
Mkurugenzi Mtendaji wa Global Publishers & General Enterprises Ltd na mjasiriamali, Bw. Eric Shigongo(pichani), anatarajiwa kuhutubia nchini Marekani katika Mkutano maalum ulioandaliwa na Watanzania waishio nchini humo (Diaspora Council of Tanzanians in America – DICOTA).
Katika mkutano huo unaotarajiwa kufanyika kwa muda wa siku nne kuanzia Julai 1, mwaka huu katika jiji la Minneapolis, Marriott Hotel, Minnesota, Rais wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, Mh. Aman Abeid Karume, amealikwa kuwa mgeni rasmi. Viongozi wengine watakaohudhuria mkutano huo ni pamoja na maofisa waandamizi na wafanyabishara wakubwa kutoka Serikali ya Tanzania na Marekani.
Aidha, Mwenyekiti Mtendaji wa makampuni ya IPP, Bw. Reginald Abraham Mengi, naye ni miongoni mwa wageni waalikwa wa mkutano huo ambao unafanyika kwa mara ya pili nchini humo ukiwakutanisha Watanzania waishio ughaibuni. Mada mbalimbali zitatolewa na Watanzania waishio ndani na nje ya Marekani.
Katika mkutano huo, Bw. Shigongo anatarajiwa kutoa mada itakayoelezea jinsi ya kufanikiwa kiuchumi katika mazingira ya Tanzania na anatarajiwa kuwahamasisha Watanzania waishio ughaibuni kuwekeza nyumbani Tanzania.
Katika siku za hivi karibuni, Bw. Shigongo amejipatia umaarufu kwa kutoa elimu, ushauri kwa vijana na wanafunzi wa shule za msingi, sekondari na vyuo vikuu nchini kupitia mikutano na hafla mbalimbali anazoandaa au kualikwa kwa lengo la kutoa elimu ya ujasiriamali kwa vijana wa kitanzania.
Kwa taarifa zaidi juu ya mkutano huo tafadhali tembelea ukurasa wa Diaspora Council of Tanzanians in America-DICOTA)
Ninapoandika post hii,Afrika Kusini wapo uwanjani wakimenyana na Mexico.Wanaongoza goli 1-0.
Kwa bahati mbaya,Mzee Madiba ameshindwa kuhudhuria ufunguzi wa fainali hizo kutokana na kifo cha kitukuu wake,Zenani Mandela,kilichotokea jana usiku kwa ajali ya gari.

(AP Photo/Nelson Mandela Foundation, Debbie Yazbek)
Pichani juu ni Mandela na wajukuu zake.Kutoka kushoto ni Thembela Mandela,Zenani Mandela(aliyefariki) na Mbuso Mandela.
Unaweze kutizama video kidogo ya Mandela na kitukuu wake aliyefariki kwa kubonyeza hapa.
UPDATE: Mchezo kati ya South Africa na Mexico umekwisha.Matokeo ni 1-1. Goli la South Africa lilifungwa na Siphiwe Tshabalala kunako dakika ya 55.Mexico walisawazisha kunako dakika ya kwa goli rahisi lililofungwa na Rafael Marquez kunako dakika 79.

