Vijana wengi tumeshapitia au tunapitia kwenye kipindi kigumu sana maishani. Nina uhakika wengi wetu tumeshawahi kukosa usingizi wakati tupo kitandani na kubaki tu kuangalia dari na kujiuliza maswali mengi sana; nitafanya nini maishani? Mustakabali wa maisha yangu ni upi? Nitakuwa wapi baada ya miaka miwili, mitano au hata kumi?

Bahati mbaya Watanzania hatuna hulka ya kujadili mambo kama haya kwa uwazi tukiwa na ndugu, jamaa na marafiki zetu. Na matokeo yake (tunaonekana kama) hatujifunzi kutoka kwa wenzetu — hili suala ndilo linalonipa misongo kwenye mijadala mbalimbali. Kwahiyo, ni matumaini yangu kuwa nasaha zilizopo kwenye makala hii zitabadilisha fikra za angalau kijana mmoja na kutambua kuwa maisha yake ya baadae yako kwenye viganja vyake! Kwa maneno mengine, wewe msomaji ndio mwenye uwezo mkubwa wa kuamua maisha yako huko mbeleni yaweje.

Je, unajua una kipawa, kipaji au talanta ipi? Baada ya kumaliza elimu ya sekondari au chuo kikuu, ulikuwa au unajua unataka ufanye nini; uwe mtu wa aina gani kwenye jamii?

Kama unashindwa kujibu hayo maswali haraka na kwa ufasaha, usiogope na wala usitetereke. Hauko mwenyewe. Wengi tumeshapitia na tunaendelea kupitia kwenye kipindi ambacho fikra zetu zinakuwa zimejawa na mawazo ya utata. Lakini utakubaliana nami kuwa wenzetu ambao tayari wanajua wana vipaji fulani na kuvifanyia kazi, maisha yao huonekana marahisi machoni mwa wengi.

Amini usiamini, majibu ya maswali mengi hupatikana hapa — kwenye tovuti ya Bongo Celebrity. Jeff na timu yake wamekuwa wanajitahidi kutuletea mahojiano murua ya watu maarufu wanaofanya vizuri Bongo kwenye nyanja mbalimbali, ili mimi na wewe tujifunze mawili matatu kutoka kwao na kutumia ‘maujanja’ kwenye maisha yetu; kukuza vipaji vyetu na kuviendeleza.

Jifunze kutoka kwa waliofanikiwa

Kwa mfano, Profesa Jay akihojiwa huwa anatoa nasaha nyingi sana ambazo binafsi naamini zinatakiwa kuhamasisha kila kijana anayezisikia kwa namna moja au nyingine. Cha kusikitisha read more

Miezi kadhaa iliyopita niliongelea jinsi ya kupata kazi. Niliongelea mambo kadhaa ya kufanya au kutokufanya endapo umeitwa kwenye usaili(interview).

Pia kama utakumbuka wiki kadhaa zilizopita niliandika kuhusu mambo ya kufanya ili kuepuka migogoro makazini.Ukijiepusha na migogoro utakuwa umefanikisha jambo moja muhimu; kulinda ajira yako. Kama hupatani na wafanyakazi wenzako na kila kukicha wakuu wako wa kazi wanashinda wakisuluhisha migogoro yako, ni wazi kwamba siku zako zinahesabika.Utaipoteza ajira.

Leo naomba kuendeleza kidogo jinsi ya kulinda ajira yako.Kumbuka nyakati tulizonazo kiuchumi ni ngumu.Kuwa na ajira(ukiwa na uwezo ushauri wangu ni kwamba;jiajiri mwenyewe) ni muhimu.Ufanyeje ili kulinda ajira uliyonao?Unaweza kuzingatia mambo yafuatayo;

  • Fanya kazi yako vizuri: Hili la kwanza linaweza kuwa wazi.Umeajiriwa kwa sababu mwajiri wako anahitaji msaada kutokana na ujuzi ulionao.Unategemewa kufanya kazi zako kwa juhudi na maarifa.

    Zingatia maelekezo,sera na kila kitu kinachohusiana na kazi yako.Timiza wajibu wako.Kama kazi yako inakwenda sambamba na vitu kama “deadlines”,hakikisha unafanikiwa ipasavyo katika hilo.

  • Punguza kulalamika: Pamoja na kwamba waajiri wengi wanasema kwamba wana sera huru zinazoruhusu wafanyakazi kuelezea kero zinazowakabili nk,ukweli ni kwamba waajiri hao hao hawapendi kuwa na mfanyakazi au wafanyakazi wanaolalamika kupita kiasi.

    Kila inapowezekana,jitahidi kutatua matatizo madogo madogo unayokumbana nayo kazini bila kukimbilia kwa “wakubwa” ukiwa na lundo la malalamiko. Endapo ni lazima kulalamika,fanya hivyo huku ukiwa na mapendekezo halisi ya jinsi ya kukabiliana na tatizo husika.

  • Kuwa na siasa zisizofungamana na upande wowote: Kila mtu ana utashi wake katika siasa za nchi.Na kwa vile mwaka huu ni mwaka wa uchaguzi,utashi wa kisiasa au vyama vya kisiasa unazidi.Pamoja hayo,hakikisha kwamba katika maeneo ya kazi,unakuwa au unaonyesha kuwa na siasa zisizofungamana na upande wowote.Kwa maneno mengine,usilete ofisini ushabiki wa kisiasa unaoonekana kuzidi mipaka au hata kuingilia utendaji wako.

