MY TANZANIA   |   PLACES TO GO   |   MEDIA   |   ONLINE ENTERTAINMENT    

hasheem-thabeetb

Kwa mapana na marefu,jina la Hasheem Thabeet litatawala vichwa vya habari wiki hii.Swali au maswali ambayo wengi wanajiuliza ni je Hasheem Thabeet atajiunga na timu gani?

Mambo mengi yanasemwa kuhusu Hasheem.Wapo bado wanaoendelea kusema kwamba bado hayupo tayari kwa sababu alianza kucheza mpira wa kikapu “ukubwani’! Pamoja na hayo,wote wanaosema hivyo wanakubali pia kwamba Hasheem ataleta “impact” kubwa katika NBA.Wapo ambao wamefikia hata kumbeza kwamba hatoweza kutamba kama ilivyokuwa kwa Mzaire Dikembe Mutombo na badala ya yake atakuwa kama Msenegali Mouhamed Sene (Mo Sene) ambaye kimsingi hafanyi vizuri katika NBA kama alivyotarajiwa.

Waache waseme.Kwetu sisi muhimu ni kwamba kijana wetu atakuwa mtanzania wa kwanza kucheza katika NBA. Ni matumaini yetu kwamba Hasheem atafungua milango kwa wengine wengi ambao kupitia kwake wataamini kwamba “inawezekana”.Binafsi naamini Hasheem atafanya vizuri.Cha msingi ni kwamba ni lazima awe msikivu kwa makocha wake,wachezaji wenzake na daima azingatie mazoezi na kujiweka mbali kidogo na “mambo ya ujana”.

Watabiri wa mambo wanasema kuna uwezekano mkubwa  kwamba Hasheem atajiunga na Memphis Grizzlies ingawa yeye mwenyewe inasemekana hangependelea sana.Je atajiunga na timu gani basi? ESPN wataonyesha zoezi hili. Tizama ratiba ya hapo ulipo.Kwa sasa mtazame Hasheem na wenzake ambao ndio “wapo juu” katika pick ya mwaka huu.

ngassabc

Mshambuliaji hatari wa timu ya soka ya Yanga, Mrisho Ngassa hapo jana alijipatia “jiko”. Amemuoa Latifah Abdulhaman. Ndoa ilifungiwa huko Tabata Kisiwani.

Hivi karibuni Ngassa alikuwa nchini Uingereza kufanya majaribio ya kuchezea timu ya West Ham. Habari zinapasha kwamba sehemu ya kwanza ya majaribio hayo ilikwenda vizuri na kwamba kunako majaaliwa Ngassa atarejea tena nchini Uingereza kwa  majaribio mengine.

BC inawatakia Mr.& Mrs Ngassa kila la kheri katika ndoa yao.

Photo/Michael Jamson via Charaz

yanga12bc

Tuende mbele turudi nyuma,ukipata nafasi ya kuchezea Yanga au Simba basi suala la umaarufu au u-celebrity halina mjadala sana.Wapo watu lukuki ambao watalijua jina lako,wataitambua sura yako na ukiwa mitaani watapenda kupiga japo stori kidogo na wewe.Ndio maana zinapokuja habari kwamba ama Yanga au Simba wametwaa ubingwa nchini,basi hiyo huwa ni habari kubwa iwe mtaani au kwenye vyombo vya habari.Mpaka hivi leo mchezo wa Yanga na Simba huwa ni gumzo kubwa mtaani.

Kwa bahati nzuri au mbaya,safari hii ni Yanga tena.Yanga wameutwaa ubingwa wa ligi ya soka nchini Tanzania kabla hata ya ligi hiyo kumalizika.Kwa maana hiyo wanastahili pongezi.

Lakini ubingwa wa soka nchini Tanzania,umaarufu,pesa nk vinakuwa na raha yake kama angalau vitakumbuka walipolala na kuamkia mashabiki wao.Tumekuwa tukiona jinsi ambavyo wanamichezo katika nchi zilizoendelea wanajitolea kwa namna mbalimbali ili kuboresha jamii zilizowazunguka na pia mashabiki wao.Wengi wanajitolea kwa namna mbalimbali kama vile kujitolea muda wao,pesa zao,ujuzi wao .Kama sio hivyo, basi wamekuwa wakijitolea katika aidha kuhamasisha michango ya hiari,kujitegemea,kujiamini miongoni mwa vijana nk.

