambo ya msingi ambayo Kanali Muammar Gaddafi aliyaongelea.Kwa mfano ni kweli kwamba nchi nyingi wanachama wa UN hivi leo,hazikuwa wanachama wakati umoja huo unaanzishwa.Kwa hiyo,kuna haja ya kuangalia upya muundo mzima wa umoja huo yakiwemo mambo kama vile kura ya Veto.Gaddafi pia aliongelea jinsi ambavyo madhumuni ya kuanzishwa kwa umoja huo yameshindwa.Alisema,kwa mfano,vita zaidi ya 65 vimetokea na vinaendelea kutokea huku umoja huo ambao ulianzishwa ili kuzuia kutokea kwa vitu kama vita,ukiangalia tu.Ukitaka kusoma hotuba na kusikiliza hotuba nzima ya Muammar Gaddafi,bonyeza hapa.
Je ulipata muda wa kuiangalia hotuba ya Gaddafi?Unasemaje kuhusu hotuba hiyo? Gaddafi alitoa uwakilishi ulioutegemea kwa bara la Afrika? Unakubaliana na wanaosema Gaddafi ni mzigo kwa bara la Afrika na sababu nyingine ya kudharauliwa?
Viongozi wengine waliohutubia na kuzua gumzo ni Rais wa Iran,Mahmoud Ahmadenijad ,Rais wa Zimbwabwe,Comrade Robert Gabriel Mugabe na kama kawaida Rais wa Venezuela Hugo Chavez aliyeanza kwa kuomba wasikilizaji wake wasije wakamrushia kiatu ikiwa ni dongo la moja kwa moja kwa Rais wa 43 wa Marekani,George Bush iliyembidi akwepe viatu vya mwandishi wa habari wa Iraq alipokuwa madarakani.
Kama umewahi kusoma kitabu maarufu cha mwandishi Shafi Adam Shafi kinachoitwa Kuli, bila shaka utakuwa unakumbuka sentensi iliyofunga kitabu kile. Alisema; Yana mwisho haya.Kuli ni mojawapo ya vitabu ambavyo mpaka hivi leo namshauri mtu yeyote ambaye hajawahi kukisoma kufanya hivyo.
Kumbukumbu ya kitabu hicho ilinijia wiki hii nilipokuwa namsikiliza Katibu Mkuu wa CUF,Maalim Seif Sharif Hamad, alipokuwa akiongea na waandishi wa habari pale Buguruni ambapo aliweka wazi kwamba endapo viongozi wa chama tawala wanataka na kweli wana nia ya kuona amani inaendelea kuwepo visiwani Zanzibar,basi hawana budi kubadili mienendo yao na hususani sera na utaratibu mzima wa wananchi kujiandikisha tayari kwa kuwa wapiga kura katika uchaguzi mkuu hapo mwakani.Maalim anasema CCM inafanya njama ovu za kuwazuia wananchi kujiandikisha.
Katika kupambana na njama hizo za kiovu,Maalim anawaasa wananchi wa visiwani kusimama imara ili kutetea haki zao za msingi. Kwa msemo huu Maalim ananikumbusha yule mwanaharakati wa nchini Marekani, Malcolm X, aliyewahi kuwaasa watu weusi kwa msemo wake maarufu wa :By any means necessary”.Tayari kumeripotiwa mapambano ya silaha za moto baina ya wananchi na vyombo vya dola.
Nakiri kwamba historia ya ndani ya visiwa hivyo imenipiga chenga.Bado naisoma. Lakini kwa juu juu inaelekea kwamba lipo kundi la watu fulani ambalo linaamini kwamba ni lazima libakie madarakani milele.Kundi hilo linaamini kwamba bila wao,hakuna uongozi.Bila wao, mambo mengi yatakwenda mrama. Hilo tumeshalishuhudia tangu mfumo wa vyama vingi ulipotinga.Kwanini kundi hilo linaamini linavyoamini? Jibu kwa sasa sina.Naendelea kufanya utafiti.Anayejua tafadhali anisaidie. Kama una pendekezo la kitabu cha kusoma, usisite.
Pamoja na hayo, kama Maalim Seif anaongelea suala la kuchukua silaha,kuweka begani na kuingia msituni na kisha kurejea juu ya vifaru,sikubaliani naye. Sijashuhudia bado mahali ambapo amani ya kweli ilipatikana kwa ubabe uliokithiri. Nafasi ya kuambiana ukweli,kuketi mezani bado ipo.Demokrasia ni suala linalochukua miaka mingi sana.Sisi bado ni wachanga sana.Tusitegemee miujiza au majibu ya siku moja au mbili.Tupande na kisha tuhakikishe mizizi imeota.Tusichoke kusema,kukosoa na kuambiana ukweli bila uoga.Kama anavyofanya Maalim Seif.Yana mwisho.