    Lakini pia usionyeshe kwamba huelewi kinachoendelea nchini.Baadhi ya waajiri huutumia wakati huu kukagua watu wanaoelewa kuhusu sera mbalimbali za nchi,vyama vya kisiasa nk ili kujua nani au mfanyakazi yupi anastahili kushika usukani japo wa idara fulani.

    Kumbuka katika nchi nyingi zinazoendelea(Tanzania ikiwemo) mambo mengi(kama vile biashara na uwekezaji) yana uhusiano wa karibu sana na siasa za kiuchumi za nchi husika.Usikae kando sana. read more

Leo naomba nianze kwa shukrani kwa wote ambao mmeniandikia barua pepe,kuchangia kwa kupitia njia ya maoni aidha kupitia hapa hapa BC au kwenye ukurasa wa Facebook na hata wale ambao mmeweza kunipigia simu na kunitia moyo nisiache kuandika dondoo hizi za kusaidiana kwa kupeana maarifa mbalimbali. Inatia hamasa kuona kwamba unanisoma na zaidi unapata maarifa fulani fulani ya kuboresha maisha yako.Hiyo ndio nia yangu ya msingi.Tafadhali usisite kuniandikia.Ukiwa na swali pia usisite kuniuliza.Najibu asilimia 99.9% ya barua pepe zote zinazonijia.

Motisha au sababu ya kufanya jambo fulani(natumaini kwamba jambo hilo ni la manufaa) ndio msingi wa maendeleo ya kibinafsi na pia kijamii.Bila hamasa au motisha(motivation) ni hakika kwamba mambo mengi yangekuwa yamekwama.Dunia ya leo isingekuwa ilivyo endapo watendaji fulani fulani wasingekuwa na motisha ya kufanya mambo waliyoyafanya au wanayoyafanya.

Binadamu tunatofautiana.Kuna ambao wana motisha au hamasa zaidi kuliko wengine.Mara nyingi watu wa namna hiyo hufanikiwa maishani.Lipo kundi lingine ambalo kwa kawaida ni la watu ambao hawana motisha(not or less motivated).Hawaoni sababu yeyote ya kufanya kitu au jambo fulani.Wanahitaji kusukumwa sana,kubembelezwa,kupewa ahadi mbalimbali nk ndipo watashtuka waamke wakafanye jambo.Unaweza kuwaita wavivu ukipenda ingawa kuna tofauti kati ya mtu mvivu na yule ambaye amepoteza motisha.

Pamoja na hayo,sote hukamatwa na mtego wa kukosa au kupoteza motisha katika nyakati fulani.Unakuwa hujisikii kufanya chochote.Hutaki hata kufikiri kuhusu mbinu za kujiletea mabadiliko chanya.Unakuwa upo upo tu.Unatakiwa kwenda mazoezini lakini hujisikii.Unatakiwa kumaliza kusoma kitabu fulani lakini wapi.Unatakiwa kwenda kazini lakini motisha huna nk.Hiyo hunitokea hata mimi.Unaweza kufanya nini hali kama hiyo inapokutokea ili kurudisha motisha yako ya kawaida? Leo tutaangalia baadhi ya mambo ambayo unaweza kufanya;

  • Kuwa na Lengo Moja kwa wakati mmoja: Kupoteza au kutokuwa na motisha ya kufanya jambo fulani mara nyingi hutokana na kuwa na malengo mengi kichwani kwa wakati mmoja.Unataka kufanya mambo kumi kidogo.Matokeo yake ndio unapoteza muelekeo na hivyo motisha ya kufanya lolote.Unachotakiwa kufanya ni kuwa na lengo au dhumuni moja moja.Unapoipunguzia akili yako mambo ya kufikiri,itakusaidia kutimiza malengo uliyonayo.Kumbuka kufanya jambo moja kisha ndio urukie lingine.
  • Tafuta msukumo(insipiration): Ipo sababu inayokufanya utake kufanya unalotaka kulifanya.Kama wewe ni mwanafunzi basi bila shaka kuna mtu ambaye ungependa kuwa kama yeye katika siku za mbeleni.Kama wewe ni mwanamichezo basi sio ajabu kwamba yupo mwanamichezo fulani ambaye ungependa kufikia na hata kupita mafanikio yake.Kuna sababu katika kila kitu.Unachotakiwa kufanya ni;unapoona motisha inapotea,hamasa inapungua basi jipatie msukumo kwa kuangalia tena mafanikio ya mtu/watu au nchi unayoitamani.Unataka kujenga mwili kama aliokuwa nao Gavana wa sasa wa jimbo la California nchini Marekani (Arnold Schwaznegger) enzi alipokuwa Mr.Universe basi ni shurti ujitahidi na mazoezi. read more

Mafanikio maishani yana sura nyingi. Tunatofautiana katika maana nzima ya mafanikio.Unachokiona wewe kuwa ni cha mafanikio yawezekana jirani yako akakiona si mali kitu.

