MY TANZANIA   |   PLACES TO GO   |   MEDIA   |   ONLINE ENTERTAINMENT    

Jina la Madaraka Nyerere(pichani) sio geni miongoni mwa watanzania.Ukiachilia mbali ukweli kwamba yeye ni mtoto wa sita wa Hayati Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Kambarage Nyerere (kitu ambacho bila shaka kinampa automatic celebrity status), yeye pia ni mwandishi,mfanyabiashara na mtu ambaye huwa hasiti kuelezea hisia zake kuhusu mambo mbalimbali iwe ni katika nyanja za kisiasa,kijamii na hata kiuchumi kila mara fursa ya kufanya hivyo inapojitokeza.

Mwaka jana mwezi wa nne(April) yeye na Jaffar Amin(mtoto wa Iddi Amin-Rais wa zamani wa Uganda) waliingia katika vitabu vya kumbukumbu vya wapenda amani duniani walipokutana kwa mara ya kwanza ikiwa ni ishara ya amani na usuluhisho barani Afrika na kwingineko.

Hivi karibuni nilipata nafasi ya kuzungumza naye kuhusu mambo kadhaa yakiwemo ya kifamilia na pia kupata maoni yake kuhusu mambo mbalimbali.Je,ni kwanini mpaka leo hii hajajiingiza katika masuala ya siasa au uongozi?Anamuelezeaje Hayati Baba wa Taifa kama baba yake na kama kiongozi?Ana ushauri gani kwa wapiga kura katika mwaka huu wa uchaguzi? Ana mtizamo gani kuhusu viongozi mbalimbali ambao hupenda kumuenzi Baba wa Taifa kwa maneno huku vitendo vyao vikiwa tofauti kabisa? Unataka kujua kwanini alipewa jina la “Madaraka”? Ana ushauri gani kwa vijana kuhusu suala zima la kujiletea maendeleo? Fuatana nasi katika mahojiano yafuatayo;

BC: Madaraka,asante sana kwa kukubali kufanya nami mahojiano haya. Kwa faida ya wale ambao hawawajui watoto wa Hayati Baba wa Taifa,Mwalimu Nyerere,nyumbani kwenu mmezaliwa watoto wangapi na wewe ulizaliwa lini,ukasomea wapi na kukulia wapi?

MADARAKA NYERERE: Tuko watoto nane. Mimi wa sita. Nimesoma shule

zifuatazo:

-Shule za msingi: Bunge, Forodhani, Arusha School, Isike (Tabora), Tarime.

-Sekondari: Mzizima, na Tambaza (Dar)

-Post-secondary: Shinyanga Commercial Institute

-Vyuo: Finafrica College (Milan, Italy); Algonquin College (Ottawa, Canada)

BC: Turudishe kidogo wakati wa utoto wako.Ni kitu au tukio gani unalolikumbuka zaidi kuhusu utoto wako?Na ulikuwa na ndoto za kufanya kazi gani utakapokua?

MADARAKA NYERERE: Sina tukio lolote kubwa ninalokumbuka la utotoni. Nahisi baada ya kuanza masomo ya biashara kuanzia kidato cha tatu, tayari nilianza kuwa na mawazo ya kuwa mfanyabiashara. Kabla ya hapo, sikumbuki kama nilikuwa na ndoto za kufanya kazi nyingine.

BC: Uliwahi kuelezwa kwanini ulipozaliwa ulipewa jina la Madaraka?Ilikuwaje kukua kama mtoto wa Rais au katika mazingira ya Ikulu na mambo kama hayo? (more…)

Miezi michache iliyopita, Rais Jakaya Kikwete, alifanya mabadiliko na teuzi kadhaa za mabalozi wetu katika nchi mbalimbali. Miongoni mwa mabadiliko hayo ni pamoja na yale ya kumhamisha Balozi Peter A.Kallaghe kutoka nchini Canada kwenda kuwa Balozi mpya wa Tanzania nchini Uingereza.

Wakati akijiandaa kuondoka nchini Canada kuelekea katika kituo chake kipya cha kazi nchini Uingereza,BC ilipata nafasi ya kufanya naye mahojiano maalum utakayoyasoma hivi punde.

Balozi Peter Kallaghe anaelekea nchini Uingereza kuchukua nafasi iliyoachwa na Balozi Mwanaidi Maajar ambaye amehamishiwa nchini Marekani. Fuatana nasi katika mahojiano haya;

BC: Mheshimiwa Balozi,asante sana kwa kukubali kufanya nami mahojiano haya.Nafahamu kwamba una mambo mengi mengine ya kufanya hususan wakati huu unapojiandaa kuondoka hapa Canada.Kwa hiyo nashukuru sana kwa kunipatia fursa hii.