Katika hali ambayo bado sijaielewa,jana jioni nilikuwa nikijaribu kutengeneza orodha ya wanamuziki au miziki 100 maarufu ama kwa lugha nyingine, iliyotamba sana barani Afrika(Africa’s 100 Top Hit Songs). Nilichoamua kukifanya ni kujaribu kwenda(kwa kutumia mtandao) nchi moja mpaka nyingine huku nikijaribu kuchunguza kama nchi hiyo ina mwanamuziki au muziki ambao ulitokea kutamba zaidi barani Afrika.
Zoezi hilo bado naendelea nalo.Kwa hakika ni zoezi gumu hususani ukizingatia jinsi bara la Afrika lilivyosheheni vipaji na wasanii wa kiwango cha kimataifa.Nani aingie katika Top 100 na nani abakie nje.Mashabiki wake hawatonilalamikia kwanini nimemuweka pembeni mtu wao?Mawazo kama hayo yalitawala.
Wakati naendelea na zoezi hilo,nikawa pia napitiwa na huzuni kila nilipokuwa nasoma na huku nikisikiliza muziki kutoka kwa mwanamuziki fulani ambaye alishaiga dunia.Wapo wengi ila nazikumbuka hisia zangu nilipoyapitia majina kama Mbaraka Mwaruka Mwinshehe(Tanzania),Franco(DRC Congo),Madilu System(DRC Congo),Brenda Fassie(Afrika Kusini),Miriam Makeba(Afrika Kusini),Lucky Dube(Afrika Kusini),Fella Kuti(Nigeria) na kadhalika na kadhalika.
Nilipofika Gabon,jina ambalo bila shaka sote tunakubaliana kwamba ni vigumu(kama sio kashfa kabisa) kuliacha katika orodha ni jina la Oliver N’goma. Ni jana hiyo nilipojikuta nikisikiliza nyimbo kadhaa za Oliver N’goma kama vile Lusa,Bane,Betty,Nge’ Adia,Icole nk.Nikakumbuka sana jinsi nyimbo zake, zilivyotokea kuwa nyimbo ambazo haziwezi kukosa kunako shughuli mbalimbali hususani harusi hapa Bongo.Kwangu mimi Oliver alikuwa ni mfalme wa aina yake katika Zouk barani Afrika.
Unaweza kupata picha ya jinsi nilivyopata mshtuko na masikitiko kuamka asubuhi na kusikia kwamba Oliver N’goma amefariki dunia! Kwa mujibu wa vyombo mbalimbali vya habari, Oliver N’goma au Noli kama alivyojulikana huko kwao Gabon, amefariki kwa ugonjwa wa figo (kidney failure) akiwa hospitalini alikokuwa amelazwa.
Oliver alizaliwa tarehe 23 March mwaka 1959 katika mji unaoitwa Mayumba uliopo Kusini Magharibi mwa Gabon. Alizaliwa katika familia ambayo haikuwa ngeni katika masuala ya muziki. Baba yake alikuwa mpiga kinanda cha mdomo(harmonica) maarufu.Mwanzoni mwa maisha yake alipenda sana kuwa mpiga picha.Baadaye aliikacha taaluma hiyo na kuendelea na muziki kitu ambacho kilikuwa kwenye damu.
Mwishoni mwa miaka ya 80 ndipo alipotoa albamu yake iliyobeba jina Bane ambayo ndio ilikuwa chanzo cha umaarufu na mafanikio makubwa katika safari yake ya muziki.Rest In Peace Oliver N’goma.
Wimbo wake nilioupenda zaidi ni Bane’.

