MY TANZANIA   |   PLACES TO GO   |   MEDIA   |   ONLINE ENTERTAINMENT    

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Jakaya Kikwete amemteua Balozi Francis Malambugi(pichani) kuwa Balozi mpya wa Tanzania nchini Brazil .

Uteuzi wa Balozi Malambugi umetokana na na kuteuliwa hivi karibuni kwa aliyekuwa Balozi wa nchi hiyo Balozi Daktari Joram Mkama Biswaro kuwa Balozi wa Tanzania nchini Ethiopia na kwenye Umoja wa Afrika.

Balozi Malambugi ambaye kwa taaluma ni Mwanasheria na Mwanadiplomasia alijiunga na Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa tarehe 1/1/1978 kama Wakili wa Serikali na amewahi kufanyakazi katika Ubalozi wa Tanzania nchini Angola, Ofisi ya Umoja wa Mataifa iliyoko Geneva, Ujerumani,Ethiopia na Ubelgiji.

Mara ya kwanza tuliwasiliana mwaka jana.Akanieleza mipango yake,ndoto zake na mikakati aliyonayo katika kutimiza ndoto zake.Kama ilivyokuwa kwa mamilioni ya watu ulimwenguni, Babu Sinare ambaye kisanii anajulikana kwa jina la Albino Fulani, alikerwa na kuhuzunishwa na mauaji ya watu wenye ulemavu wa ngozi(albino) kwa imani za kishirikina. Kwake yeye,ilikuwa ni kama vile wametonesha kidonda ambacho alidhani kilishapona kwani Babu Sikare ni albino pia.

Miongoni mwa mipango yake ilikuwa ni pamoja na kuanzisha NGO yake ambayo italenga kusaidia albino wengine.Kupitia muziki wake,aliahidi kwamba atazidi kukemea mauaji ya albino.Hakuwa anatania.Alianzisha shirika lisilo la kiserikali na kuliita Afro-Bino. Matunda ya shirika hilo yameanza kuonekana.

Pichani juu ni Babu Sikare(kushoto) akimkabidhi Mkurugenzi wa Huduma za Hospitali kutoka Wizara ya Afya, Dr. Magreth Mhando (kulia) karatasi yenye maelekezo ya msaada wa mafuta ya kuzuia ngozi isiharibike na jua kwa ajili ya watoto wenye ulemavu wa ngozi Tanzania (Albino) yenye thamani ya dolla 1,500. Katikati ni Kaimu Mkurugenzi Idara ya Ustawi wa Jamii Bi. Magreth Njimba.

Kutoka moyoni,naomba kumpongeza Babu Sinare na shirika zima la Afro-Bino.We salute you and we support you.

Albino Fulani anatamba pia na wimbo wake Barua Kwa Mama.Bonyeza hapa kuusikia.


Mrema

Zimebaki siku chache tuumalize mwaka 2009 na kuingia mwaka 2010 ambao kwa mujibu wa katiba ya nchi yetu,ni mwaka wa kupiga kura ili kumchagua tena mtu atayeongoza jahazi la nchi yetu kwa miaka mingine mitano.Tunauita mchakato huo “demokrasia”.

Tunapoelekea kwenye mwaka wa uchaguzi,tayari vibweka vya wanasiasa vimeshaanza kujitokeza.Nimesahau sio wanasiasa tu,hata wanajimu kama kina Sheikh Yahya.Wanasiasa wameanza kujitokeza na kumkingia kifua Rais aliyepo madarakani,Jakaya Mrisho Kikwete. Hawataki aguswe.Hawataki kusikia mtu anasema Kikwete alitoa “ahadi hewa” aliponadi sera ya maisha bora kwa kila mtanzania. Alijua haiwezekani lakini hakujali.Akajivika ngozi ya ukweli ya uanasiasa.Longolongo.Mageuzi huhitaji muda ati!

Miongoni mwa wanasiasa waliojitokeza ni Augustine Lyatonga Mrema. Anasema kama watu wanataka kumpinga JK basi waanzishe vyama vya siasa ili wawe wapinzani.Huna haki ya kumpinga Rais kama hujavaa kofia ya upinzani! Kuwa mwananchi,mzalendo,msema kweli na mpenda maendeleo haitoshi.Anzisha chama.