Pamoja na tofauti hizo za maana au matinki ya mafanikio,wengi tunakubaliana kwamba furaha na amani maishani ni miongoni mwa mafanikio au malengo muhimu sana ya binadamu. Kila mtu anataka kuishi maisha yaliyojaa furaha na amani.Ndio maana tunapokumbwa na vitu ambavyo kibinadamu havikaribii kabisa maana ya furaha na Amani,wengi wetu huangua vilio,kujuta,kulaumiana,kufarakana nk.Kila mtu anatamani kutokuwa na huzuni au masononeko mbalimbali moyoni.

Tunatofautiana pia katika mbinu za kujenga maisha yenye furaha na amani. Kwa wengine,kuwa na pesa nyingi ndio furaha.Ndio kipimo chao cha furaha.Kwa mwingine kuendesha gari ya thamani kubwa ndio kipimo cha furaha yake.Mifano ipo mingi.

Pamoja na tofauti za kimantiki na mbinu za kuwa na furaha na amani,yapo mambo mbalimbali madogo madogo(kwa wengine yanaweza kuwa makubwa) ambayo binadamu anaweza kuyafanya ili kujiongezea furaha maishani na kuwa na amani zaidi.Haya ni mambo ambayo sote tunaweza kuyafanya bila kuzingatia sana jinsia wala hali za vipato vyetu. Ni mambo gani hayo? Leo tutaangalia baadhi ya mambo hayo.

  • Piga marufuku mawazo hasi(negative thoughts): Furaha ya kweli huanzia kwenye akili yako na mawazo yako. Ukijipa mawazo hasi,ni wazi kwamba kitu kinachoitwa furaha utakuwa unakipiga kikumbo kwenda nje.

    Bahati nzuri ni kwamba kama binadamu,tumepewa uwezo mkubwa wa kuchagua. Unaweza kuchagua kuilisha akili yako mawazo hasi,yasiyojenga,yasiyo leta maendeleo yoyote au unaweza kuamua kuilisha akili yako mawazo chanya(positive thoughts),ya kimaendeleo na yanayojenga.Chaguo ni lako.

    Nimeshawahi kusikia watu mbalimbali wakilalamika kwamba hawana furaha maishani. Cha ajabu ni kwamba watu hao hao ukiwasikiliza sana katika maongezi yao,wamejaa mawazo hasi.Kila kitu kwao ni kibaya,kila mtu ni mbaya. Mahali pa kuanzia ni kichwani,akilini mwako.Jijengee tabia ya kuhifadhi mawazo mazuri. Mabaya achana nayo.Hayakufai na huna muda nayo.

  • Angalia mazuri ya kila jambo: Hili halitofautiani sana na hilo hapo juu. Tofauti inakuja katika utekelezaji. Wakati kupiga marufuku mawazo hasi kunatokea au kunatakiwa kutokea kabla ya tukio au matukio fulani, hili la kuangalia mazuri katika kila jambo hutokea baada ya kitu fulani. Kwa mfano:Una mtoto ambaye hakusikilizi? Badala ya kuzidi kumfokea na kulaani bahati yako ya kumzaa,kwanini usitumie nafasi hiyo kumfundisha jinsi na faida ya maelewano miongoni mwa binadamu. Kwanini usichukulie hali hiyo kama mojawapo tu ya mambo ambayo wewe kama mzazi ni lazima uyapitie? Kwanini usimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kukupa mtoto kwani unajua kabisa kwamba wapo wengine wengi ambao wanaomba kupata mtoto/watoto? read more

Je, imewahi kutokea ukawa na mgogoro na mfanyakazi mwenzako au hata kundi fulani la wafanyakazi wenzako,bosi wako nk? J,umewahi kushuhudia wafanyakazi wenzako wakiwa katika mgogoro au kutokuelewana kiasi kwamba wote hapo kazini mkakosa amani? Iwe ni wewe mwenyewe ulikuwa katika mgogoro au umeshuhudia wafanyakazi wenzako wakikosa kuelewana,ni imani yangu kwamba hukufurahishwa na jambo lile.

Tangu uchumi wa dunia ulipotetereka,tafiti mbalimbali zimeonyesha kwamba migogoro katika sehemu za kazi nayo imeongezeka maradufu.Wana-saikolojia wanaihusisha hali hiyo na wasiwasi uliowakumba wafanyakazi wengi kuhusu kutokuwa na uhakika wa nini kitatokea kesho(fear of uncertainity)

Haishangazi kuona kwamba,leo hii,jinsi ya kutatua migogoro mbalimbali inayoweza kutokea makazini ni mojawapo ya majukumu makubwa ya mameneja,wakurugenzi na pia wafanyakazi wenyewe. Tafiti mbalimbali zinaonyesha kwamba asilimia 24-60 ya muda makazini hutumika katika kutatua migogoro. Isitoshe,migogoro isiyokwisha katika sehemu za kazi matokeo yake huwa ni utendaji mbovu wa kazi, viwango hovyo vya utoaji wa huduma na kama ni sehemu ya biashara basi ni hasara au upotevu mkubwa wa hela.

Bila shaka ndio maana swali la ni hatua gani utazichukua ili kutatua migogoro mbalimbali inayoweza kujitokeza katika sehemu ya kazi ni mojawapo ya maswali yanayoulizwa zaidi wakati wa usaili(interview).

