MY TANZANIA   |   PLACES TO GO   |   MEDIA   |   ONLINE ENTERTAINMENT    

Kila siku huwa napokea hoja,mapendekezo,ushauri kutoka kwenu wasomaji wa BC.Pia huwa napokea maswali mbalimbali.Nikiwa na ufahamu mkubwa juu ya swali lililoulizwa huwa najibu.Ninapokuwa sina jibu,wajibu wangu ni kutafuta jibu ama kwa kuomba msaada kutoka kwenu wasomaji na wachangiaji wa BC au vinginevyo. Leo nimepokea swali ambalo sina jibu kwani swali hili limeelekezwa moja kwa moja kwa celebrities. Mwenzetu mmoja ameuliza swali lililopo hapo chini na mwisho ametoa ombi.

Ningefurahi sana kama angalau celebrity mmoja angejitolea kulijibu. Sio lazima ajibu kama mwakilishi wa celebrities wengine,bali yeye kama mtu binafsi. Asante Allen kwa swali zuri.

Napenda kuwapongeza sana kwa kazi nzuri mnayofanya. Nina swali dogo sana kwa hawa Bongo Celebrity kwamba mbona hatuwaoni wakiwa mstari wa mbele katika kuhakikisha nchi yetu inapunguza au kutokomeza kabisa vifo vya mama na mtoto vinavyotokana na uzazi.

Mwezi wa kumi na mbili mwaka jana tulishuhudia mwana Mitindo mashuhuri nchini Uingereza Naomi Campbel akifanya onyesho la mitindo pale Movenpick kwa ajili ya kuchangisha fedha kwa ajili ya kupunguza vifo vya mama na mtoto dunia nzima. Wanamuziki wetu, wanamichezo , wanamitindo na hawa wengine tunaowaita Bongo Celebrity wako wapi katika kuhakikisha nchi yao inafikia malengo ya milenia namba 4 na tano ifikao 2015.

Hongera kwa Stara Thomas kwa kuwa mstari wa mbele kuhakikisha nchi yetu inapunguza vifo vya mama na mtoto kwa kiasi kikubwa. Napenda kuwakumbusha kuwa Tanzania bila vifo vya mama na mtoto inawezekana.

Timu ya taifa ilipocheza na Ivory Cost fedha nyingi sana zilipatikana.
Wachezaji hawa ni matokeo ya kina mama hawa ambao leo wanakufa kutokana na matatizo ya ujauzito. Tunaweza kutumia timu yetu ya taifa kupunguza pia vifo hivi vya mama na mtoto.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ni miongoni mwa viongozi wakubwa duniani wanaohakikisha nchi zao zinapunguza vifo vya mama na mtoto.

Nawaombatuungane pamoja kwa kutumia vipaji Mungu alivyotupatia kumsaidia Rais wa Jamhuri ya Muungano wa tanzania kupunguza vifo vya mama na mtoto kwa vipaji vyetu na umaarufu tulio nao katika jamii yetu.

mariabcUkimuuliza mtanzania yeyote wa kawaida kuhusu tatizo kubwa linaloikabili nchi hivi sasa,jibu utakalopewa ni “ufisadi”. Hili ni tatizo ambalo mpaka hivi sasa linaelekea kuzidi tu kuota mizizi. Viongozi wetu nao wanawanyooshea wengine vidole. Wale wa chama tawala nao wananyoosheana vidole. Wanasema ndani ya chama chao kuna mafisadi wanne tu!Ni kina nani hao?Kama wanajulikana inakuwaje bado wapo?

Hivi ni nani atamfunga paka kengele? Tatizo tumeshalijua. Ni ufisadi. Ni kuporomoka kwa maadili ya ki-uongozi. Kujilimbikizia mali ndio ujanja kwa mujibu wa wale walio kwenye nafasi za kufanya hivyo. Uzalendo leo hii unaishia kwenye bendera na lugha tu. Ukiwaona wanavyokenua utadhani wanakujali. Kumbe wanajiuliza una shilingi ngapi mfukoni ili wazichukue.

Mama Maria Nyerere,mjane wa Baba wa Taifa, hivi majuzi ameuliza maswali ya msingi na kukemea kwa jinsi anavyoweza. Alikuwa huko Hai mkoani Kilimanjaro. Bonyeza hapa usome alichokisema na kuonya. Bidii hizi hazina budi kuungwa mkono. Isitoshe uchaguzi umekaribia.Huu ni wakati wa kusema Imetosha Sasa. Amka na mwamshe mwenzio.

anna_tibaijukabc

Miongoni mwa wanawake ambao ni nyota,mfano wa kuigwa na ambao Tanzania inajivunia kuwa nao ni Prof.Anna Tibaijuka. Ni miongoni mwa wale wanawake ambao DaMija huwaitwa “Wanawake wa Shoka”.