Aliyekuwa Makamu wa Rais wa Marekani,Al Gore,ametangaza kutengana na mke wake, Mary Elizabeth “Tipper” Gore, baada ya miaka 40 ya ndoa!
Kwa mujibu wa barua pepe waliyowatumia marafiki zao na baadaye kuthibitishwa na msemaji mkuu wa Al-Gore,Kalee Kreider, wanandoa hao ambao wiki kama mbili zilizopita walisheherekea miaka 40 ya ndoa yao,kwa pamoja wamesema wamefikia uamuzi wa kuifikisha mwisho ndoa yao baada ya mlolongo mrefu wa majadiliano baina yao.Hawakutoa maelezo zaidi na wameomba watu wote kuheshimu maamuzi na faragha yao.
Al Gore, mshindi wa Tuzo ya Nobel,ambaye watu wengi wanaamini alipokwa ushindi wa kiti cha urais na George W.Bush mwaka 2000, alikutana na mkewe tangu wakiwa shule ya sekondari. Walioana tarehe 19,Mei mwaka 1970 huko Washington,DC. Wana watoto wanne wakubwa.
Ama kweli aliyesema kwamba ndoa sio mchezo wa kuigiza bila shaka alikuwa na mantiki.
Zimebaki takribani siku 15 kabla kipute cha kugombea Kombe la Dunia la Soka hakijaanza huko nchini Afrika Kusini au “bondeni” kama ambavyo wengine wanapaita.
Jumla ya timu 32 zinashiriki fainali za kombe la dunia la mwaka huu ambazo kwa mara ya kwanza kabisa,zinafanyikia barani Afrika. Wawakilishi wa bara la Afrika katika fainali za mwaka huu ni wenyeji Afrika Kusini, Nigeria, Ghana,Ivory Coast, Cameroon na Algeria.
Licha ya hii kuwa mara ya kwanza kwa nchi yeyote ya bara la Afrika kuwa mwenyeji wa mashindano hayo, hakuna timu ya Afrika iliyowahi kuchukua ubingwa au hata kufikia nusu fainali.Mafanikio ambayo bara la Afrika linajivunia nayo mpaka hivi leo ni kufikia hatua ya robo fainali ambapo Senegal(ilifika hatua ya robo-fainali mwaka 2002 kabla ya kutolewa na Uturuki kwa goli kwa 1-0) na Cameroon(mwaka 1990 ilifikia hatua ya robo fainali kabla ya kutolewa na Uingereza kwa jumla ya goli 3-2)
Wachambuzi mbalimbali wa soka hawaipi Afrika nafasi ya kufanya vyema japokuwa ni wenyeji kwa sababu mbalimbali kama vile kuwa katika makundi magumu;mfano hapa unatolewa kwa kundi G ambalo ndani yake kuna Ivory Coast,Brazil,Portugal na Korea Kaskazini. Wengi hawaipi Ivory Coast nafasi ya kuendelea raundi ya pili na kwa maana hiyo kuziacha ama timu za Brazil na Portugal ambazo zinapewa zaidi nafasi ya kusonga mbele.
Sababu zingine zinazotolewa ni ukosefu wa uzoefu(Ghana na Ivory Coast zinashiriki kwa mara ya pili wakati Algeria inashiriki kwa mara ya tatu baada ya kutofanya hivyo kwa muda mrefu)
Pamoja na hayo, kwa upande mwingine wale wanaozipa nafasi timu kutoka barani Africa wanajitia moyo wa ushindi kwa sababu ukweli ni kwamba bara la Afrika lina wachezaji lukuki katika ligi za Ulaya jambo ambalo linatuhahakishia kwamba timu za Afrika zilizofuzu zinao wachezaji wengi tu wenye ufundi na uzoefu(skills and experience) na mikikimikiki ya mashindano makubwa kama ya Kombe la Dunia.
Je, Africa tutacheka au tutaendelea kulia na kununa? Miongoni mwa timu hizi ambazo picha zake zipo hapo chini ni ipi ambayo unaishabikia? Ni ipi ambayo unaipa nafasi ya juu kufanya vyema zaidi kuliko zingine? Kwanini unaipa nafasi hiyo?