Kwa kuanzia na kwa sababu wewe ni Balozi wa kwanza kufanya nasi mahojiano,ningependa kukuuliza swali ambalo bila shaka lipo katika vichwa vya wasomaji na wafuatiliaji wetu.Ilikuwaje mpaka ukafikia hatua ya kuteuliwa kuwa Balozi?Katika historia yako ya utumishi wa umma(Public Service) umepitia ngazi zipi,milima na mabonde yapi?Hapa ninamaanisha ulisomea wapi,ukakulia wapi na nini kilikusukuma katika ajira ya serikalini au utumishi wa umma kwa ujumla?

Balozi Peter Kallaghe: Historia yangu kielimu ni kwamba nimehama hama sana shule, kwa sababu baba yangu, Marehemu Balozi Cecil A. Kallaghe, alikuwa mtumishi wa umma na alipata kufanya kazi nje ya nchi kama Balozi.

Kwa ufupi nilisoma elimu ya msingi katika shule za OysterBay na Arusha School katika miaka ya sitini. Na nilipata elimu ya sekondari katika shule ya Pugu Secondary School. Chuo Kikuu nilisomea Kieve State University ambapo nilihitimu na degree ya M.A. in International Relations. Aidha nina Post-Graduate Diploma kwenye Diplomacy, Negotiatiations and Strategic Communications.

Kikazi maisha yangu yote nimefanya kazi katika Wizara ya Mambo ya Nje na Ikulu, hususani kama msaidizi wa Rais kwa kipindi kirefu.

Niliteuliwa Balozi kwa mara ya kwanza mwaka 2004 nikiwa pale Ikulu, na mwaka 2007 niliteuliwa Balozi nchini Canada. Mwaka 2010 nimeteuliwa kuwa Balozi wa Tanzania nchini Uingereza (UK).

Kuteuliwa kwangu kuwa balozi nakuchukulia kama fursa ya kipekee niliyopewa ya kutoa mchango wangu katika kulitumikia Taifa letu la Tanzania na watu wake. Na ninafanya hivyo nikitambua uzito wa dhamana hii hasa kwa nchi ambayo bado inakabiliana na changamoto nyingi za kimaendeleo.

BC: Sasa kama sikosei hii ilikuwa ni mara yako ya kwanza kuteuliwa kuwa Balozi kamili. Je,ulikuwa na matarajio gani kabla hujafunga safari kuja Canada? Je, ulichokitarajia ndicho ulichokutana nacho? (more…)

Jina la Sauda Mwilima (pichani)sio geni miongoni mwa watanzania wengi hususani wapenzi wa vipindi mbalimbali vya televisheni.Yeye ni mtangazaji kupitia Kituo Cha Televisheni cha Star kinachomilikiwa na kampuni ya Sahara Communications sambamba na vituo vya radio vya Kiss FM na Radio Free Africa.Vipindi anavyoruka navyo hewani ni Bongo Beats na Mcheza Kwao.

Hivi karibuni BC ilipata nafasi ya kufanya naye mahojiano utakayoyasoma hivi punde.Je unajua Sauda anapendelea kuvaa namna gani anapotoka?Kuna mahali maalumu anapopenda kununulia “viwalo” vyake? Ana ushauri gani kwa vijana wengine ambao wangependa kuja kufanya kazi ya utangazaji kama yeye? Fuatana nasi katika mahojiano yafuatayo;

BC: Sauda,asante sana kwa kukubali kufanya nami mahojiano haya…mambo vipi?

SM: Mambo fresh tu.Nashukuru Mungu,siku zinakwenda.

BC: Kwa kuanza na kwa faida ya wasomaji wetu,unaweza kuniambia ulizaliwa lini,wapi,ukakulia wapi na mambo kama hayo?

SM: Nilizaliwa miaka 30 iliyopita,hapa hapa jijini Dar-es-salaam katika hospitali ya Rufaa ya Muhimbili.Baadaye tulihamia Dodoma ambapo niliishi mpaka nilipomaliza elimu ya msingi ambapo nilirudi jijini Dar-es-salaam.Mpaka sasa maisha yanaendelea hapa hapa jijini Dar.

BC: Ilikuwaje ukaamua kufanya kazi ya utangazaji wa televisheni?Unaweza kukumbuka siku yako ya kwanza uliporekodi au kurusha kipindi cha televisheni “live”?

