
Jina la Sauda Mwilima (pichani)sio geni miongoni mwa watanzania wengi hususani wapenzi wa vipindi mbalimbali vya televisheni.Yeye ni mtangazaji kupitia Kituo Cha Televisheni cha Star kinachomilikiwa na kampuni ya Sahara Communications sambamba na vituo vya radio vya Kiss FM na Radio Free Africa.Vipindi anavyoruka navyo hewani ni Bongo Beats na Mcheza Kwao.
Hivi karibuni BC ilipata nafasi ya kufanya naye mahojiano utakayoyasoma hivi punde.Je unajua Sauda anapendelea kuvaa namna gani anapotoka?Kuna mahali maalumu anapopenda kununulia “viwalo” vyake? Ana ushauri gani kwa vijana wengine ambao wangependa kuja kufanya kazi ya utangazaji kama yeye? Fuatana nasi katika mahojiano yafuatayo;
BC: Sauda,asante sana kwa kukubali kufanya nami mahojiano haya…mambo vipi?
SM: Mambo fresh tu.Nashukuru Mungu,siku zinakwenda.
BC: Kwa kuanza na kwa faida ya wasomaji wetu,unaweza kuniambia ulizaliwa lini,wapi,ukakulia wapi na mambo kama hayo?
SM: Nilizaliwa miaka 30 iliyopita,hapa hapa jijini Dar-es-salaam katika hospitali ya Rufaa ya Muhimbili.Baadaye tulihamia Dodoma ambapo niliishi mpaka nilipomaliza elimu ya msingi ambapo nilirudi jijini Dar-es-salaam.Mpaka sasa maisha yanaendelea hapa hapa jijini Dar.
BC: Ilikuwaje ukaamua kufanya kazi ya utangazaji wa televisheni?Unaweza kukumbuka siku yako ya kwanza uliporekodi au kurusha kipindi cha televisheni “live”?
SM: Wakati nipo sekondari, ndoto yangu kubwa ilikuwa nikimaliza shule niwe Mwanasheria au Mwandishi wa Habari.Lakini baada ya kumaliza shule nikaangukia kwenye mambo ya habari. Na kikubwa zaidi nilivutiwa katika kazi ya utangazaji na dada yangu, Saida Mwilima, ambaye alikuwa mtangazaj TVT(Televisheni ya Taifa) ambayo kwa sasa inajulikana kama Tanzania Broadcasting Corporation (TBC). Nilivutiwa sana na kazi aliyokuwa akiifanya sister kwa sababu ni mtu ambaye nilikuwa naishi naye kipindi nasoma.Wakati huo yeye tayari alikuwa mtangazaji.
Yeah nakumbuka kipindi cha kwanza kwenda hewani ilikuwa mwishoni mwa mwaka 2004.Katika kipindi hicho niliwahoji AY,Ray C,Stara Thomas,Banana Zorro na Ruge Mutahaba. Hicho kilikuwa kipindi kimoja ambacho tulikuwa tunajadili kuhusu wasanii wa Kiume kuwapa support wa kike.Ruge nilimhoji katika nafasi ya Promoter anayechangia kukua kwa muziki.Hicho ndicho kilikuwa kipindi changu cha kwanza.
BC: Tuambie kidogo kuhusu kipindi chako pale Star TV.Maandalizi ya kipindi huwa yakoje na kwa mtu ambaye hajawahi kuangalia kipindi chako,nini maudhui ya kipindi?
SM: Star Tv nina vipindi viwili ambavyo nafanya kwa sasa. Cha kwanza kinaitwa Bongo Beats na cha pili kinaitwa Mcheza Kwao. Miaka miwili iliyopita niliwahi kufanya kipindi cha Afya.
Maandalizi ya kipindi ni kwamba kabla sijakutana na msanii husika kwanza huwa nafanya research(utafiti) kumhusu yeye kwa kutumia vyanzo mbalimbali. Kutokana na ninachokuwa nimepata kutoka kwenye utafiti,ndio naandaa maswali yangu. Kinachofuata baada ya hapo ni miadi ya kukutana katika location kwa ajili ya mahojiano. Kipindi cha Bongo Beats kinaruka hewani kila siku kasoro Jumapili tu. 