South Africa

Cameroon

Algeria

Ivory Coast

Ghana

Nigeria
Editor’s Note: World Cup 2010 ni tukio kubwa na la kipekee ambalo bila shaka litafuatiliwa na mabilioni ya watu ukiwemo wewe msomaji na mtembeleaji,msomaji na mchangiaji wetu.Kwa kutambua hilo,BC itakuwa,kwa msaada na ushirikiano wa wapenzi,wataalamu na wafuatiliaji wa soka,itakuwa ikikuletea chambuzi mbalimbali kuhusu fainali hizi.Asanteni
Rais wa Nigeria, Umaru Yar’Adua(pichani) amefariki dunia. Kwa mujibu wa vyombo mbalimbali vya habari likiwemo Shirika La Habari la Uingereza(BBC), Rais Yar’Adua amefariki dunia leo hii huko katika mji wa Abuja ambao ndio mjii wa Nigeria. Alikuwa na umri wa miaka 58.
Rais Yar’Adua amefariki dunia baada ya kuugua kwa muda mrefu hali iliyopelekea aliyekuwa makamu wake, Goodluck Jonathan kukabidhiwa madaraka na Bunge la nchi hiyo ili kunusuru mgogoro mkubwa wa kisiasa uliokuwa unanukia katika nchi hiyo ya Afrika Magharibi yenye watu wengi kupita zote barani Afrika. Nigeria ina jumla ya watu wanaokadiriwa kufikia milioni 150.
Rais huyo ambaye aliingia madarakani mwaka 2007 ndiye Rais pekee wa nchi hiyo ambaye aliweka wazi mali alizonazo pindi alipoingia madarakani ikiwa ni ishara ya uadilifu na upingaji wa ufisadi.
Mungu ailaze roho yake mahali pema peponi.Amin.
Posti hii nilitakiwa kuipandisha jana lakini sikufanikiwa maana jana nilifunga kiroho na kifikra ili kumkumbuka Malcom X, mpigania haki za watu weusi kule Marikani. Malcom X alizaliwa na kupewa jina la Malcom Little kisha akaamua kubadili “Little” na kuweka “X” kwa kile alichodai kuwa jina la awali lilikuwa ni la kikoloni na lenye nia ya kuiba utu wake. “X” inasimama kama “Aliyepotea/Asiye na Jina” ikimaanisha Mwafrika aliyepoteza utambulisho wake baada ya kutekwa na kupelekwa utumwani kule Marikani.
Nimeona niweke posti hii ili tuelewe kwamba isingekuwa Malcom X na wengine waliotangulia kama Martin Luther King Jr., Mama Rosa Parks, au mapambano ya kuwakomboa watumwa ya Reli ya Ardhini” (Undeground Railroad) yaliyoongozwa na mwanamke mweusi Harieth Turbman, pengine Marekani ya leo isingekuwa na Rais Mweusi tunayemfahamu na kumshabikia, Barack Obama.
Malcom X alizaliwa katika familia yenye maisha duni na akiwa na umri wa miaka 13, baba yake ambaye alikuwa mpigania haki za watu weusi pia aliuawa na wazungu wabaguzi waliojulikana kama Ku Klux Klan (KKK), na mama yake alikuwa amefungiwa katika hospitali ya wagonjwa wa akili. Hivyo Malcom akaanza maisha ya kujitegemea akitumia wizi wa mifukoni kama njia ya kujipatia kipato.
Mwaka 1946 Malcom alifungwa jela kutokana na wizi. Akiwa Jela, Malcom ambaye hakuwahi kusoma vitabu akajikuta akiwa msomaji mkubwa wa vitabu ambavyo vilimwongezea maarifa aliyokuja kuyatumia baadae katika mapambano dhidi ya ubaguzi wa watu weupe kwa watu weusi. (more…)