SM: Wakati nipo sekondari, ndoto yangu kubwa ilikuwa nikimaliza shule niwe Mwanasheria au Mwandishi wa Habari.Lakini baada ya kumaliza shule nikaangukia kwenye mambo ya habari. Na kikubwa zaidi nilivutiwa katika kazi ya utangazaji na dada yangu, Saida Mwilima, ambaye alikuwa mtangazaj TVT(Televisheni ya Taifa) ambayo kwa sasa inajulikana kama Tanzania Broadcasting Corporation (TBC). Nilivutiwa sana na kazi aliyokuwa akiifanya sister kwa sababu ni mtu ambaye nilikuwa naishi naye kipindi nasoma.Wakati huo yeye tayari alikuwa mtangazaji.

Yeah nakumbuka kipindi cha kwanza kwenda hewani ilikuwa mwishoni mwa mwaka 2004.Katika kipindi hicho niliwahoji AY,Ray C,Stara Thomas,Banana Zorro na Ruge Mutahaba. Hicho kilikuwa kipindi kimoja ambacho tulikuwa tunajadili kuhusu wasanii wa Kiume kuwapa support wa kike.Ruge nilimhoji katika nafasi ya Promoter anayechangia kukua kwa muziki.Hicho ndicho kilikuwa kipindi changu cha kwanza.

BC: Tuambie kidogo kuhusu kipindi chako pale Star TV.Maandalizi ya kipindi huwa yakoje na kwa mtu ambaye hajawahi kuangalia kipindi chako,nini maudhui ya kipindi?

SM: Star Tv nina vipindi viwili ambavyo nafanya kwa sasa. Cha kwanza kinaitwa Bongo Beats na cha pili kinaitwa Mcheza Kwao. Miaka miwili iliyopita niliwahi kufanya kipindi cha Afya.

Maandalizi ya kipindi ni kwamba kabla sijakutana na msanii husika kwanza huwa nafanya research(utafiti) kumhusu yeye kwa kutumia vyanzo mbalimbali. Kutokana na ninachokuwa nimepata kutoka kwenye utafiti,ndio naandaa maswali yangu. Kinachofuata baada ya hapo ni miadi ya kukutana katika location kwa ajili ya mahojiano. Kipindi cha Bongo Beats kinaruka hewani kila siku kasoro Jumapili tu. (more…)

Pamoja na kwamba inasemekana kampeni za uchaguzi hazijaanza rasmi au hazitakiwi kuwa zimeanza,ukweli ni kwamba kwa namna moja au nyingine,kampeni zimeshaanza.Huu ni ukweli ambao Tume ya Uchaguzi lazima waukubali ili marekebisho yafanyike endapo wanataka kuwa makini zaidi katika kuhakikisha kwamba vyama vyote na wagombea wote wanasubiri mpaka tarehe 20 Augosti siku ambayo ndio kampeni rasmi zinatakiwa kuanza.

Tunathubutu kusema hivyo kwa sababu tayari tumesikia mara kadhaa viongozi/wagombea mbalimbali wakijinadi kwamba wamefanya nini katika miaka mitano iliyopita na wanatarajia kufanya nini endapo wananchi watawapa tena dhamana ya kuongoza nchi kwa miaka mingine mitano.

Pia tumeshasikia tambo mbalimbali kutoka kwa wanaowania kuunda serikali mpya,wakijinadi kuhusu watakachokifanya tofauti endapo “ngekewa” ya kuwaongoza watanzania itawaangukia wao.Sasa kama tambo hizo sio sehemu ya kampeni,sijui Tume ya Uchaguzi ina tafsiri ipi kuhusu maana ya “kampeni”.

Bila shaka,baada ya kuwasikia wagombea mbalimbali wakijinadi na kutokana na uzoefu wako na jinsi unavyofuatilia shughuli mbalimbali za kisiasa,umeshafanya maamuzi(japo katika fikra tu) kwamba pindi itakapofika mwezi Octoba,kura yako utampa mgombea fulani.Ndio maana tunauliza;Uchaguzi Ungefanyika Leo,Ungemchagua Nani?Kwanini? Wanaogombea nafasi ya Urais kutoka vyama mbalimbali,hawa hapa:

Civic United Front(CUF): Professor Ibrahim Haruna Lipumba(kulia) na mgombea mwenza,Juma Duni Haji.

Chama Cha Mapinduzi(CCM):Jakaya Mrisho Kikwete na Mgombea Mwenza,Dr.Gharib Bilal.