Leo ningependa tukumbushane mambo ya kufanya au kutofanya ili kuepuka migogoro makazini.Mambo ya kufanya au kutofanya ili kuepuka migogoro yaweza kuwa mengi sana.Mimi nitaongelea 8 kama ifuatavyo.Nakukaribisha ndugu msomaji,uongeze(kupitia njia ya maoni/comments) njia mbalimbali ambazo pengine umewahi kuzitumia au unatambua kwamba zinasaidia katika kuepusha migogoro makazini;

  • Punguza Kuongea: Maongezi ni jambo zuri. Lakini maongezi yakizidi huwa na tabia ya kuleta matatizo. Bahati mbaya zaidi ni kwamba punde maneno yakishakutoka,huwezi kuyarudisha.Utaomba msamaha,utaambiwa umesamehewa lakini ukweli ni kwamba ulichokisema kitabakia vichwani mwa mfanyakazi au wafanyakazi wenzako daima milele.

    Jitahidi kufikiri kwanza kabla ya kuongea.Njia pekee ya kuweza kufanya hivyo ni kuongea taratibu na kwa mpangilio.Kwanza utasikika vizuri zaidi na pili utaepuka migogoro inayoanzia kwenye maneno.

  • Epuka Umbea: Umbea na majungu ni chanzo kikubwa cha migogoro makazini. Sasa kama wewe ni mwanaume usidhanie kwamba hili halikuhusu. Umbea na majungu ni kwa wanaume na wanawake ingawa kuna tofauti kidogo za kitakwimu linapokuja suala la nani zaidi.Kwa vyovyote vile jiepushe na umbea au majungu kuhusu mfanyakazi au wafanyakazi wenzako.Jitahidi kufanya kazi yako kwa bidii na maarifa. Isitoshe huo ndio mwanzo wa kuheshimika.Hautoheshimika kwa kuwa msambazaji wa maneno ya uongo na matukio ya kutunga.
  • Subiri,tafakari kisha tenda: Makazini,kama zilivyo sehemu zingine ambazo binadamu hukutana,kupishana,kutofautiana kimavazi na kimawazo,huwa inatokea. Watu hukosa kuelewana.Inapotokea hivyo usikurupuke katika kuelezea malalamiko yako,mawazo yako au hata maoni yako.

    Unapojipa muda wa kutafakari unachotaka kukisema au kurekebisha, unajipa nafasi ya kuwa sahihi zaidi mara utakapoamua kutenda. Fanya utafiti wa kina kabla ya kusema.Kwa kufanya hivyo utaheshimika zaidi na pia utaepusha migongano isiyo ya lazima.Nasema isiyo ya lazima kwa sababu naamini kwamba wakati mwingine mashauri hujitokeza kwa nia njema ya kuwekana sawa. read more

Kama kichwa cha habari hii kinavyoashiria,makala yangu ya leo inatokana na barua pepe niliyotumiwa na msomaji wangu mmoja ambaye aliandika na kuuliza “Bro Jeff…nifanyeje ili niwe mzungumzaji mzuri mbele za watu kama vile Obama?“. Bila shaka kama tulivyo wengi wetu, msomaji huyu ni mpenzi wa Rais wa Marekani, Barack Hussein Obama. Anapenda jinsi Obama anavyoongea mbele ya watu, anavyofikisha ujumbe alioukusudia na anavyoeleweka.

Pengine na wewe,kama msomaji aliyeniandikia,unapenda kuongea mbele ya watu au ungependa kuwa muongeaji bora zaidi lakini linapokuja suala la kuongea mbele za watu wengi ila umekuwa ukishikwa na uoga au mchecheto kila mara ulipojaribu kufanya hivyo. Wakati mwingine umeshindwa hata kufikisha ujumbe uliokusudia na badala yake ukaishia kujilaumu kwamba huna ujuzi wa kutosha wa kufanya kile unachotaka kukifanya.

Bahati nzuri au mbaya ni kwamba dunia ya leo, inahitaji sana uwezo wa kuongea mbele ya watu. Kama wewe ni mwanafunzi ipo siku utahitajika kuwasilisha kitu fulani mbele ya darasa,mbele ya waalimu (Presentation). Hali ni hiyo hiyo kwa meneja, muuzaji(salesman),mkurugenzi wa idara fulani nk nk.

Kwa ufupi,sote tunahitaji kujifunza mbinu mbalimbali zitakazotuwezesha kuwa hodari zaidi katika kuzungumza mbele ya kadamnasi.

Bahati mbaya ni kwamba hakuna mtu anayeweza kuongea kama Obama. Wapo wanaoweza kuiga sauti yake na miondoko yake lakini si zaidi ya hapo. Kujaribu kuongea kama Obama ni kupoteza muda. Nina uhakika hata yeye hajaribu kuongea kama mtu mwingine. Anabakia kuwa yeye. Anachojaribu kufanya au ambacho amefanikiwa kufanya ni kuwa na uwezo wa kufikisha ujumbe wake pengine kama wengine waliomtangulia mfano Martin Luther King, Malcolm X na wengineo.

Obama ni Obama na wewe ni wewe.Hamfanani ingawa kama binadamu mna mahitaji sawa.Sote tunapenda kueleweka na kusikilizwa tunapoongea. Uwakilishi mzuri na uliokusudiwa kwa hadhira yetu(audience) ni jambo muhimu na linaloleta faraja mioyoni mwetu. Binadamu ndivyo tulivyo!