Mrema anatumia mbinu ya utaratibu.Anasema kama upo ndani ya CCM na unataka kumkosoa Rais,basi fuata utaratibu wa vikao vya chama na sio hadharani.Vikao vya chama huwa vinafanyika in closed doors! Kwa Mrema,hiyo ndio demokrasia ya kweli.Hajali kitu kinachoitwa Uhuru wa Habari na Uhuru wa Kujielezea.

Huyu ndie mpinzani ambaye huenda akawania Urais hapo mwakani!Ni Mwenyekiti wa chama cha upinzani cha Tanzania Labor Party(TLP).Watabiri wa masuala ya siasa wanasema Mrema keshakwisha kisiasa.Sasa anatapatapa.Ujumbe wangu kwa Mrema ni kwamba Mzee hatuendi hivyo.Wacha watu waseme,wajielezee.Kama JK kakosea,lazima aambiwe.

KikweteJK

Kesho ni 9 Desemba.Bila shaka unaelewa umuhimu wa siku hiyo kwa nchi yetu.Kama historia ya nchi imekupitia kushoto,naomba nikukumbushe.Ni siku ya kukumbuka siku mkoloni alipoamua kukubali yaishe na kuirudisha nchi kwa wenye nchi yaani wananchi.Uhuru.

Sitaki kuhesabu ni miaka mingapi imepita tangu mwenge ule ulipopandishwa kileleni Kilimanjaro.Nina sababu zangu.

Wakati wa kumbukumbu kama hizi za Uhuru,kinachoendelea ni hotuba,ahadi za uongo na kweli na mambo kama hayo.Tunatakiana kheri pia.Kwa kipi?Sina uhakika.Hapo ndipo katika pitapita yangu mtandaoni,kwenye wavuti na blogs mbalimbali,nikakutana na ya Mubelwa akiwa pale Laurel,MD nchini Marekani.Yeye anasema,wakati anawatakia watanzania wote kila la kheri katika kusheherekea miaka— ya Uhuru,ana maswali 10 kwenda kwa Rais Jakaya Mrisho Kikwete.Bonyeza hapa uyasome.

Mubelwa,sidhani kama atajibu.Hulka hiyo bado haipo.Ninachoweza kukuhakikishia ni kwamba atayasoma.Kama sio yeye basi “miongoni mwao”.

KabweDAVID Kafulila, mwanachama mpya wa NCCR-Mageuzi, ambaye amekuwa akitumia uhusiano wake binafsi na Mbunge wa Kigoma Kaskazini, Kabwe Zitto, kama kete ya kisiasa katika ugomvi wake na uongozi wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), amesema Zitto ni mzushi.

Kafulila, ambaye alikuwa Ofisa Habari wa CHADEMA kabla hajavuliwa cheo hicho na kukimbilia NCCR-Mageuzi, alisema hayo jana Dar es Salaam, wakati akijibu taarifa kuwa mbunge huyo amekanusha kumsaidia magari matatu ya kufanyia harakati za kujijenga kisiasa mkoani Kigoma baada ya kujiunga na NCCR-Mageuzi.

Msukumo wa Kafulila kumshutumu Zitto umetokana na tetesi kwamba amekuwa anatumia barua pepe ya mbunge huyo kusambaza taarifa zinazoleta chokochoko katika CHADEMA, kwa kuwa anajua neno siri la anuani ya barua pepe ya mbunge huyo ambaye amekuwa anamtumia kama msaidizi wake katika masuala mengi walipokuwa CHADEMA.Bonyeza hapa kwa habari kamili.

Machupa-FrontBC

Machupa ni mfungaji hodari. Usemi huo pekee unatosha kumuelezea Athuman Iddi Machupa (pichani) mshambuliaji kijana ambaye kwa upande wa Tanzania, aliwika zaidi alipokuwa akichezea timu ya soka ya Simba maarufu kama “Watoto wa Msimbazi”.

Hivi leo Machupa anasakata kabumbu nchini Sweden akiwa na timu ya Vasalund IF.