Imeandikwa na Na Angela Semaya wa Habari Leo
MAISHA yake sasa yamebadilika, amelazimika kuwa mtumwa wa kujificha kwa kuvaa vazi aina la Hijab ambalo anasema kwake limegeuka kuwa vazi analoliheshimu na kulithamini kwa kuwa ndio msiri wake mkubwa siku hizi, hii yote ni gharama inayotokana na moyo wake wa ujasiri na ushupavu uliotokana na kutumia kalamu yake kufichua uovu na unyanyasaji dhidi ya watu wenye ulemavu wa ngozi kwa kuuawa kwa imani za kishirikina.
Kwa walio wengi ndani na nje ya Tanzania, jina la Vicky Ntetema sio geni masikioni mwao kwani ni mwandishi mahiri wa Idhaa ya Kiswahili ya Shirika la Utangazaji la Uingereza (BBC).
Ntetema aliyezaliwa miaka 51 iliyopita ameibuka kuwa mwandishi mahiri, jasiri na shupavu baada ya kufichua siri ya kutisha kutokana na uchunguzi wa mauaji ya albino na familia zao akitaka kujua kwa undani sababu hasa za mauaji na ukatili dhidi ya albino. Hatimaye kazi yake hiyo imemuwezesha kupata Tuzo ya Ujasiri katika fani ya Uandishi wa Habari inayotolewa na International Women’s Media Foundation.
HABARI LEO Jumapili iliamua kumtafuta Vicky baada kutaka kufahamu kwa undani wa kilichomsukuma kufuatilia habari hiyo na kwa kiwango gani amefanikiwa, maisha yake kwa ujumla na kuhusiana na tuzo hiyo.
Ntetema ambaye alifanya uchunguzi wake kwa siri bila woga anasema Novemba, 2007 alipokea ujumbe wa maneno ukimuelezea kuhusu matukio ya kuuawa albino na kukatwa viungo vyao kwa imani za kishirikina, lakini awali naye hakuamini kama hicho kitu kinawezekana.
Na baada ya kufuatilia kwa muda na kujithibitishia habari hizo, alianza kuishawishi BBC, lakini walionekana kusitika wakiwa na mashaka kwamba kweli inawezekana kuwepo kwa matukio hayo? Hata hivyo anasema hakukata tamaa aliwasiliana na waandishi wengine walioko katika maeneo husika nao walimsaidia kuchunguza na kumpa taarifa zaidi.
Wakati akiendelea na uchunguzi wake aligundua kuwa waganga wa kienyeji ndio waliokuwa wakisababisha mauaji ya albino kwa kuwaambia wateja kuwa wanaweza kupata utajiri kwa kutumia viungo vya walemavu hao, ndipo alipoamua kuishawishi tena BBC huku akiendelea na uchunguzi wake kwa njia ya simu kwa kuwasiliana na watu wa Kanda ya Ziwa.
Kile alichokuwa amekusudia kukifanya na kukifichua, kilithibitishwa na Rais Jakaya Kikwete ambaye Mwezi Machi, 2008 alikemea vitendo hivyo vya kikatili dhidi ya albino na kuweka wazi kuwa tayari watu 19 walishauawa.
“Baada ya Rais kutangaza hivyo, nikasema kama kiongozi wa nchi amekemea kiasi hili na ametaja hadi maeneo yanayohusika na matukio hayo…kwa sababu ya kuwa na uhusiano mzuri na wahariri nilipeleka maombi yangu bila kusita wanisaidie ili niweze kwenda kabisa eneo husika ingawa waliniambia kwa kipindi hicho hawakuwa na bajeti,” anasema.
Dhamira yake ilimsukuma Ntetema kuchukua fedha zake za mshahara na kuamua kwenda Mwanza kwa ajili ya kuendelea na uchunguzi wake. Anasema kazi hiyo ilimlazimu kuzunguka sehemu mbalimbali hadi akajikuta ameishiwa fedha na kulazimika kuomba kwa mama yake. 
Kwa mtu yeyote ambaye anapenda fani ya utangazaji au mtu yeyote ambaye ni msikilizaji wa radio,hakuna shaka kabisa kwamba jina la Master T sio geni. Lakini Master T sio jina lake halisi. Jina alilopewa na wazazi wake ni Taji Liundi.