Bahati nzuri ni kwamba na wewe unaweza kujifunza alichojifunza Barack Obama. Ukijifunza kwa dhati utafanikiwa kufikisha ujumbe kama afanyavyo Obama lakini sio kuwa Obama. Leo tutaangalia mambo kadhaa ambayo unaweza kuyafanya ili kujifunza sanaa ya uongeaji mbele ya hadhara.

Sasa kwa sababu mwaka huu ni mwaka wa uchaguzi nchini mwetu, makala hii inaweza kuwa muhimu kwa wale ambao wameshajitoa muhanga kugombea nafasi mbalimbali za uongozi. Hao watahitaji sana kujua kuongea…kushinda hata anavyofanya Rais Obama au Kikwete.Haya hapa ni mambo unayoweza kufanya au kuzingatia;

  • Ongelea matatizo yanayowakabili au mafanikio ya unaozungumza nao: Jambo la kwanza la msingi unapoanza kuongea na watu ni kuhakikisha kwamba wanakuwa tayari kukusikiliza.Njia rahisi ya kufanikiwa katika hili ni kuanza kwa kuongelea matatizo yanayowakabili. Kufanya hivyo sio tu kutakupa masikio ya hadhira yako bali pia kutakusaidia hata kuyaelewa zaidi matatizo yao. Imani yao juu yao itaongezeka pia.

    Kinyume chake, anza kwa kuongelea mafanikio yao.Binadamu hupenda kusifiwa.Anza kwa kuweka bayana kwamba unavutiwa na kitu ambacho wamekifanya au wanakifanya. Watakuwa na uhakika kwamba wanaongea na mtu anayewaelewa vizuri na bila shaka watakuwa tayari kabisa kukusikiliza.

  • Usiongelee mambo magumu au kwa undani sana(Keep it Simple):Binadamu walio wengi hatupendi mambo magumu magumu. Wengi tunapenda kusikia mambo yenye kupendeza,kuleta matumaini,kuchekesha nk. Unapoongea na watu au mhadhara wa watu,jaribu kutoongelea mambo kwa undani sana au kuongea vitu vigumu vigumu.

    Mfano mzuri ni Rais wa Marekani Barack Obama. Kama ulimfuatilia wakati wa kampeni yake ya kuwania uraisi, ujumbe wake ulikuwa makini lakini mwepesi kueleweka kwa mtu yeyote. Ujumbe wake ulikuwa Change au “Mabadiliko”.

    Wengine walimbeza kwamba ujumbe wake ni mwepesi sana lakini matokeo yake sote tunayajua. Kama wewe ni daktari au mwanasheria au injinia nk,jaribu kusahau kuhusu elimu zako unapoongea na watu(hususani wananchi wa kawaida au watu ambao hujui wana kiwango gani cha elimu au uelewa wa fani yako). Narudia,Keep It Simple. read more

Waswahili tunao msemo usemao, Siku njema huonekana asubuhi. Ni msemo wa kale ambao tafsiri yake halisi inaweza kutofautiana baina ya mtumiaji mmoja kwenda mwingine. Huo ndio utamu wa lugha na misemo ya kwetu. Tunaweza kutofautiana lakini wote tukawa sahihi, angalau kwa mapana yake.

Pamoja na tofauti kadhaa zinazoweza kujitokeza katika tafsiri, nina uhakika kwamba wengi tutaelemea katika tafsiri rahisi ambayo ni kwamba unavyoianza siku ndivyo utakavyoimaliza. Hisia na vitendo vyako unapoianza siku yako vina mengi ya kusema kuhusu itakavyokwenda na itavyofikia ukingoni.

Ukiamka na kujihisi mchovu,ukaichukia siku hata kabla haijaanza,ni wazi kwamba utakuwa umejiweka mwenyewe kwenye mtego wa kuwa na siku mbaya! Hutofanikisha malengo yako.Kazini unapokwenda mambo yanaweza kwenda mrama.Kwanini? Umeiandaa vibaya siku yako.Ikitokea mwenzako fulani iwe kazini au shuleni akakuambia mbona leo unaonekana kama unaumwa au umechoka(hata kama anakutania tu) ndio kabisaaa anakuwa amekumaliza.

Kwa upande mwingine, siku njema huonekana asubuhi unaweza kuwa msemo unaoonyesha nguvu ya utabiri tuliyonayo sisi kama wanadamu.Tunazo hisia.Unaweza kuhisi kwamba kitu fulani unachokifanya au unachoacha kukifanya kinaweza kuwa na matokeo yasiyopendeza. Kila mmoja wetu anazo nguvu za utabiri.Tofauti ni jinsi tunavyozitumia,kuziamini au kuzifanyia kazi.

Bahati nzuri ni kwamba binadamu tumepewa uwezo mkubwa wa kunyumbulisha dunia na mambo mbalimbali.Sasa ufanyeje ili uianze siku vizuri? Wataalamu mbalimbali wa mambo ya saikolojia na utabibu wanakubaliana kwamba ukiianza siku yako mapema, itakuwa nzuri! Kuanza siku mapema, kwa mapana na marefu kunajumuisha kuamka mapema na kuwaza vyema.