Niliwasiliana na Machupa hivi karibuni na kumuuliza maswali machache. Haya hapa mahojiano yetu;

BC: Mpaka sasa mambo yanakwendaje hapo Sweden?Unachezea timu gani na ipo daraja la ngapi?

Machupa: Kwa upande wangu hapa Sweden maisha yanakwenda poa kaka.Ninachezea timu inayoitwa Vasalund IF ilikuwa katika ligi ya Superettan (ligi ya pili kwa ukubwa hapa Sweden) lakini kwa bahati mbaya tumeshuka daraja hadi la kwanza..

BC: Umeshakaa Sweden kwa muda wa kutosha sasa.Unapaonaje na zaidi unaonaje nafasi za kuendeleza soka lako?

Machupa: Kwa sasa kaka napeleka mwaka hapa na kwa upande wangu mi naona maisha ni mazuri na hata nafasi ya kusonga mbele kwangu ni kubwa mno.Nazidisha bidii katika kila kitu na inshallah nitafanikiwa zaidi na zaidi.


BC: Kama mgeni katika nchi ya watu,ni mambo gani ambayo ilibidi ukabiliane nayo kwanza? Hapa nazungumzia mambo kama vile lugha,vyakula nk

Machupa: Of coz lugha kaka ni ngumu. Lakini nashukuru jamaa wamenishughulikia masuala yote ya muhimu ikiwa ni pamoja sehemu ya kujifunza lugha yao.Na kuhusu chakula; kwa kusema ukweli ni kizuri tu. Hakina tofauti sana na cha nyumbani Tanzania kwa sababu najipikia mwenyewe chakula ninachojisikia kula.Hali ya hewa nayo ilikuwa changamoto lakini taratibu ninazoea.

Machupa-Jikoni“Hebu ngoja nicheki kama vitu vishaiva”

BC: Una ujumbe gani kwa vijana wengine wanaosakata soka nyumbani Tanzania?

Machupa: Ujumbe wangu kwa vijana wanaosakata soka na hususani waliopo nyumbani ni kwamba waheshimu soka kwani soka ni kazi kama zilivyo kazi zingine zozote.Ukiheshimu soka hakika utafanikiwa.

BC: Mwakani ni mwaka wa kombe la dunia.Safari hii kipute kipo Africa.Nini matarajio yako kwa nchi za Afrika?

Machupa: Ni changamoto kubwa kwa timu za Africa ambazo zimefanikiwa kuingia katika finali hizo. Tusubiri tuone kwa sababu nina uhakika watajiandaa vizuri. Nina uhakika hatutosikia madai ya posho. Nina imani watatuwakilisha vyema kabisa,sina wasiwasi na hilo. Ila nahisi Ghana watafanya vizuri. Nawa-support.

Machupa-ZoeziniMachupa akiwa mazoezini na timu yake.Anaonekana kulia katika picha akijaribu kutuliza mpira chini.

BC: Una lolote la kuongeza kwa mashabiki wako?

Machupa: Mashabiki ndio kila kitu.Nawapenda na ninawaheshimu sana na hakika bila wao hatuwezi songa kwa sababu wao ndio wanaotukosoa pale tunapokosea.I love all my fans popote walipo.

mkapaIngawa yeye mwenyewe amejitahidi kuwa kimya tangu alipomaliza muda wake wa Urais kwa mujibu wa Katiba ya Jamhuri ya Muungano ya Tanzania,jina lake limeendelea kuongoza vichwa vya habari mara kwa mara.Kwa bahati mbaya,amekuwa akitajwa kwa mambo ambayo hayapendezi au kutarajiwa kwa kiongozi mstaafu wa nchi inayoimba vita vya umasikini kama Tanzania.Tunamzungumzia Rais Mstaafu wa Awamu ya Tatu,Benjamin William Mkapa.