Pamoja na hayo,hivi karibuni ulimwengu ulishuhudia cheo alichokuwa akikishikilia pale UN-Habitat yenye makao yake makuu jijini Nairobi-Kenya kikiota mbawa katika mazingira ambao wengi hawajaelewa wala kukubaliana nayo.Miongoni mwa wasiokubaliana na “kushushwa cheo’ kwa Prof.Tibaijuka ni wafanyakazi wenzake.

Je ni kwanini Ban Ki Moon amemshusha cheo mama Anna Tibaijuka wakati hata hivyo mkataba wake ulikuwa unaelekea ukingoni(2010)? Je kuna harufu ya ufisadi? Soma zaidi kwa kubonyeza hapa na kisha tizama taarifa ya habari hapo chini kisha uwe muamuzi.

You need to a flashplayer enabled browser to view this YouTube video

womens_day_greeting

Leo ni siku ya Wanawake Duniani(Women’s Day).Ni siku ambayo husheherekea mafanikio na mchango wa wanawake katika nyanja zote za maendeleo ya binadamu iwe ni kiuchumi,kijamii au kisiasa.Ni siku ambayo inatukumbusha sote umuhimu wa kipekee wa wanawake duniani.Hapa tunawazungumzia mama zetu,dada zetu,wake zetu,watoto wetu,shangazi zetu,binamu zetu,majirani zetu wanawake,marafiki zetu,maadui zetu nk.

Mwanamuziki maarufu kutoka nchini Marekani,James Brown, aliwahi kuimba “It’s A Man’s World but It Would Be Nothing Without a Woman”. Hilo halina ubishi.Dunia tuionayo leo kama dunia,inatokana na mchango mkubwa wa wanawake.Dunia si dunia bila mwanamke.Haipo.

BC inaungana na wote katika kusheherekea siku hii na pia kuwasihi wanawake,popote pale ulimwenguni, waendelee kufanya ambacho wamekuwa wakikifanya tangu mwanzo wa dunia hii.Happy Women’s Day.

Mtizame James Brown na Luciano Pavarotti hapo chini wakiimba Its A Man’s World.Mungu azilaze roho zao mahali pema.

You need to a flashplayer enabled browser to view this YouTube video

simbabc

Pichani ni Mheshimiwa Sofia Simba,ambaye hivi karibuni alichaguliwa kuwa Mwenyekiti mpya wa Jumuiya ya Wanawake wa CCM nchini Tanzania.

Mheshimiwa Simba alichaguliwa katika uchaguzi ambao unasemekana ulikuwa wenye upinzani mkali katika historia ya jumuiya hiyo.Alishindana vikali na Mh.Janeti Kahama.

Kama zilivyo chaguzi nyingi kinachofuata baada ya vuta nikuvute huwa ni kazi.Je unadhani ni matatizo gani ya msingi yanayowakabili wanawake wa Tanzania?Ungependa kumpa ushauri gani Mh.Sofia Simba kuhusiana na Jumuiya anayoiongoza?


Kwa wengi,nchini Tanzania na duniani,anabakia kuwa mrembo kutoka nchini Tanzania aliyeiwakilisha nchi yake katika shindano la dunia la Miss Universe mwaka 2007 na kuwa mshiriki wa kwanza aliyeamua kulipanda jukwaa akiwa kipara.Kwa wengine,wakiwemo ndugu,jamaa na marafiki zake,anabakia kuwa Flaviana Matata.

Hivi karibuni alilivua rasmi taji lake la Miss Universe Tanzania 2007 baada ya kulitumikia kwa muda wa mwaka mzima.Tulipata nafasi ya kuongea machache na Flaviana baada ya kumkabidhi rasmi mrembo mwingine,Amanda Sululu, taji la Miss Universe Tanzania. Hivi tunavyoongea tayari Amanda yupo nchini Vietnam tayari kabisa kwa shindano la Miss Universe litakalofikia kilele nchini humo tarehe 13 Julai mwaka huu.

Sasa kama sote tujuavyo,mwaka sio kitu kidogo.Mambo mengi hutokea,mengi huweza kusemwa nk.Je ni yapi aliyapitia ndani ya mwaka mmoja alipokuwa akishikilia taji la Miss Universe Tanzania 2007? Na si unakumbuka ule mkasa wa kuzimia siku ya kupima ukimwi?Nini hasa kilitokea?Ni kweli alikuwa anaogopa kupima afya yake?Ana mipango gani hivi sasa? Anampa ushauri gani Amanda na pia vijana wenzie? Kwa hayo na mengineyo mengi,fuatana nasi katika mahojiano yafuatayo; (more…)

Miongoni mwa wanawake wanaofahamika na kuheshimika katika fani ya sheria nchini Tanzania ni Jaji Eusebia Nicholas Munuo(pichani).Hivi leo yeye ndio Makamu wa Rais Mteule wa Chama Cha Majaji Wanawake Duniani(IAWT).Mbali ya cheo hicho,Jaji Munuo pia ndio Mwenyekiti wa Chama Cha Majaji Wanawake nchini Tanzania(TAWJA).Yeye ndio Hakimu wa kwanza mwanamke nchini Tanzania na pia Jaji wa kwanza mwanamke katika Mahakama ya Rufaa nchini Tanzania.