Leo nimeamua kuongelea umuhimu wa kuamka mapema kwani kama nilivyotangulia kusema hapo juu,wataalamu wengi wanakubaliana kwamba kuamka mapema ni msingi wa kuwa na siku nzuri,maisha mazuri na kubwa zaidi,afya nzuri.Watu wengi ambao tunawaita “waliofanikiwa maishani” na hata matajiri wakubwa hapa duniani,wanalo jambo moja linalofanana. Katika kuwafuatilia(kupitia makala za magazetini,vitabuni na hata mahojiano yao katika televisheni) wote wanakiri jambo moja.Wote ni wa kwanza kudamka(early birds). Kwanini?Bila shaka kuna sababu.

Pengine baada ya kusoma kichwa cha habari umeshajiuliza; kwanini niamke mapema? Sababu ya Kwanza ni kwamba unapoamka mapema, unapata muda mzuri wa kujiweka sawa,kuipanga siku yako vyema. Imeshawahi kukutokea ukakurupuka usingizini na kukuta muda umeshakwenda na umechelewa kwenda unapotakiwa kwenda iwe ni kazini,shuleni au kwingineko? Umeshaona jinsi mpangilio wako wa mambo unavyokwenda kombo? Unapofika ofisini kwa mfano, unakuwa hata kuamka vizuri hujaamka bado na kila mtu anakutolea macho kwa sababu hata nywele hukukumbuka kuchana? Ungeamka mapema,ukaipanga siku yako vyema yote hayo yasingekukuta.

Faida ya pili ni kuweza kutumia ukimya wa asubuhi. Umeshawahi kudamka asubuhi ukaona jinsi palivyo na utulivu wa aina yake? Amini usiamini,ukiutumia ukimya huo wa asubuhi kuwaza na kupanga mambo yako,ni wazi kwamba utafanikiwa zaidi. Akili ya binadamu imetengenezwa ifanye vizuri zaidi panapokuwa na utulivu. Wenzetu wa magharibi ndio maana wakaja na msemo wa Silence is Golden.

Tatu,wataalamu wa afya wanasisitiza sana kuhusu kifungua kinywa(breakfast). Huo ndio mlo muhimu zaidi katika siku. Ni wazi kwamba ukiamka mapema, utapata muda mzuri wa kuandaa na kisha kupata kifungua kinywa kwa utaratibu unaofaa bila papara kitu ambacho ni muhimu kwa afya yako. read more

Bila shaka umeshawahi kusikia msemo wa wenzetu wa magharibi usemao “Time is Money”. Yawezekana kwamba msemo huo,kwa tafsiri ya moja kwa moja, unamaanisha kwamba muda ni pesa. Lakini ninavyoelewa mimi msemo huo unaongelea au unajaribu tu kuonyesha jinsi gani muda ni kitu cha thamani! Jinsi unavyoutumia muda wako hivi leo ni ishara tosha ya jinsi kesho yako itakavyokuwa.

Kwa upande mwingine umeshawahi kusikia mtu au watu fulani fulani wakilalamika kwamba “hawana muda” wa kufanya kitu fulani. Sababu itolewayo mara nyingi ni kwamba wapo “bize”. Wapo ‘bize” na ndio maana hawana muda wa kujitolea katika shughuli mbalimbali za kijamii.Ndio maana hawana muda wa kikao cha harusi cha rafiki,ndugu au jamaa.Hawana muda wa kuhudhuria msiba wa mtu. Wapo “bize” na ndio maana hawakuweza kukupigia simu nk.

Sasa inakuwaje mtu mmoja awe na muda na wakati huo huo mtu mwingine asiwe kabisa na muda wakati sote tunaishi kwenye dunia moja na siku ina masaa yale yale 24? Sababu zinaweza kuwa nyingi. Zingine zinaweza kuwa ni za visingizio tu.Zingine zinaweza kuwa za kweli na za uhakika.

Pamoja na hayo, jinsi unavyotumia muda wako, jinsi unavyopangilia mambo yako, ratiba zako nk, ni sababu ya kutosha kama una muda wa ziada wa kufanya mambo mengine mengi uyapendayo ikiwemo mapumziko, muda wa kukaa na wanafamilia yako, kufuatilia maendeleo ya watoto shuleni na lolote lile ambalo unapenda kulifanya lakini umekuwa hulifanyi kwa sababu au kisingizio cha ukosefu wa muda.

Leo tutaangalia baadhi ya mambo ambayo unaweza kuyafanya ili kuokoa muda ili kujipatia muda unaohitaji kwa sababu ambazo nimezitaja hapo juu;

  • Anza siku yako mapema: Hili ni la msingi sana.Amka mapema. Ukiianza siku yako mapema, sio tu kwamba kuna faida za kiafya kama ambavyo tutakuja kuziongelea katika siku za mbeleni, bali unakuwa na muda wa ziada wa kuiandaa ratiba kamili ya siku yako. Kwa ujumla binadamu anatakiwa kulala kwa muda wa masaa nane. Siri ya kuamka mapema inaanza na kwenda kulala katika muda unaofaa ili upate hayo masaa manane. Kumbuka siku njema huonekana asubuhi.Ipe siku yako mwanzo mzuri.
  • Orodhesha mambo unayotaka kufanya: Ushasikia msemo usemao; Mali bila daftari hupotea bila kujua. Hali ni hiyo hiyo hata katika suala zima la muda. Unapoianza siku hakikisha umeorodhesha mahali kwenye kikaratasi au kidaftari chako cha kumbukumbu mambo yote ambayo umedhamiria kuyafanya katika siku inayokukabili.Katika zama hizi za sayansi na tekinolojia,simu nyingi za viganjani zina huduma ya kalenda ambayo unaweza kuitumia kuorodhesha mambo unayotaka kufanya kesho,mwezi ujao au hata mwakani.Zitumie.Andika pia na muda ambao ni lazima utimize mambo hayo.