Yeye ni miongoni mwa watangazaji na waongoza shughuli(MCs) ambao wamejijengea jina ,kujikusanyia idadi kubwa ya mashabiki na kujijengea heshima ya aina yake katika fani hiyo maarufu. Wiki chache zijazo ndiye atakayekuwa jukwaani kusimamia shughuli nzito ya kumtafuta mrembo mpya wa Tanzania(Miss Tanzania 2009).Atashirikiana na Nancy Sumari(Miss World Africa,2005) katika zoezi hilo.
Ukimsikiliza iwe ni redioni au akiwa msimamizi wa shughuli fulani utafurahi,utajifunza,utaburudika na kisha bila shaka utakubali kwamba jamaa ana kipaji,anaipenda kazi yake,anakuthamini wewe kama binadamu na anakupenda kama msikilizaji wake. Umakini anaouweka katika kazi yake yaweza kuwa ndio siri ya mafanikio yake.
Yeye ni miongoni mwa wale watangazaji ambao licha ya kujaaliwa kuwa na sauti inayofaa kabisa kwa masuala ya utangazaji,pia ni wenye kipaji kikubwa katika masuala ya lugha.Master T anaimudu vyema lugha ya Kiswahili na pia anakipambanua vyema Kiingereza na pia huwezi kumuweka mbali na Kifaransa.Hii inamfanya akamilishe ile preamble inayosema;ukitaka kuwa mtangazaji mzuri,sharti ujitahidi sana katika masuala ya lugha.
Hivi karibuni nilipata nafasi ya kufanya naye mahojiano ambayo utayasoma hivi punde.Katika ufupi na ufasaha wa aina yake,Master T anaweka wazi masuala mbalimbali muhimu kuhusu historia ya maisha yake,heka heka za utotoni,kazi yake kama mtangazaji,harakati zake katika mwanaharakati dhidi ya ugonjwa hatari wa ukimwi,maoni yake kwa vijana na mengineyo mengi.
Je, unajua ni mkasa gani mkubwa wa kimaisha uliowahi kumkumba Master T? Unajua wazazi wake walitaka awe nani,afanye kazi gani badala ya utangazaji?Nini mtazamo wake kuhusiana na mapambano dhidi ya gonjwa la ukimwi?Fuatana nami katika mahojiano yafuatayo na Master T;
BC: Taji,kwanza kabisa asante kwa kukubali ombi langu la kufanya nawe mahojiano haya.Pole na majukumu.Mambo yanakwendaje?
MASTER T: Vyema Kaka, nami nashukuru kwa fursa hii.
BC: Natambua kwamba wengi wana ufahamu mkubwa kuhusu historia binafsi ya maisha yako.Lakini kwa faida ya wale ambao hawana habari,unaweza kuniambia kwa kifupi tu kuhusu maisha yako ya awali;ulizaliwa wapi,ukakulia wapi,ukasoma wapi na mambo kama hayo?
MASTER T: Nimezaliwa Dar, nilisoma shule ya Msingi Kisarawe pale Kariakoo kwa muda mfupi. Nikaelekea Uswiss (Switzerland) mwisho wa miaka ya 70′ ambapo niliendelea na shule ya msingi nikijifunza Kiingereza na Kifaransa. Tukahamia Zambia na dingi, nikamalizia darasa la saba.
Ikafuata Zimbabwe niliposoma form 1-2, nikaomba kurudi Bongo, nikapangiwa Ilboru Arusha, nikapiga mpaka form 3-6, nikafurahia mafunzo ya Oljoro JKT halafu Chuo cha Diplomasia mapema miaka ya 90′. 

Majuzi wakati ulimwengu unasheherekea sikukuu ya wapendanao,mtangazaji maarufu nchini Tanzania,Michael Maluwe alihitimisha siku hiyo kwa kufunga ndoa na kipenzi chake Diana katika Kanisa Katoliki Parokia ya Msimbazi jijini Dar-es-salaam.
Pichani ni Michael na Diana wakati wa tafrija iliyofanyika katika ukumbi wa Sunset uliopo Mbezi jijini Dar-es-salaam.BC inawatakia ndoa bora yenye Baraka na maelewano tele.