Chama Cha Demokrasia na Maendeleo(CHADEMA) :D r.Wilbrod Slaa akisalimiana na Mgombea Mwenza,Hamisi Mzee Hamisi.

National Convention for Construction and Reform-Mageuzi(NCCR-Mageuzi)-Hashim Rungwe(kushoto) na Mgombea Mwenza,Ali Juma.

Miongoni mwa mambo ambayo yanatia moyo nchini kwetu ni pamoja na kuendelea kukua kwa tasnia ya filamu kama ambavyo tumekuwa tukishuhudia. Ukuaji huo unakwenda sambamba na kuona kwamba,siku baada ya siku, wapenzi wa filamu za “nyumbani” wanazidi kuongezeka na kwa maana hiyo industry nzima ya filamu inazidi kukua.

Lakini uungwaji mkono huo haukuja bure tu. Umetokana na tabia nzuri ambayo wasanii wengi wa sanaa hiyo wameionyesha.Wamekubali kukosolewa na kusikiliza maoni ya wadau mbalimbali wa masuala ya filamu na kuyafanyia kazi ipasavyo.

Miongoni mwa wasanii hao ni pamoja na Steven Kanumba ambaye bila shaka sote tunakubaliana kwamba kila kukicha ameonyesha kuwa na bidii kubwa kabisa katika kuboresha kazi zake na uigizaji wake kwa ujumla.

Mwezi ujao(August),Kanumba anatarajia kuendelea kuthibitisha jinsi anavyozidi kukomaa katika sanaa hiyo,itakapotoka filamu ambayo imepewa jina Crazy Love(Part 1 & 2). Kwa mujibu wake yeye mwenyewe kupitia blog yake,ili kuweza kuigiza katika filamu hiyo,ilimbidi kusoma vitabu mbalimbali vya wanafalsafa mashuhuri ulimwenguni kama vile Plato,Karl Max,Alexander The Great,Samuel Taylor nk ili kuelewa zaidi mambo yanayohusu tabia za binadamu,falsafa nk.

Je usomaji huo ulimsaidiaje Kanumba katika Crazy Love?Usikose kununua makala halisi ya filamu hiyo pindi itakapoingia sokoni mwezi ujao.

Photos Courtesy:Kanumba.

Kama jana ulipata muda kutizama Tuzo za Kituo cha Televisheni cha BET cha nchini Marekani(BET Awards 2010),bila shaka ulisikia jina la Tanzania likitajwa kama mara mbili au tatu hivi.

Tanzania haikutajwa kwa sababu wasanii wake walikuwemo katika kuwania tuzo hizo.La.Tanzania ilitajwa kwa sababu Mwanamuziki John Legend(pichani) alipokea BET Humanitarian Award kutokana na kazi mbalimbali za kusaidia jamii anazozifanya na hususani nchini Tanzania.

Kupitia mradi wake ujulikanao kama Show Me Campaign,John Legend amekuwa akiingia na kutoka nchini Tanzania kila mara katika kutembelea na kusimamia miradi mbalimbali. Mojawapo ya miradi aliyonayo nchini Tanzania ni pamoja na ile anayoifanya katika kijiji kiitwacho Mbola kilichoko Uyui mkoani Tabora.Unaweza kusoma zaidi kuhusu miradi hiyo kwa kubonyeza hapa. Kama inawezekana,tafadhali muunge mkono.Unaweza fanya hivyo kwa kubonyeza hapa.

Bila shaka utakubaliana nasi kwamba hatuna budi kuwashukuru watu kama hawa kwa jinsi wanavyojitolea katika kuwasaidia ndugu,jamaa na wananchi wenzetu.

Thank You John Legend.We appreciate all you are doing for Mbola and for Tanzania.

Photo/AP

Mwanaidi Hassan,akilia kilio cha furaha na kutoamini alipotangazwa kuwa Mwanamichezo Bora nchini Tanzania kwa mwaka uliopita wa 2009.Mwanaidi anacheza mchezo wa Netball.Anachezea timu ya JKT Mbweni na Timu ya Taifa ya Netball.Utoaji wa tuzo hizo ulifanyikia New Africa Hotel jijini Dar-es-salaam.