Amekuwa akitajwa na kuhusishwa na matumizi mabaya ya madaraka na kufanya biashara akiwa Ikulu mahali ambapo Baba wa Taifa,Hayati Mwalimu Julius Kambarage Nyerere(mwezi huu tunakumbuka kifo chake) alionya kwamba pale sio mahali pa kufanya biashara wala kujipatia utajiri.Baadhi ya Mawaziri wa serikali yake(nakumbuka alipoingia aliwaita “askari wa miamvuli”) tayari wameshafikishwa mahakamani wakikabiliwa na tuhuma mbalimbali nzito za matumizi mabaya ya madaraka na ufisadi kitu ambacho kinazua maswali kama vile,kwanini yeye bado na ikiwa ni msafi,alikuwa wapi wakati mawaziri wake wakitumia vibaya madaraka?

Wiki hii,jina lake limetawala tena vyombo vya habari.Kuna wanaosema wakati umefika sasa kwa Rais Mkapa kufikishwa mahakamani ili “akajisafishe” mwenyewe kwa tuhuma mbalimbali ambazo zimekuwa zikimkabili na kuna ambao(hususani viongozi wa serikali inayotawala-CCM) wanaosema kwamba Mkapa alikuwa kiongozi muadilifu na hivyo hana sababu za kufikishwa mahakamani ukizingatia pia kwamba,kama Rais mstaafu,anayo kinga ya kisheria na kikatiba ya kutokufikishwa mahakamani kwa mambo/hujuma ambazo zilitokea wakati akiwa madarakani.Baadhi ya viongozi wa vyama vya upinzani kama Dr.Slaa wanasisitiza sio tu kwamba ni lazima Mkapa afikishwe mahakamani kujibu tuhuma bali pia anatoa ufafanuzi wa kikatiba kwamba kinga inayosemekana anayo Mkapa,haipo kikatiba.

Kwa mujibu wa maelezo ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais anayeshughulikia Utawala Bora,Sophia Simba,sasa kuna shinikizo kubwa kutoka nje ya nchi(bila shaka kutoka kwa nchi wahisani) linalotaka Rais Mkapa ashitakiwe.

Je,nini maoni na mtazamo wako?Rais mstaafu Benjamin William Mkapa afikishwe mahakamani ili apate kujibu shutuma mbalimbali ambazo zinaelekezwa kwake?Kama kuna kipengele cha katiba ambacho kinamkingia kifua, je wakati umefika kwa kipengele hicho kurekebishwa?

Photo/Ayoub Mzee

tz-leadersbc

Nimeshawahi kusema na leo nitarudia tena; Kama umekosa kabisa jambo au mambo yanayokufanya ujisikie furaha kuwa Mtanzania,basi angalau unaweza kupata ahueni unapoangalia jinsi ambavyo “demokrasia” ya nchi yetu imekuwa mfano wa kuigwa barani Afrika na hata sehemu mbalimbali za ulimwengu.Of course demokrasia yetu ina mapungufu mengi bado lakini ipi ambayo haina?Marekani au?

Mpaka leo,tangu Nyerere ang’atuke,hajatokea mtu akasema anataka kubadili katiba ili aendelee kutawala.Muda ukiisha mtu anaachia madaraka. Lakini kuachia madaraka haitoshi.Lipo suala zima la kuachia madaraka na pia kuendelea kushiriki katika shughuli mbalimbali za kitaifa na hata kimataifa kwa jina la Tanzania. Hali hii ni lazima ilindwe kwani ni wazi kwamba haitokei kama ajali.

Pichani ni Marais wetu,wastaafu Ally Hassan Mwinyi(mwisho kulia),Benjamini William Mkapa(mwisho kushoto) na Rais aliyepo madarakani hivi sasa,Jakaya Mrisho Kikwete(katikati). Kama unavyoona pichani wapo na wake zao au kina mama zetu wa kwanza waliostaafu na aliyepo kwenye uskani hivi sasa.

Sijui kama ni mimi tu ndio nimeona hili au vipi lakini nadhani mpangilio kidogo wa picha hii ulikwenda kombo.Sijui kwanini Mama Anna Mkapa ilibidi awe mbali vile na Mzee na pia Mama Sitti Mwinyi.Sijui.

Picha kwa hisani ya Bodi ya Utalii Tanzania

mamaz

Unaweza kuiponda Tanzania kwa mambo mengi. Lakini jambo moja ambalo huna budi kutupa ni kwamba kuna uvumilivu wa hali ya juu. Tunavumiliana.

↑ Go Back to Top of Page