Miezi kadhaa iliyopita Jaji Munuo alifanya mahojiano maalumu na mwandishi Happy Katabazi kuhusiana na mambo mbalimbali ya kijamii,kisheria na pia kumhusu yeye binafsi.Je ni kweli kwamba Jaji huyu aliwahi kuamuru kwamba mumewe atiwe ndani kutokana na kuidharau mahakama?Ili kupata jibu la swali hilo na mengine mengi kumhusu Jaji Eusebia Munuo,bonyeza hapa uitembelee blog ya Happy Katabazi.

Photo/Happy Katabazi

Mbunifu wa Mitindo maarufu,Khadija Mwanamboka, akiwa pamoja na Shamim Zeze,mmiliki na mwendeshaji wa blog ya 8020 Fashions,hivi karibuni jijini Dar. Khadija Mwanamboka ni miongoni mwa waanzilishi wa shirika lisilo la kiserikali lijulikanalo kama Tanzania Mitindo House ambalo linajaribu kusaidia watoto yatima na wasiojiweza nchini Tanzania. Mwaka jana tuliwahi kuongea kidogo na Mwanamboka kuhusiana na TMH.

Katika nchi nyingi za magharibi,leo ni Mother’s Day au kwa maneno mengine Siku ya Mama.Leo ni siku maalumu ya kumkumbuka,kuutambua na kuuthamini rasmi mchango wa mama yako katika maisha yako.Huu ni utamaduni wa kimagharibi ambao unazidi kuenea kwa kasi ulimwenguni kote zikiwemo pia nchi zetu za kiafrika.Sasa hii sio kumaanisha kwamba katika siku zingine usimkumbuke,usiutambue wala usiuheshimu rasmi mchango wa mama yako.La Hasha!Kila siku,kwa walio wengi, ni siku ya mama. Kwetu sisi waafrika ndio kabisaa.Ndio maana kuna ule usemi kwetu wa Nani Kama Mama?

Itumie siku ya leo kumkumbuka mama yako.Kama kwa bahati mbaya alishaiaga dunia,basi chukua muda maalumu kumkumbuka,kumuombea na muhimu zaidi kumuenzi.Kama upo karibu na mama yako,basi mkumbatie na umkumbushe kwamba unampenda na unamtakia kila la kheri katika maisha.

Ni muhimu pia kukumbuka kwamba, kama binadamu,huwa inatokea wakati mwingine tukakosa kuelewana.Ndio.Huwa inaweza kutokea tukakosa kuelewana hata na mama zetu! Kama hali ipo namna hiyo katika maisha yako,itumie siku hii kusameheana na kuweka mambo sawa na mzazi wako.Jinsi moja nzuri ya kuweza kusamehe ni kujiuliza swali;Je kuna ulazima au manufaa yoyote ninayoyapata kutokana na kutokuelewana huku? Usiwe mgumu wa kusamehe ili nawe upate kusamehewa.Sote tunakosea katika maisha.Kama leo basi ni kesho.Usisite kutenda lililo jema leo.

Katika kuisindikiza siku hii,tumekuchagulia wimbo maalumu kutoka kwa mwanamuziki mkongwe wa nchini Nigeria, Prince Nicco Mbagga.Wimbo unaitwa Sweet Mother. Huu ni wimbo maalumu kwa kina mama wote.Kinamama,tunawapenda na tunawathamini.Bila ninyi dunia si dunia.Bonyeza player hapo chini upate burudani,sikiliza ujumbe uliomo ndani ya wimbo.Happy Mother’s Day!

Audio clip: Adobe Flash Player (version 9 or above) is required to play this audio clip. Download the latest version here. You also need to have JavaScript enabled in your browser.

Picha moja ni sawa na maneno elfu moja.Wakati mwingine huwa ni zaidi ya hata ya maneno elfu moja.Ukiisoma picha hii vizuri utaweza kuona mengi.Hatuhitaji kuandika maneno mengi ili kukuwezesha wewe msomaji na mtazamaji kupata ujumbe.Picha hii ambayo ni ya kina mama huku wengine wakiwa na watoto wao migongoni(sijui kina baba wako wapi hapa) ni kutoka katika kijiji cha Bermi huko Babati,kaskazini mwa Tanzania. Picha ni kwa hisani ya peacecorpsonline.org.Hii ndio picha yetu ya wiki hii.

Read the Next Page →

↑ Go Back to Top of Page