Mwanaidi Hassan(katikati) akikabidhiwa Tuzo ya Uanamichezo Bora na kitita cha shilingi Milioni Moja(1m Tshs).Anayemkabidhi ni Mwenyekiti wa Baraza la Michezo Tanzania(BMT),Kanali Iddi Kipingu.Wanaoshuhudia pembeni,kutoka kulia kwenda kushoto ni David Nyombo,aliyechukua Ushindi wa Tatu kupitia mchezo wa kunyanyua vyuma vizito(body building),Juma Kaseja,aliyechukua ushindi wa pili kupitia mchezo wa Soka.Kaseja ni golikipa wa Simba Sports Club ya jijini Dar-es-salaam.Mwingine pichani ni Mwenyekiti wa Chama Cha Waandishi wa Habari za Michezo(TASWA),Boniface Wambura.TASWA ndio waandaji wa tuzo hizo.

Juma Kaseja(kulia) akipokea Tuzo ya ushindi wa pili.Kaseja, golikipa nambari moja wa Simba.Anayemkabidhi ni Jaji Mark Bomani,Mwenyekiti wa Bodi wa Kampuni ya Serengeti ambao ndio wadhamini wakuu wa tuzo hizo.

David Nyombo,mnyanyua vyuma vizito,akikabidhiwa tuzo yake ya ushindi wa tatu.

Washindi wakiwa katika picha ya pamoja na wadhamini na wadau wa TASWA.

Picha zote na Richard Mwaikenda.

Wakati suala zima la nani alileta mradi wa Zinduka nchini Tanzania,nani alianzisha idea hiyo na mchakato mzima wa mradi huo likiendelea,nadhani sio vibaya kama tukajionea kile ambacho wasanii waliweza kufanya.

Kimsingi,kampeni hii ina umuhimu wa aina yake.Malaria ni tishio la uhai wa mamilioni ya watu ulimwenguni.Inaua kuliko ugonjwa mwingine wowote.Inaua zaidi ya Ukimwi!Kuna haja ya kuendelea kusambaza ujumbe.Kuna haja ya kuendelea kupeana maarifa kuhusu jinsi ya kupambana na ugonjwa wa malaria.Mapambano dhidi ya ugonjwa wa malaria ni zaidi ya chandarua.Ni suala la mazingira.Vidimbwi vya maji yaliyotuama.Misitu ya majani inayoachwa bila matunzo.Ni pamoja na kutumia kila aina ya kinga zilizopo.Hongera kwa wasanii waliotengeneza na kushiriki katika video hii;Zinduka. Kwa msaada zaidi wa jinsi ya kupambana na malaria,bonyeza hapa.

You need to a flashplayer enabled browser to view this YouTube video

Rais wa Zanzibar Dr Karume ametangaza kutogombea tena uraisi katika uchaguzi ujao mwakani kwa kuwa katiba ya Zanzibar haimruhusu yeye kufanya hivyo.

Raisi ameyasema hayo hapo jana kwenye hotuba yake Kwenye sherehe za Miaka 46 ya Mapinduzi Zanzibar zilizofanyika kwenye viwanja vya Gombani Pemba ambazo zilihudhuriwa na na viongozi mbalimbali wa chama na serikali akiwemo Rais Jakaya Mrisho Kikwete,Rais Mstaafu Benjamini William Mkapa,Rais Mstaafu Mzee Alhaj Hassan Mwinyi,Waziri Mkuu Mheshimiwa Mizengo Pinda,Waziri Mkuu Mstaafu Edward Lowassa,Mwenyekiti wa Chama cha Wananchi Cuf Sheif Sharrif Hamad pamoja na Lipumba,Waziri Kiongozi wa serikali ya mapinduzi Zanzibar Mheshimiwa Nahodha na Wakuu wa Majeshi na vyombo vingine vya Ulinzi na Usalama.

Je unadhani nini itakuwa ni hatma ya Chama Cha Mapinduzi huko Zanzibar? Wakati wa CUF umewadia?Nani atamrithi Karume?

Source: Charaz

salma

Msomaji na mtembeleaji wetu mmoja,ameomba tumwekee hapa picha ya karibu(close-up) ya First Lady wetu,Mama Salma Kikwete.Msomaji huyo anasema tangu picha za Marais na viongozi wa nchi mbalimbali wakiwa na Rais wa Marekani Obama na mkewe Michelle Obama zitokee katika vyombo mbalimbali vya habari amekuwa akipata tabu na marafiki zake ambao wamekuwa wakimhangaisha kutaka kumuona First Lady wa Tanzania.Mama Salma Kikwete hakuwepo katika picha zile za viongozi mbalimbali na kina Obama.Msomaji/mtembeleaji wa BC,hiyo hapo juu ni picha ya karibu ya Our First Lady,Mama Salma Kikwete.

Read the Next Page →

↑ Go Back to Top of Page