    Faida za kuorodhesha mambo unayotaka kufanya ni kwamba kwanza orodha hiyo itakuwa inakusuta. Itakuwa inakuuliza,ulisema leo utafanya hivi imekuwaje? Pili orodha hiyo hiyo itakupa pia nguvu au ari ya kutimiza malengo yako. Tatu na muhimu zaidi kama mada yetu ya leo inavyodai, utaokoa muda. Utafanya kila jambo kutokana na muda uliojipangia kwani orodha itakuwa inakuonyesha kwamba siku bado haijaisha na mengine yanakungoja.

    Pia wakati unaandika orodha yako, kumbuka kuweka pamoja mambo ambayo yanaweza kufanyika kwa pamoja au katika muda huo huo.Kwa mfano, leo umepanga kwenda katika benki fulani kuomba mkopo wa biashara.Wakati huo huo umepanga kwenda kwa chakula cha mchana na rafiki yako anayefanya kazi katika benki hiyo hiyo. Hayo unaweza kuyatimiza kwa pamoja. Unaweza kumuona meneja wa mikopo wa benki na kisha baada ya kumaliza ukaenda na rafiki yako kupata chakula. Hakikisha tu kwamba rafiki yako sio huyo huyo tena ndio meneja wa mikopo.Hapo kutakuwa na harufu ya ufisadi.Unajua tena jinsi mambo yalivyo nchini mwetu hivi sasa.Kuwa makini. read more

Ujasiriamali ndio neno jipya. Kila mtu anaongelea habari za ujasiriamali. Pengine hii inatokana na wengi wetu kutambua kwamba nyakati zimebadilika na ujasiriamali ndio njia iliyo sahihi zaidi kama mtu anatamani mafanikio ya kweli maishani.Vijana ndio chachu zaidi ya ujasiriamali au naweza kusema ndio wanategemewa zaidi kuendeleza ujasiriamali hususani katika ulimwengu wa leo wa sayansi na tekinolojia.

Pamoja na nia nzuri walizonazo vijana, pengine ukiwemo wewe unayesoma makala hii, kipo kizingiti ambacho ni lazima watu wajifunze mbinu mpya za kukivuka. Kizingiti hicho ni aina ya elimu itolewayo mashuleni. Kwa bahati mbaya elimu zitolewazo mashuleni bado hazijawekwa katika msingi unaomuwezesha kijana kujiajiri au kwa maneno mengine kuwa mjasiriamali pindi amalizapo masomo yake.

Bado tupo katika ule mfumo wa kikoloni. Ukimaliza shule unachotakiwa ni kuanza kutafuta kazi. Zunguka jijini Dar-es-salaam kwa mfano, utakutana na vijana wengi wasomi waliohitimu katika vyuo vikuu mbalimbali nchini wakiwa wamebeba vyeti vyao kwenye vijifuko vya plastiki wakizurura kusaka ajira. Hakuna anayefiria kujiajiri kwa kutumia elimu aliyoipata chuoni. Kwanini? Ndivyo ilivyo. Elimu aliyopewa haikumuandaa.Utakutana na engineer wa umeme ambaye hajawahi kubadilisha hata balbu!(nimeongeza chumvi kidogo hapa lakini kuna ukweli ndani yake!) Amesomea nadharia zaidi ya vitendo. Utakutana na mwanafunzi mhitimu wa masomo ya kilimo na mazingira ambaye hajui shamba ni nini.Hilo ni kosa katika mfumo wetu wa elimu. Ni lazima serikali ichukue jukumu la makusudi kubadili mfumo huo.

Lakini wapo wengine wengi ambao wana nia ya kweli ya kuwa wajasiriamali. Wana nia ya kujiajiri. Leo tutaangalia jinsi gani mjasiriamali chipukizi aanzishe kampeni yake. Si ushasikia kwamba biashara siku hizi ni kujuana? Ujasiriamali pia. Ni muhimu sana kujua ni nani au ni wapi uende endapo mambo yatakwama. Siongelei wapi uende kutoa au kupokea rushwa.La. Nataka kuongelea kitu kinachoitwa na wenzetu wa magharibi “networking”.Kwetu sisi hiki ndicho tunachoita “mtandao”.Mitandao ya kijamii kama vile facebook,twitter,myspace nk ni sehemu nzuri ya kutengeneza network.Itumie vizuri.

Ni muhimu kutengeneza mtandao mzuri kama unataka kuwa mjasiriamali makini na hususani kama unataka kufanikiwa. Kumbuka kwamba hapa hatuongelei kubadilishana business cards peke yake bali kumjua mtu kwa nia njema ya kusaidiana.Kumbuka neno ni “kusaidiana” na sio wewe pekee kupokea msaada.Lazima pawe na nia njema ya kusaidiana.