Miezi saba baadaye,aliyekuwa daktari wa Mfalme wa Muziki wa Pop ulimwenguni,Michael Jackson, Dr.Conrad Murray ameshtakiwa rasmi kwa kifo cha mwanamuziki huyo maarufu ambaye katika maisha yake,aligusa wengi.Michael Jackson alifariki dunia tarehe 25 June mwaka jana akiwa na umri wa miaka 50.
Kwa mujibu wa vyanzo mbalimbali vya habari, Dr.Murray ambaye alifikishwa mahakamani mchana huu huko Los Angeles,amekana shtaka lake na ameachiwa kwa dhamana ya dola 75,000. Kesi hiyo imepangwa kusikilizwa tena tarehe 5 April.
Ndugu wa Michael Jackson,kaka zake Jermaine,Tito,Jackie na Randy ,dada yake LaToya na wazazi wake Joe na Katherine walikuwepo mahakamani kusikiliza kesi hiyo.
Hapo kabla Dr.Conrad Murray ambaye ni mzaliwa wa nchini Grenada,alikiri kwa polisi kwamba alimchoma Michael Jackson sindano ya dawa aina ya Anaesthetic Propofol kwa dhumuni la kumsaidia bingwa huyo wa Pop kulala.Alisema aliporudi tena chumbani alimkuta Michael akiwa hapumui.
Mchunguzi wa vifo wa Los Angeles alithibitisha baadaye kwamba dawa hizo ndizo zilizosababisha kifo cha Michael Jackson. Dr.Murray alikuwa ameajiriwa maalum kwa ajili ya kumuandaa Michael Jackson katika tour iliyokuwa ijulikane kama This Is It ambayo ilikuwa ianzie nchini Uingereza.
Unapoongelea sinema,hakuna ubishi kwamba majadiliano yako inabidi yaanzie Hollywood.Na unapokuwa Hollywood na kuamua kuanzisha mjadala wa Tuzo(awards) basi yakupasa uanzie kwenye tuzo maarufu za Academy au Oscars.
Muda mchache uliopita majina ya sinema,waigizaji,waongoza sinema na vipengele vingine walioteuliwa kuwania tuzo hizo kwa mwaka huu yametangazwa. Kama ambavyo ilitarajiwa, sinema ya Avatar iliyoongozwa na James Cameron pamoja na sinema ya The Hurt Locker ambayo imeongozwa na Kathryn Bigelow(mke wa zamani wa James Cameron) ndio zimepata teuzi nyingi zaidi katika kuwania tuzo hizo maarufu ambazo zinafanyika kwa mara ya 82 (miaka 82). Movie hizo zimeteuliwa mara 9 au katika vipengele 9.
Shughuli za mwaka huu za tuzo hizo zinatarajiwa kufanyika tarehe 7 Mwezi Machi(takribani siku 33 zijazo).Zitaonyeshwa moja kwa moja(live) kupitia kituo cha televisheni cha ABC cha nchini Marekani.
Kwa orodha kamili ya Oscar Nominations kwa mwaka huu,bonyeza hapa. Je kuna movie,actor au actress ambaye ulitarajia angeteuliwa kuwania tuzo za mwaka huu ambaye hajatokea katika orodha?
Hatimaye Mfalme wa Pop,Michael Jackson,anatarajiwa kuzikwa leo huko Forest Lawn-Glendale,California katika makaburi yajulikanayo kama Holly Terrace.Mazishi yanatarajiwa kuanza saa moja usiku kwa saa za California.
Kwa mujibu wa taarifa kuhusu mazishi hayo,yatakuwa ni mazishi “private” na hivyo ni ndugu,jamaa na marafiki wa karibu pekee watakaoweza kuhudhuria.
Mazishi haya yanafuatia mlolongo wa matukio tangu alipofariki mwanamuziki huyo ikiwemo uchunguzi wa kipolisi kuhusiana na kifo chake na pia kupingana kwa ndugu na wanafamilia yake kuhusiana na swala la wapi azikwe. Mengine yaliyoibuka tangu afariki dunia ni pamoja na habari za matumizi mabaya ya madawa ya kutuliza maumivu na kulaza aliyokuwa nayo Michael Jackson.
Hivi karibuni Mchunguzi wa vifo wa California,alithibitisha kwamba Michael Jackson alifariki dunia kutokana na kuchomwa sindano ya kupunguza maumivu ambayo ilikuwa na dozi kubwa kuliko kawaida. Daktari aliyekuwa naye siku hiyo,Dr.Murray, ndiye anatupiwa lawama zote ingawa mpaka leo hakuna mashtaka rasmi kuhusiana na kifo cha mwanamuziki huyo.
Pumzika Salama Michael.