Picha hii ni kwa hisani ya Father Kidevu ambaye kama unamuhitaji kwa shughuli yako unaweza kumpata kupitia simu yake namba +255 755 373999.

Paschal Mayalla(pichani) mwandishi na mtangazaji maarufu hajambo na tayari yupo tena mitaani kuendelea na shughuli zake ingawa kidogo mkono bado unamsumbua.Hiyo ni kwa mujibu wa blog ya Mzee wa Sumo.
Kama mtakumbuka hivi karibuni Mayalla alipata ajali mbaya ya pikipiki alipokuwa akisafiri kuelekea Dodoma akitokea Dar-es-salaam Pichani ni Pascal Mayalla akikatisha katika mitaa jijini Dar-es-salaam kama alivyonaswa na Mzee wa Sumo.BC inaendelea kumtakia Mayalla afya njema.
Kabla ya makundi ya muziki kama vile Wanaume TMK,Das Nundaz,Nako2Nako,East Coast na mengineyo kuibuka au hata kutambulika kwenye anga za muziki nchini Tanzania yalikuwepo makundi ambayo hivi leo wengi tunakubaliana kwamba hao ndio waanzilishi wa kinachoonekana hivi leo kuwa kama vuguvugu la vijana katika kupigania haki yao ya msingi ya kujielezea(freedom of expression) katika jamii kupitia sanaa ya muziki.
Miongoni mwa makundi hayo ni lile lililotamba sana na kujulikana kama Kwanza Unit.Miongoni mwa wasanii waliokuwa wanaunda kundi hilo ni KBC au KSingo(pichani) kama alivyojulikana wakati ule na hata hivi sasa.Mbali na Kwanza Unit,wengi bado mtakuwa mnamkumbuka kama mpigania haki za Wana Hip Hop na pia miongoni mwa wanamuziki waliojitolea sana katika kuhakikisha kwamba Hip Hop ya Tanzania inaeleweka na kukubalika.Pia wengine mtamkumbuka kama DJ pale Clouds FM katika Dr.Beat.
Tukiwa bado katika kuhakikisha kwamba historia ya vuguvugu hilo na kwa ujumla historia nzima ya muziki tunaouita “wa kizazi kipya” hivi leo,haipotei na inawekwa vyema mtandaoni,hivi karibuni tulifanya mahojiano na KBC kama utakavyoyasoma hivi punde.
Je unakumbuka Kwanza Unit ilianzishwa mwaka gani?Nini yalikuwa malengo ya mwanzoni?Leo hii KBC akiangalia nyuma anaona tofauti gani au maendeleo ya aina gani katika muziki wa kizazi kipya?Nini ushauri wake kuhusu masuala ya haki miliki na utawala wa biashara ya muziki?Kwa maoni yake,nani anachangia kudidimiza muziki?Ni producer au Radio DJ?
Ili kupata majibu ya maswali hayo na mengineyo mengi,fuatana nasi katika mahojiano yafuatayo ambayo pia yana Swanglish ya aina yake katika kuleta au kuchanganya ladha kiaina; 

Kama umeshawahi kutembelea Zanzibar hivi karibuni na ukapata nafasi ya kufungulia radio yako baada ya kupata ushauri wa wenyeji,hatutoshangaa kabisa ukituambia kwamba ulisikiliza radio ya Coconut FM.Na kama ulipata muda zaidi wa kuisikiliza Coconut FM,bila shaka ulipata nafasi ya kumsikia mtangazaji Hafidh Sutti(pichani).Kipindi chake kinaitwa Africoco na huruka hewani kuanzia Jumatatu hadi Ijumaa kuanzia saa kumi na moja jioni mpaka saa tatu usiku.Tune in and feel the vibes!
Jina lake kamili ni Robert Gathecha Mongi.Wengi hivi leo tunamtambua kama Bobby.Bila shaka kabisa,Bobby ni miongoni mwa wasimamizi mahiri wa shughuli(MC),watangazaji wa radio na televisheni ambao Tanzania ya leo inaweza kujivunia.Awe anasimamia shughuli,radioni au kwenye televisheni ukimsikiliza utagundua jambo moja;anaipenda kazi yake na anaifanya kwa umakini na utulivu wa hali ya juu.Pengine utulivu huo ndio uliomfanya awe ni mtangazaji wa kutegemewa katika vituo mbalimbali vya radio nchini Tanzania na pia msimamizi wa shughuli zenye hadhi za kimataifa.