Nchini Marekani kuna kitu kinaitwa NBA Gives Back.Hawa ni wachezaji wa ligi ya mpira wa kikapu ya Marekani ya Kaskazini waki-toa chochote wanachoweza au walichopata kwa jamii zao,kwa mashabiki wao.Wachezaji wenye majina nchini Tanzania,wanaweza kuiga hili.Wadhamini wa ligi hiyo,Vodacom,wanaweza kuhamasisha hili kwa kuwatumia wachezaji wa ligi ya soka Tanzania.Shirikisho la Soka nchini linaweza kusimamia au kuongoza harakati kama hizo.

Tusiishie kwenye kufurahia tu Ubingwa bila kukumbuka walikolalia au kuamkia mamilioni ya mashabiki wa soka nchini.Lakini mbali ya yote,BC inatoa Hongera kwa Yanga!

Mojawapo ya majina yaliyovuma sana katika ulimwengu wa soka nchini Tanzania,hususani miaka ya themanini, ni lile la Ahmed Abdulthabit Amasha(pichani).Ahmed Amasha alikuwa ni beki wa kutumainiwa wa timu ya Yanga ya jijini Dar-es-salaam. Mwaka 1984 Amasha alichaguliwa kuwa Mchezaji Bora wa Mwaka.Hivi sasa anafundisha soka huko Oman akiwa kocha wa timu ya Seeb SC.

Picha kwa hisani ya Mroki.

 

 

Hapo zamani kulikuwa na majina kama Athumani Mambosasa, Juma Pondamali,Joseph Fungo,Sahau Kambi, Iddi Pazi, Mohamed Mwameja na wengineo. Hao wote walikuwa ni walinda milango (makipa) waliojizolea sifa kemkem kutokana na umahiri wao katika kuzilinda nyavu zao zisitikiswe na timu pinzani.

Hivi sasa, huku watanzania wakiwa wamepata upya mwamko wa kupenda soka na kuunga mkono timu za nyumbani(hususani Taifa Stars), tunaye Tanzania One,Ivo Mapunda (pichani). Huyu ndiye kipa nambari moja wa timu ya taifa ya soka kwa upande wa wanaume,Taifa Stars na pia klabu maarufu na kongwe ya Yanga ya jijini Dar-es-salaam. Ameshatwaa tuzo ya Mchezaji Bora wa mwaka nchini Tanzania mara mbili. Ushauri kwa Ivo Mapunda?

Leo hii anaaminika kuwa mnenguaji wa kike maarufu kupita wote nchini Tanzania hususani katika muziki wa dansi. Ubunifu,uwezo wake katika kunengua na kujituma vilivyo awapo jukwaani inasemekana ndio siri ya mafanikio yake.

 

Huyu si mwingine bali ni Aisha Mohamed Mbegu maarufu kwa jina la Aisha Madinda, mnenguaji tegemeo wa bendi ya African Stars ’Twanga Pepeta’. Alijiunga na bendi hiyo mwaka 2001.Umaarufu huo ndio umemfanya Aisha Madinda awe mnenguaji au mcheza show ambaye huongelewa zaidi mitaani na pia kwenye vyombo mbalimbali vya habari nchini Tanzania.

Hivi karibuni tulipata fursa ya kufanya naye mahojiano kuhusu mambo mbalimbali yakiwemo kuhusu maisha yake binafsi,mipango yake ya baadaye nk.Pia Aisha anajibu kuhusu shutuma mbalimbali ambazo zimekuwa zikimzunguka kama vile matumizi ya madawa ya kulevya,upigaji wa picha za uchi nk.Ukweli uko wapi katika yote haya? Fuatana nasi katika mahojiano yafuatayo; (more…)

Pichani Raisi Jakaya Mrisho Kikwete, akiwa na wachezaji wa Taifa Stars na makocha wao alipowatembelea kambini kwao katika hoteli ya Golden Tulip jijini Dar hapo juzi.

