
Mojawapo ya majina yaliyovuma sana katika ulimwengu wa soka nchini Tanzania,hususani miaka ya themanini, ni lile la Ahmed Abdulthabit Amasha(pichani).Ahmed Amasha alikuwa ni beki wa kutumainiwa wa timu ya Yanga ya jijini Dar-es-salaam. Mwaka 1984 Amasha alichaguliwa kuwa Mchezaji Bora wa Mwaka.Hivi sasa anafundisha soka huko Oman akiwa kocha wa timu ya Seeb SC.
Picha kwa hisani ya Mroki.

Hapo zamani kulikuwa na majina kama Athumani Mambosasa, Juma Pondamali,Joseph Fungo,Sahau Kambi, Iddi Pazi, Mohamed Mwameja na wengineo. Hao wote walikuwa ni walinda milango (makipa) waliojizolea sifa kemkem kutokana na umahiri wao katika kuzilinda nyavu zao zisitikiswe na timu pinzani.
Hivi sasa, huku watanzania wakiwa wamepata upya mwamko wa kupenda soka na kuunga mkono timu za nyumbani(hususani Taifa Stars), tunaye Tanzania One,Ivo Mapunda (pichani). Huyu ndiye kipa nambari moja wa timu ya taifa ya soka kwa upande wa wanaume,Taifa Stars na pia klabu maarufu na kongwe ya Yanga ya jijini Dar-es-salaam. Ameshatwaa tuzo ya Mchezaji Bora wa mwaka nchini Tanzania mara mbili. Ushauri kwa Ivo Mapunda?

Wote kwa pamoja, kama unavyowaona pichani ni celebrities. Majina yao hivi sasa ndio yametawala vinywa vya wapenda michezo, watanzania kwa ujumla. Wengine wamediriki hata kusema “utaifa” uko mabegani mwao hivi sasa.
Jumamosi hii kuanzia saa tatu usiku, timu yetu ya taifa ya soka ambayo inajulikana kwa jina lisilo rasmi la JK Boys, watateremka dimbani kukabiliana na majirani zetu kwa upande wa kusini, Msumbiji, katika mchezo muhimu wa mwisho katika kuwania tiketi ya kucheza katika fainali za mataifa ya Afrika 2008 zitakazofanyikia nchini Ghana mwakani. Mchezo huo utafanyikia katika uwanja wa taifa mpya na wa kisasa wenye uwezo wa kuchukua mashabiki 60,000.
Mara ya mwisho Taifa Stars ilishiriki katika fainali za mataifa ya Afrika mwaka 1980 zilizofanyikia nchini Nigeria. Je vijana wetu watatutoa kimasomaso hiyo jumamosi? BongoCelebrity inaungana na watanzania wote popote walipo, kuitakia kila la kheri timu yetu ya taifa. Go Go Taifa Stars!