Kabla sijaanza kuorodhesha mbinu mbalimbali za kutengeneza ‘mtandao’ wako, naomba nikwambie kwamba siri ya kwanza ya kuanza kuwa mjasiriamali ni maandalizi.Jiandae kwa mtaji,elimu(ya darasani na mtaani),mbinu za kibiashara nk. Pili hakikisha kwamba una mapenzi ya dhati na hicho unachotaka kufanya.Usiingie kwenye biashara au ujasiriamali kwa sababu tu umemuona fulani amefanya hivyo.Kuna umuhimu mkubwa wa kujitambua katika suala zima la ujasiriamali. Baada ya kusema hivyo,sasa tuingie kwenye maeneo ya kutengeneza mtandao wako kama mjasiriamali;

  • Washindani wako: Biashara ni ushindani lakini sio uadui.Kama unataka kuwa mjasiriamali mwenye mafanikio ni vizuri sana ukawajua washindani wako wa kibiashara.Pata vipeperushi vyao,tembelea tovuti zao,wajue wateja wao na kwanini hao watu ni wateja wao.Kisha jitambulishe kwao.Najua hapa unasema;nijitambulishe?!! Ndio,jitambulishe.Kama nilivyosema ni washindani lakini sio maadui zako. Mshindani wako anaweza kukufaa pia.Anaweza kuzidiwa na kazi akakusukumia zingine.Jitambulishe,jenga uhusiano mzuri wa kibiashara.Isitoshe nyote mpo kwenye biashara moja,sekta moja.Ya kesho hamyajui.Kama kuna chama au ushirika wa watu waliomo kwenye eneo lako la ujasiriamali,jiunge. read more

MafanikioKuanzia wiki hii BC inaanzisha kitu kitakachokuwa chini ya kipengele cha BC MAARIFA.Kila mwisho wa wiki(jumamosi au jumapili)kutakuwa na makala kuhusu mambo mbalimbali ya maendeleo ya kimaisha na kibinadamu katika nyanja mbalimbali kama vile mahusiano,kazi,pesa,afya,familia nk.Kutakuwa kunatolewa dondoo mbalimbali zinazohusiana na maendeleo binafsi ya mtu(Personal Development.

Nia ni kupeana maarifa au ujuzi fulani fulani ambao unaweza kutusaidia sote kama watu binafsi au jamii.

Naomba tu niweke wazi kwamba hii ni Pilot Project kwa maana ya kwamba ni kitu ambacho tunakifanyia majaribio.Kama unapenda kipengele cha namna hii,tungefurahi kama utatuambia aidha kwa kupitia kwenye sehemu ya maoni au kwa kutuandikia e-mail.Kuendelea kwake kutategemea sana mchango wako.

Pia kama wewe ni mwandishi na ungependa kuandika katika mtindo huu huu wa Tips for Personal Development,usisite kutuandikia.Leo tunaanza na mada iliyopo hapo chini.Asante kwa ushirikiano.

KWANINI SIFANIKIWI VYA KUTOSHA?

Tamaa ya mafanikio katika maisha ni safari ndefu. Kwa wengi wetu ni safari ya kudumu. Kila mara tunataka zaidi. Tunataka kuwa kama fulani au fulani.Tunatamani kuwa na kiasi cha fedha kama au kuliko fulani.Kuwa na mke au mume mzuri na mwenye heshima kama fulani. Na kwa wale ambao maisha yao huendeshwa na tamaa za kuwa maarufu basi kila leo huwa wanataka kuwa kama mwanamuziki,muigizaji filamu,mwanasiasa fulani na vitu kama hivyo.

Ingawa ni vigumu sana kwa binadamu kufikia mahali ambapo anaweza kusema kwamba amesharidhika vya kutosha na alichonacho na hataki nyongeza yeyote zaidi,yawezekana kabisa mtu akafikia mahali pa kuridhisha ingawa hiyo haimaanishi kwamba akipata nafasi ya kupata zaidi hatoitumia. Hapa tunaweza kusema mtu anakuwa ameridhika kwa kiasi cha hali ya juu.

Lakini kwanini basi baadhi yetu tunashindwa kufikia japo robo tu ya mafanikio tunayoyatamani? Ni mambo gani yanatukwamisha? Leo nimeona tuongelee kidogo sababu kadhaa ambazo zinatufanywa wengi wetu tukwame na hata kuishia kulaumu watu wengine bila kutambua kwamba yawezekana sababu sio ukosefu wa elimu ya kutosha,mtaji wala chochote kile bali sisi wenyewe;

  • Hujiamini vya kutosha: Ukijaribu kuangalia au kufuatilia maisha ya watu ambao sote tunaamini kwamba wana mafanikio zaidi yetu utagundua jambo moja muhimu;Wanajiamini.

    Wanaamini kwamba wanalo jambo au mambo ya msingi wanayoweza kuchangia katika jamii. Wanajiamini na wana madhumuni ya makusudi kuhakikisha kwamba jamii itawakumbuka.

    Watu hao pia huwa ni wajuzi wa kuketi chini wakajikosoa wenyewe na kisha kusonga mbele zaidi na zaidi.

    Je wewe hapo ulipo una kitu gani cha kipekee? Unayo maarifa au ujuzi (skill or talent) gani maalumu ambao hujaufanyia kazi kwa sababu ya kutojiamini tu? Kwanini usiamke leo ukaanza kujiamini zaidi kisha uone jinsi utakavyobadilisha muelekeo? read more

↑ Go Back to Top of Page