Pamoja na kuungwa mkono na kila mtanzania, timu yetu ya taifa ya soka, Taifa Stars, imeshindwa kututoa kimasomaso katika iliyokuwa kampeni nzito ya kutaka kutupeleka nchini Ghana hapo mwakani kwenye fainali za kombe la mataifa ya Afrika.

Matokeo ni kwamba Taifa Stars imechapwa goli moja kwa bila (1-0) na timu ya taifa ya Msumbiji,(Mambaz). Kwa maana hiyo kampeni zetu kuelekea Ghana ndio zimefikia kikomo kwa mwaka huu.

Unadhani nini kimetokea? Kwa maoni yako kwanini Taifa Stars imeshindwa? Nini kifanyike kwa siku za mbeleni? Unauongelea vipi utaratibu mzima wa shirikisho la soka la Tanzania (TFF) katika uuzaji wa tiketi za mchezo wa Taifa Stars na Msumbiji? Ungepata nafasi ya kumhoji kocha mbrazili wa Taifa Stars, Maximo au raisi wa shirikisho la soka la Tanzania, Leodgar Tenga, ungependa kumuuliza swali/maswali gani? Tunaomba maoni yako.

Kwa mpenda soka ya Tanzania yeyote yule, hususani mnamo miaka ya themanini,jina Lawrence Mwalusako sio geni hata kidogo. Alikuwa sio tu kipenzi cha wapenda soka bali beki wa kutumainiwa wa timu zote alizowahi kuchezea, zikiwemo Waziri Mkuu Dodoma, Pan African, Yanga na timu ya taifa,Taifa Stars. Ndio maana yanapotajwa majina ya wachezaji soka nchini Tanzania waliowahi kuwika na jina la Mwalusako likakosekana,wadau wa soka,wanaoijua vyema historia ya soka la Tanzania,watakuambia wazi,something is missing.

 

Lawrence Mwalusako ni wa sita kutoka kushoto waliosimama.

Waliosimama kutoka kushoto: Marehemu Daktari wa timu Peter Manyika,Meneja John Manongi,Abeid Mziba “Tekero”,Athumani China,Yusuf Ismail Bana,Lawrence Mwalusako,Said Mrisho,Edgar Fongo,Isihaka Hasan,Golikipa Joseph Fungo,Kocha Mwinda Ramadhan.

Waliochuchumaa kutoka kushoto: Marehemu Lucias Mwanga,Rashid Idd Chama,Moshi Majungu,Allan Shomari,Ali Mchumila,Freddy Ferix Minziro,Abubakar Salum “Sure Boy”

Picha hii ilipigwa Mwaka 1987 uwanja wa taifa wakati wa mechi ya premier kati ya Yanga na Maji Maji.

Safari ya Mwalusako katika medani ya soka inaanzia kule Kyela mkoani Mbeya alipozaliwa mnamo mwaka 1960.Tulipofanya naye mahojiano hivi karibuni,Mwalusako ameongelea mambo mengi yakiwemo mtazamo wake wa soka la bongo hivi sasa,washambuliaji aliokuwa anawaheshimu,ushauri kwa wanasoka chipukizi nk.Pia anagusia jinsi “juju” ilivyo katika timu kubwa na pengine hata zile ndogo. Fuatana nasi katika mahojiano haya ambayo hata yeye mwenyewe anakiri,hajawahi kufanya na chombo chochote cha habari duniani akiwa kama mchezaji na hata baada ya kustaafu. Hivi sasa yeye ni Corporate Affairs Manager wa kampuni ya Sumaia Group Tanzania.Anaishi Dar-es-salaam.

BC: Unaweza kukumbuka wakati ulipokuwa mdogo ni nani alikuvutia katika mchezo wa soka? Kulikuwa na mtu yeyote maalumu ambaye ulimuona kama role model wako katika soka? (more…)

↑ Go Back to Top of Page