Pamoja na mafanikio na “soko” ambalo tayari alikuwa ameshajitengenezea,hivi karibuni alifanya uamuzi mgumu wa kuamua kurudi shuleni ili kunoa zaidi kipaji alichonacho.Hivi sasa anasoma katika Chuo Kikuu cha Cape Town nchini Afrika Kusini.Mbali na kuamua kurudi shule,Bobby ndio kwanza alikuwa “amepata jiko” kabla ya kuwa baba mapema baadaye.Mchanganyiko huo wa mambo ndio unaotufanya tuuite uamuzi wake wa kurudi shule kuwa mgumu!How is he handling all these?
Hivi karibuni tulipata nafasi ya kuzungumza naye machache kuhusiana na maisha yake,shule,ndoto zake na mengineyo mengi.Je anasemaje kuhusu Afrika Kusini anaposomea hivi sasa?Anasomea nini?Nini ushauri wake kwa vijana wanaoota kila siku kwenda “bondeni”?Anazungumziaje maendeleo ya muziki na filamu ya Tanzania akilinganisha na Afrika Kusini? Fuatana nasi katika mahojiano yafuatayo; 

Mbunifu wa mavazi Mama Asia Idarous (kulia)akiwa amepozi na mtangazi wa Clouds Fm,Dina Marious,wakati wa fashion show iliyokwenda kwa jina Kimasomaso hivi karibuni jijini Dar-es-salaam.Vazi alilolivaa Dina ni mojawapo ya ubunifu wa Asia Idarous.Mavazi mengi yatumikayo kwenye harusi yalionyeshwa katika show hiyo.
Photo/Ahmad Michuzi
Hakuna ubishi kwamba kipindi cha PowerBreakfast kinachorushwa na radio ya Clouds FM ni mojawapo ya vipindi vya radio vyenye wapenzi na wasikilizaji wengi nchini Tanzania.
Hivyo basi haishangazi kwamba hivi karibuni watangazaji wawili wa kipindi hicho waliokuwa wamezoeleka,Masoud Kipanya(KP) na Fina Mango, walipopotea hewani maswali mengi yaliibuka.Wako wapi KP na Fina?Maoni na e-mails zikarushwa kwetu tukiombwa kuwatafuta na kujua nini kimetokea na kama wapo likizo tu au inakuwaje?
Wakati tukifanya juhudi za kujua nini kimetokea,blog maarufu ya Michuzi ikaandika habari iliyokuwa na kichwa cha habari Fina Mango na Masudi Kipanya niaje?Mjadala ukazuka.Kwa bahati nzuri,nasi tukawa tumebahatika kumpata mhusika mmojawapo yaani Masoud Kipanya(KP) ambaye hakusita kutupa yake machache kuhusu nini kimetokea au kilitokea,yuko wapi,anafanya nini nk.Anasisitiza kwamba nia yake ni kutoa ufafanuzi(kwa upande wake) ili watu wasiendelee kujenga picha ambazo pengine hazitakiwi kujengwa wala hazipo.
Je PowerBreakfast ya Masoud na Fina ndio imefikia kikomo? Je ni kweli kwamba masuala ya mshahara ndio yamesababisha wapotee hewani?Fuatana nasi katika mahojiano haya mafupi;
BC: KP,kwa muda wa wiki kadhaa sasa kumekuwepo na tetesi,minong’ono,udaku nk kuhusu kuwepo au kutokuwepo kwenu katika kipindi chenu maarufu cha PowerBreakfast kupitia CloudsFM.Hivi leo,blog ya Michuzi(bila shaka umesoma kilichoandikwa) iliweka kidogo kuhusiana na kilichokuwa kinazungumzwa mitaani. Je ukweli uko wapi? Upo au haupo tena katika PowerBreakfast?Nini kimetokea? 




sending...











